Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Timotheo Paul Mnzava

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kutoa mchango wangu kwenye bajeti ya Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa. Awali kabisa, namshukuru sana Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema, ambaye ametujalia uzima, ametuwezesha kuwa pamoja humu kuifanya kazi hii nzuri ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili, nampongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye ndiye msimamizi wa Wizara hii, maana ni Wizara iliyo chini ya Ofisi yake kwa kazi nzuri ambayo anaifanya kwa nchi yetu na kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee nampongeza sana Ndugu yangu Mheshimiwa Innocent Bashungwa kwa kuteuliwa kuwa Waziri wa TAMISEMI, na Manaibu wao kwa kuendelea kuaminiwa. Naamini kazi hii ataifanya vizuri, ana timu nzuri TAMISEMI. Nampongeza pia Katibu Mkuu, Profesa Shemdoe na timu yake ya Manaibu Katibu Wakuu, wanafanya kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya pongezi hizo nitumie nafasi hii kutoa mchango wangu kwenye maeneo machache. Eneo la kwanza ni miundombinu ya barabara vijijini. Hapa naizungumzia TARURA. Kipekee kabisa, naipongeza sana Serikali kwa kazi nzuri tuliyoifanya ya kuongeza fedha kwa ajili ya kushughulikia barabara za vijijini. Nikitoa mfano, kule Korogwe tulikuwa na bajeti ya shilingi 670,000,000 kwa miaka kama mitatu mfululizo, lakini kwa mwaka wa fedha tuliokuwa nao, tumepokea zaidi ya shilingi 1,400,000,000/= kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa barabara za vijijini, pia tumepokea shilingi bilioni tatu kwa ajili ya ujenzi wa daraja kubwa kule Mswaha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee, kwenye fedha hizi namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kukubali kutoa zile shilingi 500,000,000 za Jimbo kupitia kwa Wabunge kwenda kufanya matengenezo ya barabara. Kwa kweli TARURA wamejitahidi kufanya kazi nzuri. Pamoja na kujitahidi kufanya kazi nzuri, yapo maeneo manne naomba nishauri. Eneo la kwanza, pamoja na kuwa fedha zimeongezwa, lakini ukweli ni kwamba bado mahitaji ya fedha kwa ajili ya barabara za vijijini ni makubwa. Naiomba Serikali iendelee kuangalia namna ya kuongeza bajeti kwa ajili ya TARURA ili waendelee kupata fedha nyingi zaidi kufanya miradi mingi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la pili tuwaombe TARURA, Serikali imekubali kuongeza fedha, na kama Wabunge tunaendelea kuomba fedha iongezwe zaidi; tujitahidi kubuni na kuweka mfumo mzuri wa usimamizi wa matumizi ya hizi fedha ili kazi inayofanywa kwa fedha hizi iwe na thamani halisi ya fedha ambayo imetolewa na Serikali ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la tatu ni la teknolojia. Wakati fulani tumemsikia Mheshimiwa Rais akishauri kwamba kuna teknolojia nzuri iliwahi kuja hapa lakini haikuwahi kufanya kazi, ikaenda maeneo mengine. Ni kweli tunatoa fedha nyingi tunatengeneza barabara na kukarabati, lakini ukweli ni kwamba barabara zetu za vijijini, wanamaliza kutengeneza, ikinyesha mvua ya siku moja, barabara hazipitiki tena. Ni lazima kama nchi tufikirie teknolojia nyingine sahihi zaidi itakayosaidia matengenezo yanayofanywa kwenye barabara zetu yaweze kukaa muda mrefu na wananchi wetu wanufaike na matunda ya kazi hii nzuri iliyofanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la nne na la mwisho la kushauri kwenye TARURA, tumeona iko miradi mingi ya barabara inafanyika kwa maeneo ya mijini hasa kwenye maeneo ya Makao Makuu ya Halmashauri ambazo ni za Miji na Manispaa. Maeneo yetu sisi tunaotoka maeneo ya vijijini, tunayo miji ambayo pia ni centre kubwa na nzuri za kibiashara, tuwaombe TAMISEMI kuwaomba TARURA, fikirieni namna ya kuwa na maandiko ya kutafuta fedha kwa ajili ya maeneo haya. Siyo maeneo haya tu peke yake, nimeona kwenye bajeti mnaendelea kuzungumzia kuhusu miradi maalum ya maeneo yale ya uzalishaji, na sehemu kubwa nimeona mnazungumzia eneo moja tu la kule nyanda za juu Kusini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Tanga, Wilaya ya Handeni, Korogwe na Muheza ndiyo zinaongoza kwa kilimo cha Mkonge. Leo tunavyozungumza, moja ya changamoto kubwa wanayopata wanachi wetu na wakulima wadogo wadogo wa Mkonge, ni miundombinu ya kutoa mkonge kutoka mashambani kupeleka kwenye viwanda vya kuchakata. Pia eneo la Lushoto na eneo la milimani la Korogwe kuna kilimo kikubwa sana cha chai, lakini kwa muda mrefu tumesahaulika. Tunaomba TARURA ije na miradi ya namna hii pia kwenye maeneo ya mkonge na maeneo ya chai ili tusaidie kuongeza thamani ya mazao ya wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ni Afya. Tunaishukuru Serikali imefanya kazi nzuri kwenye eneo la ujenzi wa vituo vya afya na pia kwenye kukamilisha maboma ya Zahanati. Nimemsikia ndugu yangu, Mheshimiwa Mabula hapa amesema tuendelee kupunguza bajeti ya ujenzi. Mimi nasema mwendelee kupunguza bajeti ya Ujenzi lakini kwa wale wa mjini kama Nyamagama.

Mheshimiwa Spika, kwa sisi wa vijijini kama Korogwe, miundombinu ni muhimu na vifaa tiba ni muhimu na vyote hivyo ni lazima viende kwa pamoja. Leo ninapozungumza Korogwe vijijini, nina maboma zaidi ya 24 ambayo…

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Mnzava kuna taarifa kutoka kwa Mbunge wa Nyamagana, Mwanza Mheshimiwa Stanslaus Mabula.

T A A R I F A

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, naomba kumpa taarifa mzungumzaji ya kwamba hoja ya kupunguza ujenzi haimaanini kuacha ujenzi. Kwa hiyo, kama Korogwe wana uhitaji zaidi wa ujenzi, watajengewa, lakini hoja yangu ya msingi ni kwamba ujenzi uambatane na vifaa zaidi. Sasa sijui kama yeye anaiona hiyo haifai au inafaa, ataichukua. Nakushukuru sana. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Timotheo Mnzava, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, naipokea na ninajua imemsaidia na yeye kufafanua jambo hili kwa wapiga kura wake kule, sasa wamemwelewa. Mwanzoni hawakuwa wamemwelewa, ndiyo maana nimesema, ujenzi huu uendane na vifaa tiba. Vifaa tiba ni muhimu na ujenzi ni muhimu. Nimesema, kwa mfano Korogwe Vijijini, nina maboma sasa hivi zaidi ya 24 ya Zahanati ambayo yanahitaji kukamilishwa ili wananchi wetu waweze kupata huduma. Ukiwaambia wananchi unaacha, unaweka nguvu kwenye vifaa tiba, tunawavunja moyo. Mambo haya yaende kwa pamoja.

Mheshimiwa Spika, nampongeza Mheshimiwa Rais, pamoja na Sera na Ilani kusema tuwe na Kituo cha Afya kwenye kila Kata, tuwe na Zahanati kwenye kila Kijiji, utekelezaji wake ulionekana ni mgumu. Alipoingia Mheshimiwa Rais, Mama Samia, amesema angalau tujihakikishie kila Tarafa kuwa na Kituo cha Afya. Nasi tunashukuru, Tarafa yetu ya Korogwe ambayo ilikuwa haina kituo cha Afya hata kimoja, imepata Kituo cha Afya cha Mnyuzi, shilingi milioni 500, tunaishukuru Serikali. Naiomba sana TAMISEMI, tusimchonganishe Mheshimiwa Rais na wananchi wake. Nikitoa mfano wa Korogwe, nina Tarafa nne; Tarafa moja ya Bungwi ina Kata tisa; ina Kituo cha Afya kimoja; hawajapata kituo afya kingine kwa sababu tayari wana kituo cha Afya.

Mheshimiwa Spika, lakini kituo hicho walichokuwanacho, hata operation hakifanyi. Huduma za upasuaji hakuna, ni cha muda mrefu, ni kikongwe na chakakavu. Kuna kituo cha Afya cha Magoma. Pamoja na miradi hii ya vituo vya afya tuliyokuwa nayo ya kila Tarafa na inavyoendelea, tunaomba sana, vituo vya afya za zamani, vikongwe na vichakavu, viboreshwe ili wananchi wetu waweze kupata huduma. Kwenye hili la Vituo vya Afya, siyo tu majengo, pamoja na hivyo vifaa tiba, lakini tuna changamoto kubwa sana ya watumishi kwenye sekta ya afya na kwenye sekta ya elimu. Tunawaomba sana TAMISEMI tulingalie hili kwa uzito wake liweze kwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la mwisho ni la usimamizi wa Serikali za Mitaa. Tunaendelea kusema, Wabunge wote ni mashahidi, muda tunaotumia Majimboni ni mdogo sana, muda mwingi tupo kwenye vikao vya Bunge karibu nusu ya mwaka, tupo huku Bungeni. Wanaotusaidia kufanya kazi vizuri ni Waheshimiwa Madiwani. Naiomba Serikali, tuangalie namna ya kuboresha maslahi ya Madiwani wetu. Fedha wanayopata, kiwango cha posho yao ni kidogo na kimekaa kwa muda mrefu. Tuna Madiwani karibu 4,500; Serikali ikiamua kutenga shilingi bilioni 30 kwa mwaka, tunawaongezea nguvu hawa Madiwani wanafanya kazi yao vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia na Wenyeviti wetu wa Serikali za Mitaa, naomba nao tuangalie namna ya kuweza kuwaongezea uwezo waweze kufanya vizuri.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana. Naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)