Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Jesca Jonathani Msambatavangu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Iringa Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi pia niungane na Wabunge wengine kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungnao wa Tanzania Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayofanya katika Taifa letu na hasa kwa kuangalia wananchi wetu wa chini kuhakikisha kwamba anashughulika zaidi na masuala ya elimu na afya na tumeona kwa vitendo siyo kwa maneno. Nimtie moyo kwamba tupo nyuma yake na tutaendelea kupigana na kuhakikisha kwamba kazi inaendelea na zaidi sana kwa kuwa amesimama kama taa ya mabinti zetu na sisi wanawake tutahakikisha haizimi, ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo nitakuwa naongea mambo mawili na hayo yote yanahusu ukatili. Jambo la kwanza nitaongelea ukatili wa kijinsia lakini dhidi ya watoto, lakini nitaongelea pia ukatili wa kiuchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa leo tumekaa hali ya watoto wetu kwenye Taifa hili si salama hata kidogo. Mheshimiwa Waziri amesema hapa kati ya mashtaka yaliyopelekwa mahakamani ya ukatili wa kijinsia asilimia 33 ni kwa ajili ya watoto na 67% ni kwa wanawake. Lakini nimuongezee hajasema wanaume, lakini upo ukatili pia dhidi ya wanaume na tafiti zinaonesha kabisa kiwango cha wanaume kupigwa kimeongezeka mpaka 71.7% wakati wanawake wamepigwa kwa 73.5%. Ukichukua takwimu hizo zinaonesha wanaume wanashuka kwa sababu wao walikuwa juu zaidi kwenye kiwango cha kupiga na wanawake wanapanda kwa kasi kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivi kwa sababu hizi zote zinaonyesha namna gani sasa athari inakwenda kuangukia kwa Watoto, kwa sababu vipigo vinavyoendelea usitahimivu wa ndoa unakuwa haupo, watu wanaachana wanaacha watoto katika hali hatarishi. Katika hiyo 33% watoto wa kiume waliofanyiwa ukatili ni 11.5% na watoto wa kike ni 22%. Tunaposema watoto wa kiume wamefanyiwa ukatili wa kingono maana yake wameingiliwa kinyume cha maumbile. Ipo miaka kumi inayokuja usishangae kuona mtoto wako wa kiume anakuja nyumbani na mkwe wako wa kiume na tusije tukaanza kuleta maneno astaghfilillah, tusije tukaanza kuleta maneno God for bid, tusije tukaanza kuleta maneno Mungu niepushie mbali, atakuwa hajakuepushia mtoto wako wa kiume, atakuwa amekuja na mwanaume mwenzie na anataka kumuoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu katika watoto waliofanyiwa ukatili 3% ndiyo waliopata ushauri nasihi na kutibiwa, 7% wako mitaani na wale wanageuka kuwa makonki master na watoto wa kike 13% tu ndiyo waliopata ushauri. Nasema hivi kwa sababu sisi Iringa tumepata tatizo hili, mtoto mmoja ambaye ameweza kuwalawiti wenzie 19 ndani ya mwezi mmoja, sasa wale saba wanaobaki ambao hawajafanyiwa matibabu wala ushauri nasihi wanarudi mitaani na wanaendeleza ile tabia. Nilivyoongea na yule mtoto aliniambia kwa uchungu sana akaniambia nilifanyiwa matendo haya nikiwa nursery school miaka mitano, leo hii tumepata takwimu kutoka kwa Mheshimiwa Waziri watoto walioandikishwa nursery school ni karibu 1,198,564 lakini watoto walio nje ya shule kwa maana ya pre-primary kwa data zilizoko na utafiti ulioko wa UNICEF ni 61.8%. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hatujaona mpango hapa tumesema tumewaandikisha hawa ni awali na tunapongea awali hawa ni watoto wa shule ya msingi miaka sita chini ya hapo wako nyuma na yule mtoto anasema alifanyiwa akiwa chini ya miaka sita.

Leo aliachwa amekwenda mtaani na akaniambia Mheshimiwa Mbunge nikasema nikusaidiaje kama Mbunge wako maana mtoto ana miaka 13; akaniambia naomba uhamishe watoto wote wanaokaa lile eneo uwapeleke shule ya bweni au uwapeleke kwenye vituo maana yake pale watoto wote ndiyo tunachofanya.

Sasa nikawa nasoma pia maendeleo ya wenzangu Wizara mpya ambayo mama ametuanzishia ya Maendeleo ya Jamii, wanasema wameanzisha kamati za kulinda watoto na wanawake. Kamati 18,186 kati ya kamati 20,750 walizotaka kuanzisha kwenye nchi hii kwa ajili ya kulinda wanawake kwenye mitaa na vijiji, kamati hizo hazipo na hazifanyikazi, hatujaziona. (Makofi)

T A A R I F A

NAIBU SPIKA: Taarifa.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii. Jambo hili la ulawiti kwa watoto wadogo, ukatili wa kijinsia kwa Watoto, limeshika kasi sana katika nchi yetu na kumekuwa na kesi nyingi sana ambazo mwisho wake haueleweki kumekukuwa na rushwa mbalimbali na hakuna hatua madhubuti ambazo zinachukuliwa mimi niombe sasa kupitia hili kwamba Mheshimiwa Mbunge anachokisema ni sahihi kabisa na wale wote watakaobainika basi wahasiwe iwe ndiyo adhabu kubwa ikiwa ni pamoja na kifungo, ahsante.

NAIBU SPIKA: Taarifa hiyo?

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea kasoro ile ya kuhasiwa. Sipokei ya kuhasiwa kwa sababu tuna namna tutawashughulikia na kuwashughulikia hawa kwa sababu zipo sababu zinazosababisha wafanye mambo haya ikiwepo ukata, nitaongezea yaani yale mambo ya uchumi yale.

Sasa hivi mapenzi au huduma ya mapenzi ni product kama product zingine watu wamepunguza purchasing power hawana nguvu ya kununua kwa hiyo wanakwenda kwenye kundi la watoto wadogo na kuwaonea. Kwa nini wamepunguza purchasing power? Ni kwa sababu ya ukatili mbalimbali unaofanyika kwenye jamii kiuchumi ikiwepo pamoja naweza nikasema sasa hivi na sisi tunachangia kama kuna Wizara hapa inafikiria kutowapa kipaumbele Watanzania katika miradi inayotolewa na Serikali hao ndiyo wanaosababisha matatizo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo ukiniambia nguzo za umeme zitanunuliwa nje ya nchi una maana vijana wangu wote walioko Iringa, Songwe, Tanga wote wamepanda miti wakose fedha, watakapokuwa wanahitaji la mapenzi watafanya nini? Kwa sababu kiuhakika sasa hivi hamna mwanamke atakupenda sura kwa sababu wanaume kwanza hawana sura nzuri unampendaje mwanaume sura. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwanamme anapendwa kitu alichonacho anapendwa fedha leo tunapoharibu mazingira ya utendaji kazi wa machinga hatuangalii kama mimi Mheshimiwa Bashungwa Iringa hujanipa hela yoyote ya kuandaa mazingira ya machinga. Wanakaa katika mazingira hatarishi wanapoteza mitaji wale ni watoto wa kiume rijali unategemea unaenda wapi? Inapofika hatua anataka hamu ya mapenzi anafanyaje?

Mheshimiwa Naibu Spika, hayo ndiyo tunayoyasema, lakini pia kuendelea kuwanyanyasa vijana wetu waliojiajiri kwa mfano kwenye bodaboda, kwenye bajaji wanafanya kazi zao unawabana unawanyanyasa kwa leseni wasifanyekazi vizuri una mnyanyasa yule kijana akikosa hela atafanya nini? Huo ndiyo unyanyasaji wa kiuchumi.

Sasa tuhakikishe kwamba Watanzania wanajengewa mazingira mazuri ya kufanyakazi, wanajengewa mazingira mazuri ya tiba, mimi naomba vijana wangu pale watibiwe vizuri zile hela za vijana naomba jamani kutoka mfuko wa Waziri Mkuu shilingi milioni 200 tu tukawawezeshe vijana wa pale wafanyekazi wawe na uwezo wa purchasing power za mapenzi, wasibake watoto wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana tuangaliwe masuala ya huduma za afya tuboreshe, watoto hawa wengine wanabakwa wamekosa nimekuambia ni asilimia tatu katika 11 wanaopata matibabu lakini hata wakienda hospitali sisi tumetoa watoto wengi kuwapeleka Muhimbili pia wakatibiwe baada ya kuwa wamefanyiwa ubakaji hatuna Hospitali ya Wilaya na leo sioni kama imetengwa hapa nimetengewa milioni 500 tu ya kukarabati lakini tuliwaomba tujengewe kwa sababu ile iliyokuwa ya Wilaya mmechukua Mkoa na inahudumia mkoa mzima tunaomba hospitali yetu ya Wilaya ili sisi watoto wetu waweze kutibiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niseme hivi katika masuala ya ukatili haya mimi nasimama leo kama Mheshimiwa Mbunge hapa kwa sababu kuna masuala ya ushirikina yapo ndani yake, sasa ushirikina ni mambo ya rohoni na tunayashughulikia kiroho. Walioko humu ndani watumishi wa Mungu watanielewa, mimi nasema hapa sasa kama Mbunge na ninyi wenzangu kama mnaniunga mkono mtajibu amina mwishoni nasema hivi Mungu tusaidie hatutawafanyia hatutawahasi kama alivyosema Mheshimiwa lakini ninaomba hivi tuachilie nguvu za Mungu kuanzia hapa zikawashughulikie wote kwenye kile kiungo wanachotumia kulawiti watoto wetu, kipigwe nguvu kisifanye kazi na zile mashine mbili zinazozalisha nguvu, zipotee kabisa na madaktari watakapoona mtu mwenye dalili hizo mnitafute ili tumuombee arudi katika hali ya kawaida na tumfanyie counselling ili watoto wetu waendelee kuwa salama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwenye masuala ya kiuchumi tuwatengenezee vijana wetu mazingira rafiki ya kufanyakazi tusiwanyanyase mama ntilie sijui akina nani wanapoonekana wanafanyakazi usimwage bidhaa zao, uangalie namna utakavyotumia hekima kuwasaidia ili wajijengee uchumi. Tumesema hapa tuwape vipaumbele Watanzania kwenye miradi tuwape vipaumbele tuwape elimu ili Watanzania waweze kuwa na purchasing power ya mahitaji yao ya muhimu ikiwepo suala la mapenzi, ahsante. (Makofi)