Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Ally Mohamed Kassinge

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nami nianze kuchangia hotuba ya Bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kuipongeza Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mama Samia kwa juhudi ambazo imeendelea kuzitekeleza kiasi kwamba Watanzania wanashuhudia kwa macho na wenye kusikia wanasikia shughuli mbalimbali ambazo zinatekelezwa, ikiwa ni pamoja na utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunge lako hili la 12 katika Mkutano wake wa nne liliazimia kwamba sekta ya kilimo ni sekta ambayo inatakiwa ipewe kipaumbele namba moja katika mpango huu wa tatu wa maendeleo. Na nitumie fursa hii kuipongeza sana Serikali kupitia Wizara ya Kilimo kwa kile ambacho imeanza kukifanya, kitu ambacho kinaleta matarajio makubwa sana kwa Watanzania hususan wakulima ambao ndio wazalishaji wa mazao yetu ya kilimo, kwa maana ya mazao ya biashara lakini pia mazao ya chakula katika nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia sekta ya kilimo kabla hatujawagusa wenyewe wakulima tutakuwa tunatwanga maji kwenye kinu. Ni lazima tunapozungumzia kilimo tubainishe maeneo ambayo kweli yatamsaidia mkulima mmoja mmoja na pia kwa vikundi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika kilimo kuna suala la ushirika ambalo kimsingi ndilo eneo pekee litakalomsaidia Mkulima. Niishukuru sana hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu katika ukurasa wake wa 29 na 30 amegusia kidogo ushirika na pale ambapo mambo hayakwenda vema Serikali imechukua hatua, na ninaomba ninukuu sehemu ya hotuba hii.

“Hatua mbalimbali za kisheria zimechukuliwa dhidi ya wote waliohusika na ukiukwaji wa taratibu za uendeshaji wa vyama vya ushirikia ikiwemo vitendo vya wizi wa mali na fedha za ushirika”

Mheshimiwa Mwenyekiti, hongera kwa Serikali kwa hatua hii. Lakini wakati hatua hizi zinachukuliwa kwa masikitiko makubwa nielezee kilio cha wakulima wa Nanjilinji katika Jimbo langu la Kilwa Kusini wanaotokana na Chama cha Msingi cha Nanjilinji ‘A’ ambao kwa msimu wa kilimo uliopita wa 2021/2022 wamedhulumiwa mazao yao, mpaka tunazungumza katika Bunge hili wakulima hawa bado hawajalipwa mazao yao. Wmezalisha kiasi cha zaidi ya tani 40 lakini hawajalipwa mpaka leo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbaya zaidi kumekuwa na matumizi mabaya ya nafasi za watu ikiwemo viongozi wa chama cha msingi wakishirikiana na viongozi wa ushirika au watendaji wa Idara ya Ushirika Wilayani; ambapo wameandikia hati hewa watu ambao hawahusiki katika kulipwa mazao haya. Mbaya zaidi hizi hati hewa ambazo zimekwenda kwenye malipo hewa zinawagusa viongozi na watendaji wa Serikali, na mpaka sasa tunavyozungumza wakuliwa hawa wapatao 40 wameendelea kulalamika na hawajasaidiwa mpaka leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninayo heshima kutoa taarifa hii, na wakulima hawa walipwe fedha zao za msimu uliopita mara moja ili waweze kujikimu na kuanza tena shughuli za Kilimo kwa msimu ujao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikitoka kwenye sekta ya kilimo nije katika sekta ya afya. Niendelee kuipongeza Serikali ya Awamu ya Sita ya Mama Samia, wote tumeshuhudia namna ambavyo Vituo vya Afya vimeboreshwa, katika baadhi ya maeneo, kadhalika zahanati zimeboreshwa, lakini katika wilaya mpya hospitali za wilaya zimeendelea kujengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo hili nipongeze, katika Jimbo langu la Kilwa Kusini kuna Hospitali yetu ya Wilaya, ipo Kilwa Kivinje, inaitwa Kinyonga. tumepata Shilingi milioni 300, fedha kwaajili ya jengo la emergence, na kwakweli ujenzi unaendelea vizuri; tunaendelea kuipongeza na kuishukuru Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika eneo hili niiombe Serikali, kwamba Hospitali hii ya Wilaya ya Kilwa Kinyonga ni Hospitali chakavu, ni ya tangu miaka ya sitini na kwa maana hiyo miundombinu yake si ya kuridhisha. Wakati tunaendelea kuboresha miundombinu katika maeneo mengine katika mpango huu niombe kabisa kwamba ifikirie kutenga fedha za kutosha kwaajili ya ukarabati na uboreshaji wa miundombinu katika Hospitali ya Wilaya ya Kinyonga pale Kilwa Kivinje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ningeweza kupongeza ni mwendelezo wa ujenzi wa barabara nchi nzima; na hapa kwa upekee wake kabisa nipongeze kwa barabara ile ya mwendokasi inayojengwa kutoka Mbagala Rangi Tatu Dar es Salaam kuelekea mjini. Barabara hii itakuwa ni ufumbuzi na utatuzi wa kero kwa wakazi wa Mbagala ambao sisi watu wa kusini wengi ndio tunaishi maeneo haya. Kwa hiyo, tunaipongeza sana Serikali kwa eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika eneo hili nisikitike tu kwamba, kuna usumbufu mkubwa ambao unafanywa na mamlaka ya Serikali za Mitaa kwa jina Halmashauri ya Manispaa ya Temeke. Halmashauri hii imelazimisha abiria wanaotoka Kilwa Kivinje na Kilwa Masoko kutumia stendi inayoitwa Biansi kinyume na utaratibu wa kutumia stendi ya mabasi ya kusini iliyopo pale Rangi Tatu, maarufu kama stendi ya mjini. Huu ni utaratibu ambao unaleta usumbufu usio na lazima. Niiombe Serikali iingilie kati jambo ili abiria waendao Kilwa na maeneo mengine ya Mikoa ya Kusini ya Lindi, Mtwara na Ruvuma watumie Stendi ya Mkoa iliyopo pale Mbagala Rangi Tatu na si stendi za pembezoni, ambazo zinaleta usumbufu mkubwa kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho niendelee kuipongeza Serikali kwa kuleta miradi ya kuboresha miji yetu, manispaa na majiji yetu, kama vile mradi wa TSCP umeboresha miundombinu ya miji nchini, mradi wa ULGSP umeboresha miundombinu ya miji, mradi wa DMDP Dar es Salaam inapendeza sasa hivi na sasa hivi tupo katika mradi wa TACTIC. Rai yangu katika mradi huu wa TACTIC na miradi mingine ya kuboresha miji, itakayoendelea, kuwe na uniformity katika nchi, ili isije ikawa unaenda katika miji mingine imedorora haipendezi na miji mingine inapendeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kutoa mapendekezo, kwamba katika mpango huu wa tatu wa maendeleo miji mingine iliyopo ndani ya nchi yetu ya Tanzania ikumbukwe katika miradi hii ikiwemo Mangaka, Ifakara, Chalinze, Mafinga, Kilwa Masoko, Kilwa Kivinje, Tarime, Mpanda na mingineyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya ushauri huu naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)