Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

Hon. Husna Juma Sekiboko

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa nafasi hii. Nami nianze kwa kuzipongeza Kamati zote mbili na taarifa zilizowasilishwa, lakini nimpongeze zaidi Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa anayoifanya katika kuwaletea maendeleo wananchi wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, namuomba Mwenyezi Mungu anisaidie lakini leo nina jambo moja tu mahsusi kama nitajaliwa kuongea na lingine basi ni kwa rehema za Mwenyezi Mungu. Jambo lenyewe ni ubora wa elimu yetu.

Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2022 inaonesha tumeendelea kupata matokeo mabaya hasa kwenye mitihani ya watoto ya sayansi. Tumeendelea kuwa na matokeo mabaya hasa kwenye shule zetu za Serikali. Tumeendelea kuwa na matokeo mabaya ya sayansi lakini tumeendelea kuwa na upungufu mkubwa wa walimu wa sayansi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwaka 2022 tulihitaji kuwa na walimu 19,216 wa hesabu, tulifanikiwa kupata Walimu 5,537. Tunao upungufu wa Walimu 13,679 kwa asilimia, tuna upungufu wa Walimu kwa asilimia 71, huo upungufu wa walimu asilimia 71 umesababisha watoto kufeli somo la hesabu kwa asilimia 83.

Mheshimiwa Spika, suala la somo la fizikia, (physics) tulihitaji kuwa na Walimu Elfu Kumi na Sita na kidogo, tumekuwa na walimu elfu tatu na kidogo. Tumekuwa na upungufu wa walimu elfu kumi na mbili na kidogo, tumepata upungufu kwa asilimia 77. Failure ambayo imesababishwa na huo upungufu wa Walimu ni asilimia 82, tunawekeza kwenye standard gauge, tunawekeza kwenye ujenzi wa barabara kubwa kubwa fly overs tunawekeza kwenye ujenzi wa mahospitali ya rufaa chungu nzima, tumewekeza kwenye miundombinu mizuri sana excellent nani anakwenda kuihudumia? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumewekeza vya kutosha kwenye majengo na mimi nataka nimpongeze sana mama yangu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan tumejennga sana madarasa, mama umefanya kazi kubwa mno kwenye ujenzi wa madarasa! Ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge tuishauri Serikali sasa wageukie kuajiri walimu namna pekee itakayo tutoa kwenye hii failure ni kusaidia kuajiri walimu walioko mtaani waende watusaidie kuwafundisha watoto.

Mheshimiwa Spika, mwaka jana wa 2022, walimu walioomba kuajiriwa TAMISEMI walikuwa 165,948 tumeajiri walimu takribani 16,000 kutoka kwenye 165,948. Katika hao walimu 30,000 ni Walimu wa Sayansi walioajiriwa ni takribani walimu 5000 wa sayansi kutoka kwenye walimu 30,000. Tunataka muujiza, hatutatoka kwenye hizi failures kama hatutawekeza vya kutosha katika kuajiri walimu kwenye nchi hii. Tutaondoa namna ya kuwa grade shule zilizofanya vizuri na ambazo hazijafanya vizuri, tutaondoa wala haina shida. Lakini haitakuwa suluhisho la kufuta sifuri mashuleni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukizungumzia walimu kuna principle inasema kitu chochote kisipotumika kwa muda mrefu kinakuwa butu hata kisu usipokitumia kwa muda mrefu lazima wakati wa kukitumia lazima ukinoe kwanza. Tunaajiri leo walimu waliohitimu 2015 tunawapeleka shule wanaenda kufundisha hakuna programu yoyote ya kuwanoa, kuwakumbusha kuwarudisha kwenye nafasi yao ya kwenda ku-perform vizuri, hatufanyi hivyo! Mbaya zaidi leo kwa taarifa nilizonazo mara ya mwisho tumewaajiri walimu wa sayansi mwisho tuliishia 2017.

Mheshimiwa Spika, mwaka 2018, mwaka 2019, mwaka 2020, mwaka 2021na mwaka 2022 miaka mitano au sita hawajaariwa. Hii miaka ya karibuni wote wako mtaani hawajaajiriwa, sasa utakavyowaajiri hawa watu mtu ambaye ameshinda kwenye kijiwe cha kahawa ama cha bodaboda kwa miaka mitano mfululizo unampeleka shuleni akafanye muujiza gani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, namna ya kwenda kuboresha hili nataka niishauri Serikali, walimu walioko mtaani hawa zaidi ya laki moja. Tunaupungufu mkubwa kuliko hawa walimu walioko mtaani, tukifanya hili tutasaidia Serikali katika mambo mawili. Jambo la kwanza ni kuendelea kuwafanya wawe active, pili tutakuwa tumepunguza pia huo upungufu wa walimu ambao umesababisha hii failure ambayo tunaiona sasa.

Mheshimiwa Spika, jambo lenyewe tuajiri kutumia ajira za muda mfupi. Kwa sababu nchi yetu tunaijua, bado ni nchi inaendelea bado ni nchi maskini uwezo wa kutoa ajira zote hizo kwa wakati mmoja nchi yetu haiwezi tunafanya shughuli nyingine nyingi ambazo zote tunazihitaji. Sasa kwa sababu ya upungufu wa fedha bajeti ndogo tuliyonayo tuwapeleke hawa Walimu wakafundishe kwa maana ya ajira za mkataba za muda mfupi mfupi. Tukiwatawanya kwenye mashule huko kwanza tumepunguza upungufu wa Walimu lakini at the same time tumewasaidia kuimarisha wasisahau, wasibweteke, wasiwe butu na mwisho wa siku kutusaidia katika kuongeza ufaulu mashuleni.

Mheshimiwa Spika,sisi tulitembelea Chuo cha Mwalimu Nyerere pale Butiama. Tulikuta kwa mika kumi na tatu chuo kina watumishi zaidi ya arobaini. Kwa miaka
13 hakijafanya udahili na wale watumishi wanalipwa mishahara ya Serikali OC zinakwenda zinatumika lakini tukija tuna upungufu wa walimu wa hesabu tuna maprofesa tumewaweka pale for 13 years hawajafanya kazi.

Mheshimiwa Spika, tunakwenda wapi? Hebu twende na vipaumbele kama Taifa. Kama lengo letu ni kuisaidia Nchi hii maskini ipige hatua lazima tujiulize changamoto zetu sisi ni zipi? Changamoto yetu kubwa ni elimu, elimu, elimu! Tunahitaji kuelimisha watu wetu kwanza wajitegemee. Tumezoea kuwaambia watu jamani someni mjiajiri, well and good! Tunaweza kujiajiri, hebu niambie mimi Mwalimu wa Historia nimefundishwa niende nikamfundishe mtoto Zinjanthropus ni nini? Niende nikamfundishe mtoto evolution of man ni nini? Haya sijaajiriwa mimi niende nikajiajiri kwenye nini? Wapi nitapewa kazi ya kuelezea evolution of man… wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, namna pekee ya kunitumia mimi ni kunipa nafasi ya kwenda kufundisha hiyo evolution of man. Mtume Mohamed Swalala walah wasaalam katika maisha yake alikutana na swahaba mmoja aliyekuwa na busara sana, aliona Mtume anaishi vizuri sana na watu akamfuata akamwambia, Ya Mohammad…’ ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu nipe ushauri, nishauri mimi’. Mtume akamjibu akamwambia la tagadhabu! akarudia tena kwa sababu hakuwa anaamini kwamba huo ndiyo ushauri atakaopewa na Mtume Mohamed.

SPIKA: Sekunde thelethini kengele ya pili imeshagonga.

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika, akamwambia eeh! Mtume Mwenyezi Mungu nishauri, mara tatu akamwambia la tagadhabu! anamwambia usigadhabike. Nimejitahidi sana hivi nivyozungumza nimejizuia nisigadhabike, lakini hali halisi iliyopo huko tunapotoka, mimi natoka kijiini ndugu zangu, hali halisi iliyoko huko watu wanapata shida.

Mheshimiwa Spika, mtu kasomesha mwanae bado anaenda kumhudumia ‘libaba’ liko pale unalipika ugali, hajaajiriwa, unaangalia aliyeko shule naye anafeli, kwa nini anafeli hamna mwalimu! mwalimu unaye nyumbani unampikia ugali! Inna lillahi Mwenyezi Mungu atusaidie! Nashukuru sana. (Makofi)