Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Mohammed Said Issa

Sex

Male

Party

ACT

Constituent

Konde

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. MOHAMED SAID ISSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda nimshukuru Allah Subhanahu wa Ta’ala kwa leo kupata nafasi na mimi kuweza kuchangia katika Bunge hili tukufu katika Hotuba ya Waziri Mkuu. Lakini pia nikushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii ambayo ni kwa ruksa yako ndiyo naweza kuzungumza hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi mchango wangu kwanza utajikita katika biashara; na hii biashara ni katika nchi mbili hivi Zanzibar na Tanganyika, yaani Tanzania Bara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Zanzibar na Tanzania Bara tumekuwa tukitegemeana katika mambo mengine ikiwemo biashara. Tunatumia bandari zetu ya Zanzibar na Dar es Salaam.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MWENYEKITI: Waheshimiwa tumsikilize mchangiaji.

MHE. MOHAMED SAID ISSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatumia bandari zetu ambazo zipo katika Zanzibar na Tanzania Bara katika kupitisha mizigo yetu, lakini mara nyingi biashara huwa inatokea Zanzibar kuja Dar es Salaam ama Tanzania Bara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye biashara ambayo tunafanya sisi Wazanzibar au wananchi wa Zanzibar tumekuwa tukikutana na changamoto nyingi sana ambazo kwa kiasi kikubwa imeonekana inakuwa ni tatizo linalosababishwa makusudi lakini si mipango ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mipango hii mara nyingi iko vizuri, lakini watendaji ndio wanaoiharibu. Nitoe mfano kidogo. Katika suala la declaration ya mizigo ambayo inasafiri kutoka Zanzibar kuja Tanzania Bara, mizigo ile mara nyingi meli yetu inakuwa ni za hapo kwa hapo siyo zile Meli ambazo tayari zina shadow. Kwa maana hiyo wafanyabiashara ambao wanaleta mizigo wanakuwa na mizigo ambayo ni ya kushtukizwa. Kwa mfano kama kipindi hiki cha mwezi wa Ramadhan, mfanyabiashara ananunua mzigo leo anataka apakie mzigo kwenye meli lakini kwa bahati mbaya ni lazima awe ametuma ripoti mapema ili mzigo ule uweze kupakiwa na kufika kule, nje ya hapo mzigo ule ukifika meli inapigwa faini na mzigo unapigwa faini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hii ni changamoto ambayo wafanyabiashara wa Zanzibar wanakutana nalo. lakini si hilo tu, wafanyabiashara wa Zanzibar tumekuwa tukikutana na changamoto ya mizigo ambayo inafika pale Dar es Salaam. Tunakutana na bei kubwa ya wharfage ambayo inakuwa inachajiwa mizigo ambayo inatoka Zanzibar. Kwa hiyo tungeomba bei ile iendane na hali halisi, hasa ukizingatia ile sehemu ambayo inashushwa ni sehemu ambayo fedha zake za kujengea pale zilitoka kwa Rais wa Kwanza wa Zanzibar Mheshimiwa Abeid Aman Karume, kwa ajili ya kuwasaidia Wanzazibar lakini leo imekuwa inawakwaza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, baada ya kuyasema hayo, ningependa kwenda kwenye hilohilo la TRA. Mizigo inapotoka bandarini kwenda madukani imekuwa ikisumbuliwa na TRA haohao ilhali imeshafanyiwa inspection na kulipiwa kodi kama kawaida lakini ikifika njiani ikifika tu, ikitoka nje ya geti kuna TRA wengine wanajitokeza na kuwasumbua wafanyabiasha hawa na kushindwa kufanya kazi zao vizuri. Kwa hiyo hili naomba lifanyiwe kazi ili kuendeleza Muungano wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nizungumzie suala la Muungano. Katika ukurasa wa 72 Mheshimiwa Waziri Mkuu ameelezea kuudumisha, kuuenzi na kuulinda Muungano na mimi naipongeza Serikali yetu hilo ndiyo tunalolihitaji kwa sababu Muungano huu ni tunu ya taifa na sote tunaupenda. Lakini kubwa zaidi nilitaka nichangie hapa; hizi kero za Muungano ambazo zimekuwa zikifanyiwa kazi, mimi nakubaliana nazo, ni nzuri na zinasaidia kuondoa changamoto lakini bado tunatakiwa tufike kwa wananchi kujua ni changamoto gani hasa zinaweza kuulinda Muungano? Kwa sababu wananchi bado wanasema kwamba hizi changamoto ni zile zinazoikabili Serikali ya Zanzibar na Serikali ya Tanzania, siyo zinazowakabili wananchi. Kwa hiyo, baada ya kutatua changamoto hizi 11 basi turudi kwa wananchi ili na wao waseme ni lipi hasa linaweza kuimarisha Muungano wetu huu na ukawa Muungano wa mfano kama ilivyosema Hotuba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hapo, ahsante sana. (Makofi)