Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja iliyopo mezani kwetu na mimi niungane na wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayoifanya maana ndiye Waziri ambaye ana dhamana ya Wizara hii kwa sababu ni Ofisi ya Rais – TAMISEMI, niwapongeze Mheshimiwa Bashungwa na timu yake Naibu Mawaziri wote, Katibu Mkuu na Naibu Makatibu Wakuu na watendaji wote wa TAMISEMI kwa kazi nzuri wanayoifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu utaanzia pale alipoishia Mheshimiwa Jerry Silaa, Meya Mstaafu wa Ilala yeye amezungumzia kwenye ngazi za vijiji na Mamlaka ya Serikali za Mitaa kwa ngazi ya Halmashauri. Mimi nitazungumzia kwenye Sekretarieti ya Mkoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukisoma Sheria ya Tawala za Mikoa Sura Namba 97 lakini na policy paper ya ugatuaji ile decentralization ya mwaka 1998 utakuta majukumu ya Region Secretariat ni pamoja na kuzishauri Mamlaka za Serikali za Mitaa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vilevile kuzisimamia mamlaka za Serikali za mitaa na kutengeneza mazingira wezeshi ili Mamlaka ya Serikali za Mitaa ziweze kutimiza wajibu wake, tulitegemea kwenye Region Secretariat kuwa na maafisa waandamizi na wabobezi ili wakienda kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa wakashauri, lakini changamoto iliyopo sasa hivi Sekretarieti za Mikoa hazina wataalam hao, unakuta mtaalam anayekwenda kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa kushauri ni junior kuliko aliyeko kwenye Halmashauri, kwa hiyo hata ushauri wake hauwezi kusikilizwa na hata cha kushauri hana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, muda umefika sasa na Mheshimiwa Bashungwa tuna matarajio makubwa sana na wewe, hebu tufanye mapitio ya Sheria yetu hii ya Tawala za Mikoa ya mwaka 1997, lakini tufanye re-structuring kwenye RS je, muundo wa sasa wa RS unakidhi mahitaji ya sasa kusimamia Mamlaka za Serikali za Mitaa? Tumeona hapa juzi Mheshimiwa Aweso ameenda mahali fulani anauliza nionesheni bwana la shilingi milioni 600 na watu wa Mkoa wapo na wao wanashangaa kama tungekuwa na strong RS yale yasingetokea Mawaziri msingekimbia kimbia kungekuwa na kazi kubwa zinafanywa na Sekretarieti ya Mkoa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo naomba tufanya mabadiliko, naomba tuziwezeshe tuwe na wataalam mahiri natuwape rasilimali fedha ili ziweze kutekeleza majukumu yake na Mawaziri mtatulia kufanya maamuzi ya kimsingi na sio kwenda kukagua vitu ambavyo Sekretarieti ya Mkoa wangeweza kutekeleza mambo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu wa pili, unahusu miradi ya kimkakati; nakupongeza Waziri umesema kwamba umeunda timu ya kuzishauri na kuziwezesha Mamlaka ya Serikali za Mitaa kuandika maandiko ya miradi, lakini Mheshimiwa Waziri nikuombe tu kwamba kuna changamoto ya kuchelewesha maandiko katika ofisi yako, maandiko yamekaa muda mrefu sana na kule kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa kuna wataalam wa kuandika hayo maandiko, wachumi miongoni mwa course ambazo wanazofanya vyuo vikuu ni project writeup, sasa nashangaa kwamba wachumi hawa wame-graduate vyuoni lakini hawawezi kuandika andiko la mradi tu kujenga ghala kwenye Mamlaka ya Serikali ya Mitaa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, muharakishe kupitia hayo maandiko ili fedha zitolewe umesema hapa mwaka jana fedha zilizotumika ni asilimia 32 tu ya fedha zilizotolewa, ina maana kwamba maandiko hayapitishwi kwa wakati, na maandiko mengine Mheshimiwa Waziri yanahitaji maamuzi ya muda mchache tu, nikupe mfano kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa kwa Mkoa wa Lindi na Mtwana tunapolima korosho wengi wameomba kujenga maghala ya kuhifadhi korosho, mamlaka hizi zingepewa fedha wangeweza ku-back even kurejesha hivi fedha kwa muda mfupi sana kwa sababu kwa sasa hivi kwa mjengepo wa bei kilo moja ya korosho zinapoingia ghalani inalipwa shilingi 38. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri za Mkoa wa Mtwara mwaka huu zimezalisha tani 178 kwa bei hii kuna ina maana kuna takribani shilingi bilioni tano ingepatikana hawa hata wakiruhusiwa kwenda kukopa kwenye mabenki ya kibiashara uwezekano wa kuridisha ni mkubwa sana kwa kipindi kifupi, hivi andiko kama hili linakaa miaka mitatu linasubiri nini, na ni fedha ipo wazi kwa sababu kila msimu wa korosho yanahitajika maghala kila msimu wa korosho wapo wanunuzi wanakuja wanahitaji haya maghala kila msimu wa korosho kunahitajika maghala ya kuweka pembejeo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye stakabadhi ghalani kunahitajika maghala, sasa maandiko kama hayo yanakaa miaka mitatu yanasubiri nini? Mheshimiwa Waziri ebu fast track vitu kama hivyo tupunguze Mamlaka ya Serikali za Mitaa kutegemea utegemezi kutoka Serikali Kuu. Hapa tungeruhusu Halmashauri hizi kujenga maghala takribani kila Halmashauri ingekuwa na uhakika kupata shilingi 500,000,000 kila mwaka, sasa hii ingesaidia kufanya vitu vingi sana. Hebu naomba Mheshimiwa Bashungwa fanya maamuzi watu wajenge maghala na fedha hizi ziweze kupatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ninalotaka kuchangia ni kuhusu mradi wa TACTIC; huu mradi nampongeza Waziri kwamba mmeongeza kasi ya mazungumzo ili uanze kutekelezwa na mimi kipekee nimshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuingiza Halmashauri ya Mji wa Nanyamba katika mradi huu, tupo kwenye miji 45 na tunausubiri sana kwa hamu. Mheshimiwa Waziri nikuombe kwamba tusifanya makosa yaliyopita huko nyuma miradi hii tujenge kulingana na mahitaji ya sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Rais ameelekeza kwamba masoko yafuate watu na sio watu wafuate masoko. Tuna miradi mingi pale Mtwara Mjini kwa kaka yangu Mheshimiwa Mtenga limejengwa soko pale Chuno la fedha nyingi, lakini kukawa na mgogoro kati ya wafanyabiashara kwenda kuhamia kwenye lile soko. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye maeneo mapya tusiruhusu vitu kama hivyo nafahamu huu mradi unachangamoto ya fidia ni bora tutafute fedha mahali tufidie kwenye masoko yaliyopo sasa hivi tujenge ili tuboreshe hapo ili kusiwe na kujenga miradi ambayo haina manufaa. Tukijenga masoko ambapo watu wapo tuna uhakika wa kurudisha hizi fedha. Kwa hiyo pamoja na kuona kwamba kuna miradi hii wafadhili haina fidia basi Mheshimiwa Waziri tafuta chanzo kingine ili tulipe fidia, tujenga miradi maeneo ambayo kuna watu na hasa mradi wa soko na mradi wa vituo vya mabasi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nichangie suala la uhaba wa walimu; kama walivyosema wenzangu kuna changamoto kubwa ya upungufu wa walimu na hapa Mheshimiwa Waziri nimeona umekokotoa upungufu kwa kutumia ratio ya mwalimu mmoja wanafunzi 60 sijui kama ratio hii imebadilika siku hizi lakini mimi ninavyofahamu ratio ili mwalimu aweze kufundisha vizuri kwa kiwango chetu tulijiwekea kwamba darasa la class size darasa moja watoto 45 na mwalimu hivyo hivyo ahudumie watoto 40, hilo darasa la watoto 60 ni wengi sana darasa la wanafunzi 60 halifundishiki. (Makofi)

Kwa hiyo tumeona hapa kwenye takwimu kwamba tunaupungufu mdogo lakini kwa sababu tumetumia ratio kubwa tukirudi kwenye ratio yetu ya zamani kuna uhaba mkubwa wa walimu hili halikwepeki lazima tutoe kibali maalum kwa walimu ili waboreshe elimu yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja na ahsante. (Makofi)