Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

Hon. Dr. Amandus Julius Chinguile

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nachingwea

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na mimi kwa kunipa nafasi. Mimi ni mjumbe wa Kamati ya Utawala na Serikali za Mitaa. Awali niunge mkono maoni ya Kamati zote mbili kwa asilimia mia moja.

Mheshimiwa Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa namna ambavyo anafanya bidii ya kuhakikisha maisha bora ya Watanzania yanendelea kupatikana.

Mheshimiwa Spika, nimpongeze pia Mheshimiwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na timu yake kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wameendelea kuifanya. Wakati wamekuja mbele ya Kamati tuliendelea kuridhishwa sana na utekelezaji wa maazimio ya Bunge lako. Pia nimpongeze Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI na timu yake kwa kazi kubwa na nzuri, kwakweli kazi zinaendelea kufanyika.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo ninanyongeza ya ushauri kwenye maeneo kadhaa kwa sababu maazimio haya na maoni ya Kamati na mimi ni sehemu yake.

Mheshimiwa Spika,najielekeza kwenye TARURA, tuendelee kuwapongeza, wenzetu TARURA wanafanya kazo kubwa na nzuri kwelikweli katika maeneo ya nchi yetu. Hata hivyo bado niendelee kuomba kwa Serikali waendelee kuwezeshwa kifedha, bajeti yao iongezwe na hasa kwenye eneo la dharula. Inapotokea Msimu wa mvua hali inakuwa ni ngumu na wanakuwa na kazi kubwa kwelikweli. Wakiwezeshwa wataendelea kuimarisha utoaji wa huduma, na kwa kweli miundo mbinu kwenye maeneo yetu itaendelea kuimarika.

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo hilo hilo la TARURA tuliendelea kushauri na bado naendelea kusisitiza kuishauri Serikali; bado eneo la manunuzi liendelee kusogezwa namna ambavyo itawezekana kufika kwenye eneo la Wilaya. Kwa namna ilivyo sasa hivi manunuzi na tendering hufanyiwa kwenye ngazi ya mkoa. Wale mameneja wa TARURA walioko kule wilayani kwenye halmashauri wanabaki kama PS, hawana mamlaka kwa hawa wakandarasi kwa kuwa tayari wamepewa tender kutoka huko mkoani. Sasa matokeo yake wanakosa namna ya kusimamiwa vizuri kule kwenye halmashauri; na hata sisi tulioko kule tunashindwa namna ya kuwasimamia vizuri. Lakini kazi inayofanyika na TARURA ni nzuri na wanaendelea kufanya kazi kwenye mazingira hayo.

Mheshimiwa Spika, naomba nitoke hapo nijielekeze kwenye mradi wa ujenzi wa Shule za Sekondari. Niipongeze sana Serikali kwa uamuzi huu; na kweli hizi shule ni nzuri na zinapendeza. Hata ukifika kule kwenye jimbo langu la pembezoni la Nachingwea unakuta shule iliyojengwa kwa mradi huu wa SEQUIP inapendeza kweli kweli, tunaishukuru Serikali.

Mheshimiwa Spika, lakini bado na mimi niendelee kusisitiza kwenye eneo lile la gharama halisi ya hizi shule. Milioni 470 yako maeneo mengine huwezi kumaliza uhitaji wa hiyo shule. Bado tuendelee kuangalia kulingana na eneo. Huwezi kufananisha eneo la Dar Es Salaam na eneo la Nachingwea au kule Tunduru. Niiombe sana Serikali ipitie upya jambo hilo, na kama ni suala ambalo linaweza likarekebishika basi tuweze kupata ufumbuzi wa haraka.

Mheshimiwa Spika, nijielekeze kwenye mchango tena kwenye Kamati ya Huduma. Nimepitia vizuri hapa, lakini yapo mapendekezo kadhaa na maoni ambayo Kamati wametoa. Ni ukweli usiopingika kwamba kwenye ukatili wa kijinsia wako baadhi ya wanaume na wenyewe wanapata kadhia hiyo. Kwa sababu ya kitamaduni ya Kiafrika na Kitanzania hatuna mahala pa kulalamika, yawezekana wengine tuko ndani humu lakikini hakuna anayeweza kutuzungumzia.

Mheshimiwa Spika, kwenye mapendekezo ya Kamati na mimi naomba nipendekeze nyongeza kwenye ukurasa wa 41(i) kuishauri Serikali, kufanya utafiti wa kina kujua nini chanzo cha ongezeko la ukatili wa kijinsia nchini hususani kwa wanawake na watoto. Hapa iongezwe na wanaume, kwa sababu tunachoshauri hapa ni kufanya utafiti. Kama bado wako wanaume ambao nao wanakumbwa na mazira haya tujue.

Mheshimiwa Spika, hii inaweza ikawa ni kichekesho lakini yapo. Wapo wanaopigwa, wapo wanaofungiwa na manyanyaso mengine kadha wa kadha. Lakini ugumu wa kujitokeza na kusema mimi nimefanyiwa haya mazira kwa sababu ya tamaduni zile zile za Kitanzania na Kiafrika tunashindwa kufanya hivyo. Lakini huo ndio uhalisia; na kwa sababu hapa tunachoshauri ni kwenda kufanya utafiti basi na hilo ipendeze liingie kwenye utafiti ili watuletee sasa tafiti zinasema nini. Hilo jambo lipo sawa basi kama halipo tutamshukuru Mungu, tutaendelea na lile lile kwamba wanawake na Watoto.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naendelea kurudia tena yale maoni ya Kamati na mimi ni sehemu yake. Kwa hiyo naunga mkono kwa asilimia mia moja. Nakushukuru sana. (Makofi)