Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022

Hon. Tabasamu Hamisi Hussein Mwagao

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sengerema

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Nami nitoe mchango wangu katika sekta hii ya nishati na madini. Ni kwamba, pamoja na kwamba mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, na-declare interest kwamba pia mimi ni mfanyabiashara wa mafuta ya reja reja hapa nchini na pia ni mchimbaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaishukuru sana Wizara ya Nishati kupitia TANESCO na REA kuwa wasikivu kwa kukubali kupitia upya mpango wa uunganishwaji umeme majumbani kutoka shilingi 360,000 kurudi shilingi 27,000 katika maeneo maalumu ya vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili ni kwamba, kuna miji ambayo inaonesha ni Majiji, Manispaa, lakini Halmashauri za Wilaya na Halmashauri za Miji, wana maeneo yao ambayo yako vijijini. Kwa mfano, Dodoma hapa kuna maeneo ambayo yako vijijini kabisa, lakini yanasomeka yako katika Jiji la Dodoma. Kuna maeneo yako Mwanza yanaonekana yako Nyamagana, lakini ukitoka Nyamagana kwenda huko ni kilometa zaidi ya 30. Pia kuna maeneo yako kwa mfano Sengerema Mjini, lakini zinasomeka ni Kata za Sengerema Mjini lakini ni kilometa zaidi ya 30 mpaka 60 ndiyo unafika katika maeneo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa hili ambalo wamelichukua watu wa Wizara kurudi upya kupitia maeneo haya kwa kutushirikisha Waheshimiwa Wabunge, Waheshimiwa Madiwani na Wakuu wa Wilaya kupita kwenye maeneo hayo kurudia upya na kushusha bei hizo, tunaipongeza sana Wizara kwa jambo hilo. Naomba waharakishe, wananchi wetu wamekaa, wanasubiri kuunganishiwa umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili, ni umeme unaoenda kuunganisha vijiji na vijiji, wilaya na mikoa. Maeneo haya wana ujenzi wa transmission. Haya maeneo miradi iko mingi sana. Kwa mfano, miradi iliyopo tu ni zaidi ya 26, na yote umilikishaji wake hatujui je, ni matatizo ya fedha kutoka Wizara ya Fedha? Hatujui tatizo ni nini? Ni Makandarasi! Sasa tunaomba Wizara ifanye haraka kuharakisha huu ujenzi wa hizi transmission unakamilika, wananchi wanaohitaji umeme waweze kupata.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, kuna maeneo ya migodi. Tunaishukuru sana Wizara kwamba kupitia REA, migodi yote mikubwa na midogo inaanza kupelekewa umeme. Kwa hiyo, hili tunaipongeza sana, lakini bado hawajaharakisha upelekaji wa umeme migodini, bado watu wanatumia diesel.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, kama kwangu Sengerema tuna ujenzi mkubwa wa Mgodi wa Sotta Mining, ni zaidi ya kilometa 38 hadi 40 kufika kule kutokea Sengerema Mjini. Ila iliko submission ya TANESCO kule Geita kutoka Mpomvu kuja Sengerema ni zaidi ya kilometa 60. Sasa tunaomba watuharakishie kutujengea line mpya kwa ajili ya mgodi huo. Kwa sababu mgodi ukishaanza kufanya kazi na umeme haupo, na kuna umeme mwingine, waangalie njia rahisi kutokea Kakola - Geita kupitia Msalala - Karumwa au watoe Geita. Kwa hiyo, tunamwomba Waziri katika jambo hili aharakishe kwenye maeneo ya migodi mikubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la vinasaba limekuwa ni tatizo kubwa katika nchi hii. Tulipiga kelele hapa, vinasaba vilikuwa bei kubwa, tulizungumza na baadaye vinasaba vikashushwa bei mpaka Shilingi saba kwa cubic meter za lita za mafuta. Pamoja na hali hiyo, hivi tunavyozungumza uwekaji wa vinasaba unalalamikiwa na wafanyabiashara wa reja reja walioko katika Mikoa. Wao wanatuma madereva wao wanakuja kupakia katika malori, lakini vinasaba vinawekwa kama seal. Ni jambo ambalo katika ma-depot hawajaweka wazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hawajaweka wazi kuonesha ma-depot yale, lita 7,000 inawekewa miligramu ngapi? Lita 10,000 miligramu ngapi?

Waweke vibao vikubwa. Wakishamaliza kuweka vinasaba, tunaiomba sana Wizara, kwa sababu ni Wizara mbili; Wizara ya Nishati na Wizara ya Biashara na Viwanda ambao wako TBS, na wao wafunge seal. Kwa hiyo wafunge seal watu wa depot na watu wa TBS, Kwa sababu suala la vinasaba linabeba uchumi wa nchi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuondoa dumping katika nchi hii ni kwamba lazima vinasaba sasa viwekwe kwa seal. Halafu vinasaba kutokea huko vinakotoka visindikizwe ama na Jeshi au na watu wa usalama wa Taifa. Jamani suala la vinasaba kuuzwa mitaani ni suala la hatari katika uchumi wa nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la demurrage charges, Mwenyekiti wa Kamati amelizungumza jambo hili kwa ukubwa kutokana na muda. Hata hivyo, suala la miundombinu toka tunaingia Bungeni hapa tunazungumzia suala la miundombinu. Suala la mafuta limekuwa na changamoto kubwa kwa sababu linachangia Wizara tano. Wizara tano zote hizi zinamulika katika eneo lile.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna Wizara ya Fedha. Kwa mfano, kama sasa hivi uagizaji wa mafuta, meli zinafika hapa zinashindwa kulipiwa kwa sababu ucheleweshaji wa Dola kutoka Benki Kuu unakuwa ni tatizo. Tunaiomba sana Wizara ya Fedha iharakishe mpango wa uagizaji mafuta linalobeba uchumi wa nchi. Tunahitaji katika sekta hiyo zaidi ya Dola milioni 700 kwa miezi mitatu. Sasa hili ni jambo ambalo linachangia waagizaji wa mafuta kupata demurrage charges kule, nao wanaileta huku kwa mlaji. Mtu wa mwisho anayekuja kuumia ni mwananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, flow meter zinasimamiwa na watu wa Wizara ya Biashara. Flow meter nne ziko kule Kigamboni, ni mbovu leo mwaka wa nne hazitengenezwi. Hata hivyo, suala la ushushaji wa mafuta linasimamiwa na Wizara ya Ujenzi (Bandari). Sasa pale na penyewe ushushaji wa mafuta…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)