Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

Hon. Kasalali Emmanuel Mageni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sumve

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii, lakini kabla sijachangia ninazipongeza Kamati zote mbili kwa uwasilishaji mzuri na ushauri mzuri kwa Bunge, nadhani imekuwa ni mwanga mzuri wa kutusaidia kulijadili jambo hili kwa upana wake.

Mheshimiwa Spika, nadhani sote ni mashahidi katika wakati huu wa Serikali ya Awamu ya Sita ni wakati pekee kwa uzoefu wangu mimi wa kuishi Tanzania ambapo nimeona pesa nyingi sana za miradi ya maendeleo zinapelekwa kwenye Halmashauri za Majiji, Manispaa, Miji na Wilaya. Pesa zinazohusu madarasa, pesa zinazohusu vituo vya afya, zahanati, zinapelekwa kwa wingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sote hapa ni mashahidi na ni Madiwani huko kwenye Halmashauri zetu, hata Watumishi wetu wameingiwa na ugumu kwenye kusimamia pesa hizo nyingi zinazokuja. Sasa mimi nimesimama kuchangia kwenye Kamati hii ya Utawala na Serikali za Mitaa pamoja na Huduma za Jamii, nataka kujikita kwenye kutoa ushauri wangu wa namna bora ya kusimamia pesa za maendeleo ambazo zinapelekwa kwenye Halmashauri zetu. Pesa nyingi ambazo zikisimamiwa vizuri zitaacha historia isiyosahaulika kwenye nchi yetu na zitampa heshima kubwa sana Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sote tunafahamu binadamu yeyote anapopewa pesa hapendi sana kusimamiwa, anapenda aachwe afanye vile anavyoona yeye. Na pesa daima ni sabuni ya roho, kila mmoja akiona pesa anatamani kuitumia yeye ndio maana zikawekwa taratibu za usimamizi. Ndiyo maana kwenye level ya Serikali Kuu lipo Bunge tunaisimamia Serikali, lakini kwenye level ya Halmashauri yapo Mabaraza ya Madiwani yanasimamia zile Halmashauri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa nini nasema Mabaraza ya Madiwani hapa leo?

Mheshimiwa Spika, Mabaraza ya Madiwani kusimamia kwake Halmashauri wanasimamia kupitia ziara mbalimbali, kupitia vikao, miradi inapopelekwa kule inaenda kukaguliwa na Madiwani kwenye ziara. Hivi ninavyoongea kuna nafasi ambayo imetolewa na Wizara yetu pendwa ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa kupitia maelekezo mbalimbali na nyaraka mbalimbali, Halmashauri za Wilaya badala ya kusimamiwa kwa nguvu zote na Madiwani utendaji wa Madiwani, Halmashauri za Wilaya sasa zinaendeshwa kwa hisani za Wakurugenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hivi Waheshimiwa Madiwani kwenye baadhi ya Halmashauri za Wilaya, ikiwepo ya Kwimba, Kamati ile ya Huduma ya Jamii ambayo ilikuwa Elimu, Afya na Maji na Kamati ya Uchumi hazifanyi kabisa ziara kwa sababu, Halmashauri zinasema kuna nafasi inatoka kwenye kanuni ya kuwafanya wao waamue kama Madiwani waende ziara au wasiende. Kwa hiyo, hela zote tunazopeleka zile Kamati za Madiwani hazikagui hizo pesa, sasa hii ni hatari kubwa kuacha pesa zetu zisisimamiwe huko vizuri! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mbali na hayo Halmashauri zetu ili zisimamiwe vizuri, hapa nilishawahi kusema na leo ninarudia, ukiwa na mali yako unaweka mlinzi aliyeshiba. Ukiweka mlinzi mwenye njaa una hatari ya kuibiwa kila siku. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kutokana na nafasi hii kwa ruhusa yako naomba nisome waraka ambao ulitoka Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa kwenda kwenye Halmashauri ambao unatoa loop. Unasema hivi, katika kipengele cha nne; “Posho za kujikimu za Waheshimiwa Madiwani zinapaswa kulipwa kwa kuzingatia mahali, sehemu na umbali Diwani anakotoka. Msingi mkubwa wa kuzingatiwa ni kuwa Diwani husika sharti awe amesafiri na kulala nje ya makazi yake ili aweze kuhudhuria kikao kinachofuata.” (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sharti hili limekuwa likitumika vibaya, yaani Mkurugenzi ndio anaamua Diwani amelala au hajalala. Mwisho wa siku sasa Mabaraza ya Madiwani, Madiwani wanapoenda kwenye vikao vyao wanalipwa kwa hisani, yaani kitu kinaitwa mahusiano. Wasipokuwa na mahusiano mazuri na Mkurugenzi hawalipwi vile inavyotakiwa. Zile per diem za Madiwani zinaamuliwa kwa mahusiano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa ninaomba Bunge lako Tukufu kupitia Kamati hii tumuelekeze Mheshimiwa Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa atoe maelekezo mahsusi kuliko maelekezo kama haya yanayotoa loop hole ya watu kucheza na Mabaraza ya Madiwani yashindwe kusimamia Halmashauri zetu. Atoe maelekezo mahsusi yanayozielekeza Halmashauri za Wilaya, Manispaa na Majiji kulipa pesa kwa Madiwani kwa kuzingatia uhalisia kwamba, Madiwani wengi wanapokuja, hasa kwenye Halmashauri za Wilaya, wengi wanalala.

Mheshimiwa Spika, huwezi kusema Diwani wa Sumve um-judge kwa umbali wakati miundombinu yake haimruhusu, hakuna daladala, akishatoka kule akamaliza kikao saa 12 lazima alale Ngudu. Sasa unapomwambia kwamba, umbali wake na Halmashauri zetu hizi tunaanza kuweka, yaani imekuwa ni kwamba, ni hisani za watu wanafikiria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba Bunge lako lielekeze Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa itoe waraka mahsusi ambao unaondoa mkanganyiko wa ulipaji wa posho za kulala za Madiwani kwenye Halmashauri za Wilaya na Miji ambazo kwa asilimia kubwa Madiwani wanapoenda kwenye vikao wanaenda wanalala ili waweze kukaa kwenye vikao wakiwa na amani, wasimamie pesa zetu vizuri ili sisi tunapopeleka pesa kule ziwe salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nadhani jambo hili tumekuwa tukilisema mara kwa mara kuhusu usimamizi wa Halmashauri kwa kuboresha maslahi ya Madiwani…

SPIKA: Sekunde 30, malizia.

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Spika, naomba sasa Bunge lako Tukufu litoe maelekezo mahsusi na tumuombe Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa atoe maelekezo mahsui kwenye Halmashauri ambayo yataondoa mkanganyiko wa ulipaji wa wasimamizi wetu wa Halmashauri. Nakushukuru sana. (Makofi)