Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Joseph Zacharius Kamonga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ludewa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kukushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia bajeti hii ya Wizara ya TAMISEMI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Jimbo la Ludewa walinizuia kabisa leo kumpongeza Mheshimiwa Bashungwa kwa sababu wana changamoto hasa wale wananchi wa Mwambao, lakini kwa namna Mheshimiwa Bashungwa alivyo muungwana, ukimpigia simu anapokea na juzi nimewasilisha changamoto zangu mbalimbali za Jimboni ikiwemo kile kituo cha afya cha Mundindi wamekamilisha ujenzi, lakini wanakosa vifaa tiba ili waweze kuanza kutao huduma. Nilimpigia Mheshimiwa Waziri usiku alipokea simu na alinisikiliza vizuri. Kwa hiyo, kwa namna hiyo na kwa jinsi Mheshimiwa Waziri alivyo mnyenyekevu na Manaibu wake, nitakuwa sio muugwana nisipompongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na kutoa pongezi kwa Serikali kupitia Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI, Jimboni Ludewa kuna changamoto ambazo ningependa Mheshimiwa Waziri azitilie maanani. Kuna Tarafa ya Mwambao ambayo ipo kando kando ya Ziwa Nyasa. Tarafa hii kwa miaka mingi walikuwa wanategemea usafiri wa meli, bahati mbaya ile meli imekuwa na changamoto na muda mwingi haifanyi kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tarafa hii ina Kata nne ambazo hazijaunganishwa kabisa kwa barabara. Kuna Kata ya Lifuma haifikiki kwa gari na wananchi hawajawahi kuwa na gari maisha yao yote, kuna Kata na Makonde haifikiki kwa gari na wananchi hawajawahi kuona gari maisha yao yote, kuna Kata ya Kilondo na Kata ya Lumbila.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo jitihada za Serikali kupitia TARURA, nilikwenda kwa CEO wa TARURA nikiwa na Madiwani wangu, waliweza kuwasikiliza vizuri, lakini changamoto kubwa, bajeti ambayo wanapewa kwa ajili ya hizi barabara ni finyu sana. Kwa hiyo, naomba Serikali iweze kuwaongezea fedha hawa watu wa TARURA na ikiwezekana wahandisi kutoka TARURA Makao Makuu waende wakasaidiane na wale walioko Mkoani na Jimboni, wafanye tathmini maana wananchi wa huku wanaona kama Serikali imewasahau na wanaona mimi Mbunge wao kama siwasemei. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri naomba ulipe uzito. Kimsingi kuna barabara nyingine kupitia TARURA nazo wamekuwa wakifanya kazi nzuri, lakini changamoto ni bajeti wanayopewa, haitoshelezi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi nilikwenda kuwapa pole wananchi wa Kiogo; kutoka pale Masasi kwenda Kiogo, barabara ni changamoto kubwa. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri, siku ile nilimwona Mheshimiwa Bashe wakati anazungumzia mapinduzi ya Kilimo; Kilimo Biashara, alikupa nafasi ulizungumza pale. Kwa hiyo, mimi ni miongoni mwa Wabunge ambao tunaamini maendeleo na mapinduzi ya kilimo yanaenda sambamba na kuboreshwa kwa barabara za vijijini. Kwa sababu kama Wizara ya Kilimo watakuwa wamepewa bajeti kubwa, halafu TAMISEMI kupitia TARURA wananchi wanalima mazao halafu hawawezi kuyatoa shambani kuyafikisha kwa walaji, kwa kweli hata ufanisi wa kilimo biashara utakuwa mdogo sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana barabara za vijijini; na ninamshukuru pia Mheshimiwa Waziri siku ile aliona clip ya gari iliyokuwa inapata shida kwenye Kijiji cha Ilininda, wananchi wanahangaika sana kwenye matope. Mheshimiwa Waziri alinitafuta na kuniambia kwamba anataka kwenda kule. Nakushukuru alitoa maelekezo kupitia TARURA, wameanza kujenga zile concrete strips. Kwa hiyo, ninaamini ule ni ufumbuzi wa kudumu. Kwa hiyo, nakuomba ahadi yake ya kutembelea Jimbo la Ludewa ibakie pale pale kwa sababu kumekuwa kuna malalamiko ya wananchi kwamba Waheshimiwa Mawaziri wengi wanarudia pale Njombe, hawaendi Ludewa kule kusikiliza changamoto na nimaamini sasa tutaendelea kupata Mawaziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto nyingine ambayo inalikabili Jimbo la Ludewa ni uhaba wa watumishi. Unakuta shule ya msingi ina walimu watatu; mmoja yupo masomoni, mwingine yupo maternity leave, shule imebaki na mwalimu mmoja, labda na walimu wawili au watatu wa kujitolea. Hawa walimu wa kujitolea nafasi zinavyotangazwa Serikalini nao hawapewi kipaumbele cha kupata ajira. Changamoto ya kule walimu wengi wakipelekwa wanahama. Kwa hiyo, naomba wale wanaojitolea kule Mheshimiwa Waziri nipo tayari kukuletea orodha ili wapewe kipaumbele cha kupata ajira kwenye sekta ya elimu na afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ludewa tuna upungufu wa watumishi 986, wengi ni kwenye sekta ya elimu na afya. Kwa hiyo, naomba kwenye ajira hizi Ludewa tuweze kupata kipaumbele ili tuwaondolee wazazi usumbufu wa kuchangishwa fedha ili kulipa walimu wanaojitolea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Ludewa wamejitolea sana kujenga vituo vya afya kata saba, lakini havijakamilika muda mrefu. Kwa hiyo, hili nalo naomba Mheshimiwa Waziri alichukue kwa sababu tulishazungumza ili wananchi jasho lao lisipotee bure.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya haya machache. naunga mkono hoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. (Makofi)