Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Dr. John Danielson Pallangyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Arumeru-Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kutoa mchango wangu kwa hoja hii ambayo ipo mezani. Nitangulie kwa kuungana na wenzangu waliozungumza hapa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa uhai, afya na nguvu hata tukaweza kukutana hapa leo. Napenda pia kuendelea kuwashukuru wananchi wangu kule Arumeru Mashariki kuendelea kuniamini na niwahakikishie kwamba kazi inaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa dhati kabisa nachukua nafasi hii kumpongeza sana Waziri, Mheshimiwa Bashungwa na Manaibu wake wawili Mheshimiwa Dugange na Mheshimiwa Silinde kwa kazi nzuri sana ambayo wanafanya. Ni vijana wema, wasikivu na ndiyo maana wameimudu hii Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nisipowashukuru na kuwapongeza watendaji wakuu kuanzia Katibu Mkuu na watendaji wengine, nitakuwa sijatenda haki. Nawapongeza watumishi wote kwenye hii Wizara. Ukisoma vizuri hii hotuba ya Waziri wa TAMISEMI, utakubaliana nami kwamba ile reflection ya siku 365 za Rais wetu, Mama Samia Suluhu Hassan akiwa ofisini. Ni kipindi hiki ambacho tumeona utekelezaji wa Ilani chini ya uongozi mahiri wa Mama ukifanyika kwa umahiri mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni katika kipindi hiki, kila Jimbo lilipata shilingi bilioni moja na nusu kwa ajili ya barabara kwa kupitia TARURA. Nasi tulipata hivyo hivyo, tunavyozungumza sasa hivi barabara ya King’ori ambayo nilikuwa naizungumzia hapa mara kwa mara, imefunguka, ni barabara. Nashukuru sana na ninaipongeza Wizara kwa hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna ahadi za viongozi wakuu wa nchi ambazo zilitolewa, hazijatekelezwa. Mwaka 2012 Januari wakati wa maziko ya aliyekuwa Mbunge wetu, Marehemu Jeremiah Sumari, tulipewa ahadi na aliyekuwa Rais wa Awamu ya Nne, kwamba barabara inayoanzia Sangisi kwenda Keri hadi Ndoombwe ingejengwa kwa kiwango la lami. Leo hii ni miaka 10 na ushee, bado ile ahadi haijatekelezwa. Naomba wakati wa kuhitimisha Mheshimiwa Waziri atoe tamko kuhusu barabara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaenda kwenye suala la afya bado kuna ahadi nyingine. Mwaka 2020 Rais wa Awamu ya Tano, Marehemu Dkt. John Pombe Magufuli alitoa ahadi mbele ya wananchi wengi sana pale Usa River kwamba barabara ya King’ori kuanzia maeneo ya Kibaoni hadi Ngare Nanyuki kwa kupitia King’ori Madukani - Maruvango - Leguruki ingejegwa kwa kiwango cha lami. Ninaamini Mheshimiwa Waziri katika kuhitimisha pia atatoa tamko kuhusu ahadi hiyo ya Rais, kwa sababu pia hata kwenye maelezo ya hotuba yake amesema haya mambo ni ilani na ahadi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye afya niseme pia kwamba, ni kwa kipindi hiki cha siku 365 ambapo tumeshuhudia vituo vya afya vinajengwa vingi, nchi nzima. Kule Meru pia nasi tumepata Kituo cha Afya cha King’ori, lakini niseme pia kwamba tuna matatizo ya vituo vya afya. Vituo vingi vya afya kule zilikuwa zahanati, ni maboma yaliyochoka, Mheshimiwa Waziri ukumbuke, ukipata nafasi twende tukatembee uone hali ilivyo kwenye vituo vya afya. Tunashukuru sana tulipata Kituo cha Afya na tulipata pia fedha shilingi milioni 300 kwa ajili ya kujenga Emergence Unit pale kwenye Hospitali ya Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni katika kipindi cha siku 365 tuliweza kupata madarasa 70 ndani wa wiki nane. Ndani ya miezi miwili tulipata madarasa 70 kule Meru, kwa kweli tunapongeza Serikali kwa hilo. Tunashukuru sana, imetupunguzia mzigo, wananchi hawauzi tena kuku wakikimbizana kujenga maboma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niseme kwamba kuna shule nyingi kule Jimboni ambazo zinahitaji ukarabati. Naomba Wizara ilitazame hilo ili ije na operation ya kukarabati zile shule, kwa sababu miundombinu imekaa vibaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na wenzangu pia kuwatetea Madiwani. Kwakweli Madiwani wanafanya kazi kubwa sana kwenye Majimbo yetu, lakini ukiangalia stahiki zao hazitoshelezi. Wanapata sitting lakini wanahangaika huku na kule kusimamia miradi ambayo inatekelezwa kwa fedha za ndani, lakini pia na fedha ambazo zinatoka Serikali Kuu. Wakati umefika sasa tuangalie maslahi yao. Wabunge wamesema nadhani Mheshimiwa Waziri utaliangalia hilo ili Madiwani wetu wapate ahueni kwenye bajeti inayokuja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kukushukuru sana kwa kunipa nafasi nami nitoe mchango wangu huo kwa ufupi sana. Ahsante sana. (Makofi)