Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Daniel Edward Mtuka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Manyoni Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. DANIEL E. MTUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi hii. Nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuamsha leo salama na mimi kwa kupata nafasi hii ya kuweza kuchangia.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niseme naipongeza hotuba ya Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, ni nzuri, iko vizuri na imekaa vizuri. Nimpongeze Amiri Jeshi Mkuu, Mheshimiwa Dkt. Magufuli, anafanya kazi nzuri, yuko imara na jeshi liko imara. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika niende moja kwa moja kwenye hoja yangu. Ukitazama Sheria ya Jeshi la Kujenga Taifa, Cap. Na. 193 ya mwaka 2010, (R.E), kifungu cha 6(2) kinataja umri wa mtu au umri wa Mtanzania kwenda Jeshi la Kujenga Taifa, ni kati ya miaka 16 – 35. Kwa nini nataja vifungu hivi? Nchi yetu zaidi ya 60% ni vijana na vijana ndiyo nguvu kazi ya kujenga nchi hii. Tusipowalea vijana vizuri, tusipowajenga vijana vizuri hakika mustakabali wa nchi yetu na hasa kwenda kwenye maendeleo na hasa kuipeleka nchi yetu katika uchumi wa kati itatuchukua muda mrefu sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunahitaji tuwajenge vijana katika uzalendo waipende nchi yao. Tuwajenge vijana katika utii na nidhamu, tuwape stadi za kazi, tuwape uaminifu ili wawe wanaitika kwa sauti moja ya kiongozi anaposema, nchi hii itakwenda vizuri, nilitaka nilisisitize hili. Hakuna chombo kingine kikubwa ambacho kinaweza kuwarekebisha vijana hawa, naliona Jeshi la Kujenga Taifa hata JKU – Zanzibar, ni vyombo vya muhimu sana katika kuandaa vijana wetu. Ni vya muhimu sana! Naomba tuwekeze vilivyo kwenye majeshi haya, Jeshi la Kujenga Taifa na JKU. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tuwekeze kwa namna gani? Wengi wamechangia hapa, kuna chuo kikubwa cha VETA kinataka kujengwa Kongwa, naomba tuharakishe ujenzi huu, tuwapeleke vijana wetu huko VETA. Hata kwenye makambi, namkumbuka sana Mwalimu Nyerere, namkumbuka sana Mzee Karume, walipoanzisha majeshi haya waliainisha maeneo muhimu sana ambayo mpaka sasa hivi tunayatumia kwenye kambi za Jeshi la Kujenga Taifa na Jeshi la Kujenga Uchumi. Kuna maeneo mazuri ya kilimo, mimi nimepitia pia, tulikuwa Mgambo Tanga kule, tulikuwa tunalima mahindi Gendagenda, tulikuwa tunalima machungwa na maeneo mengine kama Itende na Chita, yamekaa vizuri kwa ajili ya uchumi. Tukiwekeza vizuri hawa hawa vijana watazalisha, watajilisha na watailisha nchi lakini tutakwenda kwa pamoja wakiwa watii ndani ya jeshi na kupitia Jeshi la Kujenga Taifa.
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme jambo moja la msingi sana. Nimesikia maneno ya Msemaji wa Kambi ya Upinzani, amesema mambo mazuri, mimi ni muungwana, mnyonge mnyongeni lakini haki yake mpeni. Kwenye mazuri mtu nitampongeza, akikengeuka nitamwambia hapo hapana!
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna jambo moja alilisema, sim-quote lakini najaribu kutoa tu ile maana kwamba anashangaa Mheshimiwa Rais anateua Wanajeshi wastaafu kuwa viongozi kwa mfano Wakuu wa Wilaya, Wakuu wa Mikoa kwamba hawa wasingekwenda huko kwa sababu ni Wanajeshi. Mimi nasema hapana! Hawa ni reserve army, reserve army ni yule mtu ambaye amekwenda jeshi either amepata kazi au hajapata lakini ni reserve army, lazima tumtumie. Amejifunza utii, anaweza kufanya kazi na ni mzalendo huyu na wamefanya kazi nzuri sana watu hawa. Tunawaona wanachapa kazi sana hawa Wanajeshi, kwa mfano Wakuu wa Mikoa tumeona wanafanya kazi nzuri sana, tuwatumie. Hiyo ndiyo maana ya jeshi la akiba. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nihame hapo niseme jambo moja kuhusu nafasi hizi za kwenda Jeshi la Kujenga Taifa. Vijana wako tayari kila mahali kwenda Jeshi la Kujenga Taifa lakini kumekuwa na ukiritimba kwenye nafasi hizi. Nadhani nafasi hizi zimegawanywa kimikoa na kiwilaya, kila wilaya na mikoa ina nafasi zake. Naomba tulisimamie vizuri suala hili kwa mfano Mkoa wa Singida wanatoa vijana kutoka Arusha wanawaleta Mkoa wa Singida. Wale viongozi, washauri wa Mgambo wanatawala zoezi hili, wanawanyima haki wale vijana wa kwenye maeneo yale. Naomba mlisimamie vizuri jambo hili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la tatu. Tuliomba hapa wakati tunachangia Wizara ya Kilimo kwamba Wanajeshi wakati wa amani wasaidie maeneo mengine. Tuna vyombo hivi, wana ma-grader, vijiko, malori ya ujenzi, hebu vyombo hivi vitumike kutusaidia kwa mfano kuchimba labda mabwawa na kujenga barabara, wananchi tuko tayari kuchangia mafuta.
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mtuka muda wako umekwisha.
MHE. DANIEL E. MTUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja hii mia kwa mia. Ahsante sana.