Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushuru, kwanza kabisa nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema aliyenijalia afya na nguvu ya kuweza kusimama mbele ya Bunge lako tukufu na kuweza kuchangia.

Pili, niunge mkono hoja taarifa zote mbili kwa maana Wizara ya Ardhi na Wizara ya Maliasili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba nijikite sehemu moja tu; Bunge la Bajeti la mwaka jana Tume ilipewa shilingi bilioni nne, lakini baada ya Kamati yetu kuangalia fedha zile hazionekani. Kama unavyojua ipo haja kubwa sana na changamoto sana katika kupima ardhi yetu nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha hizi sijajua zimekwama wapi, fedha sijajua zimekwama wapi kwa sababu fedha hizi zingetolewa kwa wakati zingeenda kupima zaidi ya vijiji 600. Hata hivyo kwenye vitabu fedha hizi hazionekani. Niiombe Serikali au Wizara ifuatilie fedha hizi ili ziweze kutolewa ziende kufanya kazi iliyokusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye fedha walizopewa Wizara ya Ardhi ambayo ni pesa ya uimarishaji wa usalama wa ardhi. Pesa hizo ambazo ni shilingi bilioni 345, fedha hizi ni nyingi sana, lakini ukiangalia walichopanga hapa ambayo ni KKK yaani Kupima, Kupanga na Kumilikisha, wamepewa asilimia asilimia 25 tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuweke legacy na tuweke historia katika Bunge hili la Kumi na Mbili chini ya Spika wetu makini Mheshimiwa Dkt. Tulia Ackson, Naibu Spika Mheshimiwa Mussa Zungu na ninyi Wenyeviti wawili yaani wewe Mheshimiwa Najma Giga na Mheshimiwa Kihenzile, lazima fedha hizi sasa zifanyiwe review ili fedha hizi ziende kupima ikiwezekana kupima nchi nzima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu gani naongea hivyo, ukiangalia sasa hivi migogoro ya wakulima na wafugaji ni mingi sana, lakini ukienda mbali zaidi ni kwamba nchi hii haijapimwa, lakini ukikusanya pesa hizi zote zikaelekea kupima ardhi nchini, tayari tutakuwa tumesaidia wananchi wetu kwa asilimia 100 na hili suala wala hatutalirudia tena katika kupima, kupanga na kumilikisha tutakuwa tumekwisha maliza kazi kama Mheshimiwa Chege alivyosema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Serikali yako tukufu, Bunge hili la Kumi na Mbili, Waheshimiwa Wabunge kwa pamoja tuombe hata kwa Mwenyezi Mungu mapendekezo haya yaridhiwe, pesa hizi ziende katika kupanga, kupima na kumilikisha ardhi nchini ili tuondokane kabisa na tatizo hili kwa asilimia 100.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye TANAPA; ni kweli TANAPA wanafanya kazi moja nzuri sana na kwa kweli watu hawa wanastahili kuongezwa fedha na ukizingatia mwaka 2017 waliongezewa hifadhi sita kwa maana ya 16 ongeza sita ni 22, bado ina maana fedha walizotengewa bado bajeti ni ile ile. Lakini bila kusahau TAWA hawa watu wa TAWA wanafanaya kazi kubwa sana. Watu hawa ukiangalia ndio wanapambana na wanyama wakali na waharibifu, lakini watu hawa hawajapewa fedha na wameongezewa mapori tengefu zaidi ya matano, lakini ceiling bado ni ile ile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe Bunge lako hili lipendekeze TAWA kuongezwa fedha ili waende kufanya kazi hii ambayo ni kujenga vizimba maeneo yote, kwa mfano sasa hivi tunavyoongea katika Kamati yetu mwaka 2019 mpaka sasa hivi wamejenga vizimba 15 tu, just imagine, wakati huo vizimba vile vinasaidia wanyama wakali na waharibifu kutoingia kwa wananchi wetu. Wananchi wetu wanadhurika. Niiombe Serikali itenge fedha za kutosha wapewe TAWA watu hawa wana kazi kubwa sana, wanafanya kazi nzuri mno. Waongezewe fedha ili tutoe migogoro ya wakulima, wanyama wakali kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo twende kwenye mahoteli yetu; kuna hoteli 23 na lodge ambazo nne ziko katika hifadhi, lakini hoteli zinazofanya vizuri ni zile ambazo zimebinafisishwa tu. Hata hivyo zote zaidi ya hoteli 10 hazifanyi vizuri. Ina maana hoteli zile zinaenda ku-corrupt kabisa, nyingine zimebaki kama magofu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama unavyojua mama yetu Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan, Royal Tour yake imejibu. Kuna wazungu, kuna watalii chungu nzima, lakini ukija kuangalia kwenye hoteli zetu hizi zime-corrupt hazifanyi vizuri, zimekufa, kwa maana hazipo. Wakati watalii wale wanahitaji hoteli nyingi, hoteli zinahitajika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, basi niliombe Bunge hili lipitishe mapendekezo wanyang’anywe wawekezaji wale ambao wamehodhi hoteli hizi wapewe watu wengine ambao wana uwezo wa kuendeleza hoteli hizi. Ukiangalia kwenye Kamati yetu hoteli hizi zimepewa watu ambao hawana uwezo. Unakuta mtu amepewa hoteli halafu anaandika kukarabati zaidi ya miezi sita. Kukarabati zaidi miezi sita hii sio sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Serikali ipitishe mapendekezo haya hoteli zile wale wawekezaji wananyang’anywe na wapewe watu ambao ni wenye uwezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie na mfumo wa ILMIS; mfumo wa ILMIS tangu mwaka 2018 nadhani mpaka sasa hivi uko katika mikoa miwili tu kwa maana ya Dar es salaam na Dodoma, lakini bado mfumo ule haufanyi vizuri, niiombe Serikali yako sasa itoe fedha za kutosha ili mfumo huu ukae vizuri ili kuepusha migogoro ya wakulima na wafugaji; vijiji na vijiji; migogoro ya Wilaya na Wilaya; migogoro ya Mikoa na Mikoa na hata migogoro ya Taifa na Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja. (Makofi)