Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Benaya Liuka Kapinga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi hii ya kuchangia Ofisi ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami niungane na Wabunge wenzangu kutoa pongezi nyingi sana kwa Serikali hii ya Awamu ya Sita kwa namna inavyofanya kazi. Siyo kwa kufanya kazi tu lakini kwa namna inavyosikiliza kero, inavyosikiliza hoja za wananchi kupitia sisi Wabunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi karibuni tu yamefanyika mambo mengi na mabadiliko makubwa na Serikali hii ya Awamu ya Sita ilipokwenda kusikiliza hoja za Waheshimiwa Wabunge naipongeza sana Serikali hii ya Awamu ya Sita. Kipekee nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa namna anavyofanya kazi. Karibuni tu tulikuwa na mgogoro mkubwa kule Ngorongoro, lakini kwa utulivu mkubwa suala hili limeshughulikiwa nampongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapo hapo tuwe wakweli, Waheshimiwa Wabunge naomba tuwe wakweli na wa wazi kabisa katika suala hili la mfumuko wa bei.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wamezungumza wenzangu hapa ni kweli kabisa kuna vita ya Ukraine na Urusi ambayo hadi leo ina siku 36, lakini suala hili la mfumuko wa bei halikuanza siku hizo. Amesema hapa Injinia Ezra mwaka jana Disemba, 2021 vitu vilianza kupanda bei, malalamiko yalianzia kwenye mbolea, yakafika kwenye vifaa hivi vya ujenzi, yamefika mafuta ya kupikia vita hakuna. Vita imeanza Februari hapa!

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo kweli tukajivika kwenye suala hili la mafuta na vita ya Ukraine, hapa pana jambo Serikali inapaswa kufanya kitu! siyo tu kukimbilia kwamba sasa mafuta yamepanda basi na vitu vitakwenda kupanda, nasema siyo sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tunakumbuka vizuri Waziri Dkt. Ashatu aliwahi kusema hapa tumeunda Tume inapitia huko itakuja na taarifa, hivi wenzangu ile taarifa mliipata? Kwa hiyo, lazima tuende vizuri, tukubaliane vizuri. Serikali ina jambo la kufanya hapo pamoja na vita hii ina jambo la kufanya.

WAZIRI WA FEDHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa wapi? Mheshimiwa Waziri wa Fedha.

T A A R I F A

WAZIRI WA FEDHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba Serikali ina fursa ya kujibu lakini ni vizuri majibu ambayo wananchi wangetamani kuyapata muda ule ule yatolewe muda ule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza ambalo ningependa na Wabunge wote pamoja na wananchi waelewe, hakuna mtu Serikalini aliyesema jambo lililosababisha bei za bidhaa kupanda ni vita peke yake hakuna! Hakuna mtu aliyesema hivyo!

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mtiririko wa vitu zaidi ya kimoja ambavyo vimesababisha bei za bidhaa ziweze kupanda. Jambo la kwanza ambalo lilitangulia kabla ya yote ilikuwa ni COVID-19 na madhara ya COVID-19 kiuchumi siyo ya siku ile ile jamani hiki ni kitu cha kawaida. Usipozalisha leo utakula ulichozalisha jana ila siku ambapo unatakiwa ule kile ambacho ulizalisha jana kwa kuwa jana hukuzalisha ndiyo hakitakuwepo. Madhara ya COVID yasingetokea mwaka 2019, madhara ya COVID lockdown ya mwaka 2019 inatokea mwaka 2020/2021 hivyo ndivyo uchumi unavyokuwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hapa mtu asipolima mwaka jana hapati njaa mwaka jana ule ambao hakulima, anapata njaa mwaka ambao unafuata. Kwa sababu, ndiyo unapotakiwa kuvuna. Kwa maana hiyo, madhara ya bei kupanda siyo tu vita peke yake yamelundikana kuanzia COVID hilo la kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili; kwetu hapa Tanzania wengine wanasema sasa mbona imetokea vita kule mbona na alizeti mafuta yake yamepanda bei? Tukumbuke mwaka jana Wabunge angalieni Hansard zetu hapa mwaka jana Mikoa yote haikupata mvua katika kipindi ambacho kinatakiwa kiwe hili wala siyo vita ni ukame. Mikoa yote, kote mnakotokea mvua hazikuanza kama ambavyo huwa zinatakiwa kuanza.

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa.

WAZIRI WA FEDHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la tatu sasa ndiyo imekuja hiyo ya vita, baada ya vita imepandisha vitu vingine vyote kwa sababu ya masuala ya mafuta, lakini hata ile demand tu imekuwa kubwa katika maeneo mengine yote yale. Baada ya demand kuwa kubwa ndiyo inasababisha pressure ya bidhaa zingine zote, hiyo inakuwa spiral yaani inaongezeka inaji-fuel.

MWENYEKITI: Ahsante sana kwa ufafanuzi Mheshimiwa Waziri wa Fedha, Mheshimiwa Benaya Kapinga endelea kuchangia.

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na nashukuru kwa maelezo mazuri ya Serikali na mimi sikatai lakini nasema tuna jambo la kufanya zaidi ya tulivyofanya sasa hivi. Kama nilivyosema mwezi Januari Serikali ilisema kuna Tume imeundwa inafuatilia hayo malalamiko ya bei ya bidhaa kupanda, nimehoji hapa ile taarifa ilipatikana na ilifanyiwa kazi ipi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nilindie muda wangu kwa sababu dakika kadhaa zimekwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale Jimboni kwangu kuna shida nimempongeza hapa Mheshimiwa Waziri Mkuu kafanya kazi nzuri Ngorongoro, Serikali imejipanga vizuri, wananchi sasa kwa utaratibu mzuri kabisa wanahamishwa au watahamishwa kutoka Ngorongoro kuja maeneo mengine yaliyopangwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale Jimboni kuna mradi wa panda miti kibiashara, mradi huu ni mzuri sana. Mradi huu utekelezaji wake niliusema hapa mwaka jana na ninaendelea kuusema leo, mradi huu ulipotekelezwa ni maeneo ya wananchi ni maeneo ya wakulima. Wakulima wale walikuwa wanamiliki maeneo yale kihalali kabisa kwa miaka yote ya nchi hii, lakini bahati mbaya sana imefika sehemu sasa umeanzishwa mradi ukawapuuza wale wananchi. Wananchi wale wamebaguliwa hawana chao, wamekalishwa tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maeneo hawana haki tena, hivi sasa hivi kuna risasi zinapigwa pale, hivi sasa hivi kuna mapanga yanapigwa pale, wananchi wale hawana haki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuomba unilindie muda sijui hiyo ni kengele ya ngapi?

MWENYEKITI: Nimekuongeza dakika moja, malizia hoja yako.

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa hiyo naiomba Serikali kama ilivyofanya Ngorongoro, naiomba Serikali vivyo hivyo iende pale Jimboni eneo la Ndika ikasuluhishe hili. Kwa sababu maeneo yale ni haki ya wakulima wale. Wamepanda miti sawa sijui ni ya nani haieleweki kwa sababu kila mtu anasema mara ya Kijiji, mara ya mtu fulani, mara ya TFS hakuna anayejulikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru sana Mkuu wa Wilaya ameunda Tume na sasa hivi wanaendelea na mchakato, lakini bahati mbaya sana kasi yake sio ile ya kutoa majibu haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni suala la Madiwani. Madiwani hawa wana kazi nyingi sana pale wanapokuwa katika maeneo yale lakini malipo yao hasa kwenye eneo la posho za kujikimu. Upo Waraka wa tarehe 02 Januari, 2019 unaosema fedha za kujikimu atapewa Diwani anayelazimika kulala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sina hakika Wabunge Waraka ule nasi unaweza ukafanya kazi, sina hakika. Kama sivyo kwa nini kwa Madiwani kuwe na Waraka unaosema fedha ya kujikimu apewe yule anayelazimika kulala, wakati maeneo ya vijijini ulazima wa kulala upo tu. Mtu anaweza akaja sasa hivi kwenye kikao, kikao kikaisha Saa 10 hakuna usafiri wa kurudi kwenye eneo lake lazima atalala. Lakini tafsiri ya wale wanaotafsiri ule Waraka wanasema posho ya kujikimu atalipwa yule Diwani anayelazimika kulala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waraka huu ni wa kibaguzi kama kwa upande wetu hautumiki ningependekeza Serikali ifute Waraka huu, kwa sababu unawabagua. Wote ni viongozi wa kisiasa Madiwani ni wanasiasa na Wabunge ni wanasiasa na viongozi wengine. Kama hautumiki hapa kwa maana ya kwamba, kwa sababu kuna Wabunge wanaolazimika hata wasilale, lakini kama hautumiki hapa basi hata kwa Madiwani Waraka huu ufutwe. Madiwani wale walipwe posho zao za kujikimu kama wanavyolipwa wengine wanaolazimika kulala. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante.

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)