Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Issa Ally Mchungahela

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lulindi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa Rehma kwa kutuweka hai, lakini nikushukuru wewe kwa kunipa fursa hii ya kuchangia pia naomba nikishukuru Chama changu cha Mapinduzi kwa kuniamini, naomba pia niwashukuru wananchi wangu wa Jimbo la Lulindi kwa kuniombea dua kuniwezesha kutimiza malengo yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote niseme kwamba sina deni kwa Wizara yoyote ile, nasema hivi kwa sababu kwa kadri jinsi walivyokuwa wananipa ushirikiano mara zote nilipokuwa nikihitaji chochote mara zote nilivyoomba msaada wamenipa ushirikiano wa kutosha na ninauhakika kwamba wataendelea kunihakikishia kwamba nitakwenda kuwaomba misaada pale nitakapohitaji kwa maana hiyo ndio maana ninasema sina deni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hivyo sina maana ya kwamba hawataniona, wataniona sana kwa sababu jukumu nililopewa na wana Lulindi ni kuhakikisha kwamba ninawaletea maendeleo pale kwao na maendeleo hayawezi kuja hivi hivi kwa mimi kusimama tu, ina maana kwamba lazima niende kila Wizara kuwaomba hayo maendeleo. Nawaomba msinifukuze, nikija mnikaribishe ndugu zangu, ninyi ndio wenye kunisaidia jukumu hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivi Jimbo langu lina uhitaji mkubwa sana kwanini ni Jimbo lina historia na viongozi wakubwa kabisa wa nchi hii, Mheshimiwa Benjamin William Mkapa aliyekuwa Rais wa nchi hii ndiye nyumbani kwake kwenye Jimbo hili na usingizi wake wa milele umelala pale Lupaso. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kuna kila sababu ya kufanya eneo hili liwe na hadhi inayostahili, mimi peke yangu kama Mchungahela sitaweza ndugu zangu naomba ndugu zangu mnisaidie kuhakikisha kwamba Mkapa anapata stahiki yake, lakini Mheshimiwa Anna Abdallah mwanamke shupavu kabisa katika hii nchi amepigania nchi hii, amejitoa kwa nguvu zake, amelitumikia Taifa hili kwa uzalendo mkubwa kabisa, nyumbani kwake ni Jimbo la Lulindi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninawaomba sana ndugu zangu mumpe heshima Mama Anna Abdallah kwa kumwezesha kila kitu ambacho kinaweza kikaonekana pale watu wakaona kwamba hapa ni nyumbani kwa Anna Abdallah. Ninayo kila sababu ya kuwaomba ndugu zangu Wabunge kuna baadhi yenu hapa mmejinasibu sana kwamba mmefanikiwa kupata miradi mingi sana katika maeneo yetu basi mkimuona Mchungahela anapewa miradi mingi msiwe na jealous ya namna yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninawaomba sana sana sana mniunge mkono kwa sababu kuna kila sababu sisi tunahitaji upendeleo na upendeleo huu ni wa umuhimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine sababu iliyotufanya tumechelewa na mpaka kuhitaji upendeleo ni kwamba eneo letu limejishughulisha sana na shughuli ya kuwasaidia wapigania uhuru wa nchi za Kusini mwa Afrika, baada ya kutumia muda mwingi sisi kujishughulisha na masuala yetu ya kimaendeleo kulijenga jimbo lakini shughuli zetu za kawaida tulijishughulisha sana kuwasaidia sana hawa ndugu zetu wakati tukifanya hivyo tumechelewa kupata maendeleo ya kutosha, kwa hiyo, jamani tunayo kila sababu ya kuonewa jicho la huruma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hapo kama nilivyosema TAMISEMI ni Wizara muhimu sana, mara nyingi sana tunaweza tukasema kama ni engine ya bajeti zote ikitumika vizuri tunaweza tukawa na mafanikio makubwa sana kwenye hii nchi na hali hiyo imejitokeza mwaka jana kwa kadri tulivyoona tuliwekewa miradi mingi sana katika maeneo yetu halikadhalika bajeti hii ya mwaka huu inaelekea mwelekeo huo huo, kitu kimoja tu ninawaomba ndugu zangu ambalo tuna jukumu la kufanya kuisimamia hii miradi katika kiwango kinachostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bado hatujafanya vya kutosha kusimamia hii miradi, tunalo jukumu la kuhakikisha miradi hii inasimamiwa na ikaweza kunufaisha wananchi kizazi chetu kinachokuja huko mbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia elimu ambayo ndio msingi wa Maisha kwa kiwango kikubwa kabisa unatekelezwa na TAMISEMI, lakini utekelezaji wake kwa hali ya sasa ilivyo kwamba kuna baadhi ya maeneo kuna malalamiko mengi sana kwamba utekelezaji unachelewa. Ninaomba kutumia vyombo vyetu husika ambavyo vinaweza kutusaidia kwa namna moja au nyingine kwa mfano TAKUKURU iweze kuweka jicho katika miradi hii, TAKUKURU isisubiri mpaka waambiwe na mama kwamba jamani kuna suala la kufanya kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunawomba sana, sana, sana waweke jicho, lakini chombo kingine cha audit unit ninaomba sana sana mara hii ilikuwa ni kipindi cha kutengeneza audit specials nyingi sana katika maeneo yetu huko kusudi angalau kuwatisha hawa watendaji ambao wenye nia tofauti na mahitaji hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hapo nizungumzie suala la Afya kwenye Jimbo langu nina Kata 18, lakini kituo cha afya kinachofanya kazi vizuri katika jimbo zima ni kimoja tu, kuna vituo vingine viwili ambavyo vilishajengwa havijaisha, lakini pia kuna Kituo cha Nagaga ambacho kinahitaji fedha kumalizia. Katika fedha shilingi 500,000,000 zilizotolewa kituo hiki kilipewa shilingi 400,000,000 peke yake na Kituo cha Chungutwa pia kilipewa shilingi 400,000,000 peke yake hivyo kufanya baadhi ya maeneo au baadhi ya miundombinu inayotakiwa katika hivi Vituo vya Afya kutokukamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, alivyopita Makamu wa Rais alituahidi kwamba tushirikiane na TAMISEMI kuhakikisha kwamba tunaangalia ile fedha iliyopungua shilingi 100,000,000 kwa Nagaga na shilingi 100,000,000 kwa Chungutwa inapatikana kwa ajili ya kukamilisha Vituo vya Afya, nasikitika mpaka sasa hivi Mheshimiwa Waziri fedha hii bado haijapatikana licha ya kuwa tumewasiliana mara kwa mara na Wizara yako, sikulaumu lakini najaribu kukumbushia naomba hii shilingi 100,000,000 ya Nagaga ipatikane na shilingi 100,000,000 ya Chungutwa kusudi tuweze kufanikisha ukamilishaji wa Vituo vya Afya hivi, angalau Lulindi na yenyewe ionekane kwamba imepata vituo vya afya vya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninayo mengi sana ya kuzungumza, lakini nikijaribu kuangalia sana naona kama yataingia kwenye lawama wakati mimi nilishajielekeza kusifia Wizara zote katika nchi hii na Mawaziri wote, kitu ninachoweza kusema kwa sasa hivi naomba ushirikiano kwa Wabunge wote pale nitakapokuja kwa namna moja au nyingine kuomba msaada wa kunishauri jambo au kunisaidia jambo mnisaidie…

NAIBU SPIKA: Ahsante kwa mchango mzuri.

MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na naomba kuunga mkono hoja asilimia moa moja. (Makofi)