Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana na mimi kupewa fursa hii ya kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza kwa kumshukuru na kumpongeza sana Mheshimwia Rais kwa matokeo mazuri sana ya utekelezaji ambayo imepelekea ni nchi pekee katika Afrika Mashariki ambayo ilikuwa na ukuaji ambao ni chanya. Tulikuwa na ukuaji ambao nchi nyingine zote ukuaji wake ulikuwa na negative GDP. Kwa hiyo ningependa sana kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa hilo lakini pia na Serikali nzima akiwemo Makamu wa Rais na Waziri Mkuu. Kazi iliyofanyika ni kubwa mno ni nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo yote mazuri lakini sasa hivi tunashuhudia dunia nzima inaingia kwenye changamoto kubwa za uchumi, na huo mdororo wa uchumi umeshaanza kuonekana hapa kwetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipokuwa najaribu kuangalia wenzetu hili suala wamelionaje na wamelichukuliaje na sisi Tanzania kama sehemu ya dunia je, tujiweke wapi?

Kwa kweli kwa kiasi kikubwa ukiangalia mashirika makubwa ya fedha ikiwemo IMF pamoja na J. P. Morgan wameonesha ya kwamba pamoja na hizo changamoto lakini kwa nchi kama Tanzania hii ni fursa. Kwa hiyo badala ya kuangalia zile changamoto zilizopo zinazotokana na hii hali sisi sasa tungejipanga kuangalia fursa ambazo zipo kutokana kwanza na athari za UVIKO na pia na athari zinazotokana na vita ya Urusi pamoja na Ukraine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuanzia hatua za haraka, nina imani Serikali kupitia Ibara 140 ya katiba yetu na Sheria ya Bajeti Ibara ya 35 mpaka 39 ilichukua hatua hizo ambazo zimeitaka Serikali kuwa na mfuko wa dharura (contingence fund). Kwa hiyo katika hali ya namna hii ninategemea kwamba Serikali itatumia mfuko huo kuchukua hatua za haraka ili tuweze kunusuru hali ya mfumuko wa bei. Lakini siyo mfumuko wa bei tu, vile vile kutakuwa na mfumuko wa mahitaji ya pesa za kigeni ambayo yanaweza kutuweka katika hali ngumu zaidi. Sasa tufanye nini ili tuweze kuondokana na hilo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, wewe mwenyewe unajua, kuwa mikopo yetu mingi tunalipa kwa pesa za kigeni. Kama kutakuwa na mfumuko na mahitaji makubwa ya pesa za kigeni, nchi yetu ifanye nini? Nina imani ya kwamba hatuwezi kuahirisha kulipa madeni lakini tutahitaji pesa za kigeni nyingi. Uchumi wetu unategemea kilimo. Nawashukuru sana Wabunge wameongea kwa kiasi kikubwa umuhimu wa kilimo kwa Tanzania. Lakini nchi yetu ina madini, nchi yetu ina utalii, nchi yetu ina bandari. Hivyo vitu vitatu vikipelekewa msukumo na Serikali ikajikita katika hivyo vitu vitatu vinne nina imani tutavuka salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye kilimo unachohitaji ni kuwa na kilimo chenye tija, huhitaji zaidi ya hapo. Kilimo chenye tija. Kwa mfano leo kilimo chetu heka moja ya mahindi tunazalisha tani moja wakati kawaida kabisa heka moja ya mahindi inatakiwa izalishe tani nne. Kwa hiyo tukianzia na hiyo tuu, ina maana tutakuwa tumejipeleka mahali pazuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini namshukuru sana Mheshimiwa Rais kupitia Wizara ya Kilimo anavyofanya mageuzi (transformation) kwenye kilimo, nafikiri katika hiyo na motisha walizopata wakulima nina imani ya kwamba kupitia kilimo hili tutaliweza. Kwa hiyo tunahitaji pesa za kigeni kupitia hata nafaka. Nimesema hii ni fursa kwa sababu Ukraine na Russia ndio walikuwa tunaingiza kwa kiasi kikubwa ngano. Lakini nchi za jirani walikuwa wanaingiza mpaka mahindi wanaagiza kutoka Russia. Sasa mahindi yetu yatapata soko kubwa na bei zimeshaanza kuwa nzuri. Kwa hiyo tukijikita kwenye kilimo cha mahindi nina imani kuwa tutaenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye madini tuna fursa kubwa lakini kuna wawekezaji ambao wanahitaji kuwekeza kwenye madini bado wanazungushwa, hawapewi kipaumbele. Mfano mmoja wapo kwa muda mrefu nimesimama hapa Bungeni; tuna madini yanaitwa Niobium. Kuna wawekezaji toka miaka ya 2015 mpaka leo wanashindwa kupata leseni. Mpaka financial institution wameamua waachane na huu mradi. Wawekezaji nao wanataka kuachana na huu mradi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi ombi langu, kwa ajili ya hii hali miradi mingine kama hiyo tuichukue kwa dharura. Tukikosa pesa za kigeni inawezekana tukakosa hata chakula. Hii mbolea tunayoisema tunahitaji pesa za kigeni. Pesa za kigeni tutazipata wapi? Pesa za kigeni hatuwezi kuzipata kwenye kuondoa tuu ruzuku. Pesa za kigeni zitapatikana kwenye uzalishaji wetu kwenye kilimo, madini na utalii. Kwa hiyo ningeomba kwa kiasi kikubwa Serikali ichukue hatua za makusudi. Hii hali tuliyonayo sasa hivi ya uchumi wa dunia ni hali ambayo inaweza kutupeleka mahali pabaya sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vile vile tunahitaji kuboresha miundombinu. Kwa sababu miundombinu nayo inaweza kutuletea inflation. Sasa kwa kiasi kikubwa...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Oran Njeza kwa mchango wako.

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana naunga mkono hoja. Ahsante sana.