Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

Hon. Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Nami niungane na Wabunge wengine wote ambao wamepongeza Kamati hizi mbili na kipekee nipongeze Kamati yangu ya Utawala na Serikali za Mitaa kupitia kwa Mwenyekiti Mheshimiwa Chaurembo na Wabunge wote kwa taarifa hii nzuri, ya kina, ambayo kwa kweli maudhui yake yatatusaidia sana pamoja na ushauri na maoni mbalimbali ambayo wameweza kuyatoa.

Mheshimiwa Spika, nikienda katika mapendekezo yaliyosomwa na Mwenyekiti, lile la kufanya uchunguzi wa kina kuhusiana na suala zima la migogoro ya ardhi lile lililoko katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma. Nipende kusema kwamba tunapokea mapendekezo haya, tutayatekeleza na vile vile tutazingatia wakati wa kufanya uchunguzi huu wa kina, kuhakikisha kwamba watumishi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma hawahusiki katika timu itakayofanya uchunguzi. Hata hivyo tumewasikia hapa Wabunge lakini pia Kamati ikieleza kwa kirefu kuhusiana na suala hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa TARURA, tunashukuru kwa namna ambavyo maoni na mapendekezo yaliyojitokeza na hasa kutokana na suala zima la ufinyu wa bajeti. Nipende kusema kwamba suala hili tumelipokea, tumekuwa tukiendelea kuwasiliana na wenzetu wa Wizara ya Fedha, tunalifanyia kazi ili kuendelea kuona ni kwa namna gani TARURA itaweza kuongezewa fedha nyingi zaidi ili kuhakikisha kwamba wanaweza kuwa na bajeti inayowatosheleza. Kwani kwa sasa tuna bajeti ya shilingi bilioni 838 na mahitaji bado ni makubwa. Ukiangalia bado tuna vikwazo vingi katika wilaya zetu na bado tunahitaji fedha nyingi kwa ajili ya kufungua na kuondoa vikwazo hivyo mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kimkakati. Kwanza ningependa kusema, hakuna upendeleo katika utekelezaji wa miradi hii na pili, nadhani kuna mkanganyiko kidogo, wako ambao walikuwa wanasema kwamba miradi hii haiangalii halmashauri ambazo ni ndogo ndogo. Nipende tu kusema kwamba miradi hii ya kimkakati inatekelezwa kwa vigezo mbalimbali. Tumekuwa tukishirikiana na Wizara ya Fedha katika kuhakikisha kwamba miradi inayoibuliwa na halmashauri ile ambayo inakidhi vigezo basi ndiyo miradi ile ambayo inaweza kuzingatiwa.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo changamoto kubwa ambayo tuliiona, unajikuta katika baadhi ya halmashauri walikuwa Maafisa Mipango wengine hawana uwezo mkubwa sana wa kuandaa maandiko ya miradi hii mikubwa ya kimkakati na ndio maana pale nilisikia hoja ya nadhani Mheshimiwa Kwagilwa, akisema kwamba nyie hamna uwezo wa kuandaa sijui moja, mbili, tatu, sijui mpaka muandaliwe mwongozo.

Mheshimiwa Spika, siyo kwamba tumeandaliwa mwongozo, ni pamoja na kutoa mafunzo kwa Maafisa Mipango wetu wa Halmashauri ili waweze kuwa na uwezo mkubwa zaidi wa kuandaa maandiko zana, kufanya upembuzi yakinifu pamoja na usanifu wenyewe pamoja na masuala mengine kadha wa kadha. Hii ni kuhakikisha kwamba miradi itakayopelekwa Wizara ya Fedha ili iweze kuzingatiwa, basi kweli iwe ni miradi ambayo itakuja kuleta thamani halisi ya fedha badala ya kuwa tu na miradi yoyote kama ambayo walikuwa wanakopiana zaidi kama miradi ya stendi na miradi ya masoko.

Mhesimiwa Spika, unakuta Halmashauri kama ya Ukerewe kumbe huenda wangeweza kuja na mradi mkakati wa kuweza kutengeneza chakula cha Samaki, mradi wa kutotolesha vifaranga vya Samaki, nyavu za kuvulia samaki na vitu vingine kadha wa kadha. Kwa hiyo, siyo kwamba tumekuwa tukipendelea au kutafuta watu ambao hawahitajiki.

Mheshimiwa Spika, siyo hilo tu, huu mwongozo tunaandaa pia na suala zima la special purpose vehicle. Nitoe tu mfano wa Halmashauri ya Wilaya ya Maswa, pale wana Kiwanda cha Chaki pamoja na Halmashauri nyingine. Sasa je, wanapokuwa wamefungua kampuni, au wanapotekeleza mradi wa aina hiyo, wautekeleze kwa mfumo gani?

Mheshimiwa Spika, na lenyewe hilo ukiangalia dhana nzima ya suala la special purpose vehicle suala jipya kidogo kwetu. Kwa hiyo, ni vema pia na lenyewe tupate maelekezo ya kina kupitia mwongozo ambao Halmashauri zetu zitaweza kuuelewa na kuweza kujua ni kwa namna gani wanaweza kutekeleza. Kwa hiyo, kwenye hili tutaendelea nalo na siyo kwamba watu hawana uwezo wa kuweza kufanya hilo, lakini tunataka tujenge uwezo mkubwa zaidi.

Mheshimiwa Spika, naomba Mungu niweze kupata muda wa kutosha kwa suala la upungufu wa Walimu. Wabunge wamelieleza kwa uzito mkubwa. Ukiangalia tuna upungufu wa walimu zaidi ya 238,000. Tunashukuru kwamba kupitia jitihada za Mheshimiwa Rais, ndani ya muda mfupi sana tangu ameingia, utaona alipoingia tu tuliweza kupata kibali cha kuajiri walimu 9,800. Siyo hilo tu, tunaendelea na jitihada hizo na kuhakikisha kwamba tunaendelea kujairi kwa mujibu wa mahitaji na kwa kuzingatia uwezo wa kifedha wa Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mkenda ataongea kwa kina kuhusiana na Mwongozo wa Walimu wanaojitolea. Tumefurahi kuona kwamba Wabunge pia wameona hili litakuwa na mvuto na litaweza kusaidia sana katika kupunguza changamoto ya Walimu wetu. Pia wamejitokeza wadau wengi ambao wako tayari kushirikiana na Serikali katika kuona ni kwa namna gani tutakapoanza sasa kuendelea kuweka mfumo sahihi namna gani Walimu wanaojitolea waweze kujitolea, wako tayari kuweza kutuunga mkono. Kwenye hili, tayari tumeshaanza mashauriano na Mheshimiwa Dkt. Jakaya Kikwete pamoja na UNICEF na wengine pia ambao wamekuwa tayari kuunga mkono jitihada hizi.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa kuna hoja ya DMDP II na kwamba mradi umechelewa. Napenda tu kumweleza Mheshimiwa Bonnah, Wabunge wa Dar es Salaam na wengine ambao wanaufuatilia mradi huu, tayari concept note tulishaiandika, tumeshaiwasilisha Benki ya Dunia, na kwa sasa tunaendelea na majadiliano na na Benki ya Dunia kupitia Wizara yetu ya Fedha.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa mradi wa TACTIC, na yenyewe pia ilijitokeza kwamba ni miji ile ile inayopewa miradi ya mikakati, na wenyewe tena wanapewa mradi huo wa uboreshaji wa miundombinu ya miji ya kimkakati ile 45. Napenda kusema kwamba miradi hii iliibuliwa kwa kufuata vigezo na hasa vigezo vya kupata wanufaika hivi vilitokana na taarifa ya idadi ya watu, na pia ongezeko la ukuaji wa idadi ya watu kwa mujibu wa taarifa ya Tume yetu ya Takwimu ya NBS na tumeweza kuzingatia hilo.

Mheshimiwa Spika, kuhusu kwa nini mradi umechelewa? Kulikuwa kuna majadiliano mbalimbali na Benki ya Dunia. Napenda kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge, na leo hii Mheshimiwa Naibu Waziri Silinde ameweza kujibu maswali hapa kwamba kuanzia mwaka huu wa fedha tutaanza na wale waliopangiwa katika awamu ya kwanza miji 12, awamu ya pili tuna miji 15 na awamu ya tatu tutakuwa na miji 18. Niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge wote, ifikapo 2025 mradi huu wa TACTIC kwa miji hiyo 45 yote itakuwa imeshatekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwatoe hofu kwa wale ambao wako katika makundi ya mwisho. Anayecheka mwisho ndiye anayecheka sana. Kwa hiyo, kama kuna hofu nyinginezo huko, wale ambao mko mwishoni mwishoni pia naamini mtaweza kucheka zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa kulikuwa kuna ile hoja ya madarasa 8,000 kuhamishwa, nadhani ilikuwa hoja ya Mheshimiwa Kunti. Napenda kutoa ufafanuzi kidogo kwenye hili. Katika yale madarasa 8,000 tulikuwa tunahangaika na changamoto ya wanafunzi 1,076,037 ambao wameanza Kidato cha Kwanza tarehe 9 mwezi Januari. Tulikuwa tuna siku 75 tu za kuweza kutekeleza mradi. Sasa kweli watu walituletea shule nyingine mpya, kwa nini badala ya madarasa haya manne, na haya manne kwa shule hii tunisiyaunganishe nipate madarasa nane nikajenge shule mpya moja? Kwa nini limeshindikana?

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Dakika moja malizia.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, tulipata mapendekezo ya shule 465, na ili shule iwe kamili inatakiwa iwe na walimu siyo chini ya 11. Kwa hiyo, tulitakiwa tuwe na Walimu wapya zaidi ya 5,115 ndani ya miezi miwili. Wote tunajua taratibu za ajira na masuala mengine, kwa muda huo isingeweza kupatikana, lakini vilevile miundombinu mingine siyo madarasa tu, kuna maktaba, maabara, pamoja na mambo mengine.

Mheshimiwa Spika, niwatoe hofu kwamba kupitia mradi wetu wa SEQUIP Februari hii mpaka June tutajenga shule 184 na tutaendelea kujenga shule nyingine zote za kata mpaka tufikishe idadi ya shule 1,000. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja hii ya Kamati na mapendekezo yote yaliyopendekezwa tutayatekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunashukuru sana. (Makofi)