Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Stella Ikupa Alex

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Spika, nami nakushukuru kwa nafasi hii ya kuweza kuchangia katika Hotuba ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote naomba nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa jinsi anavyonilinda, anavyonitetea na anavyonipigania katika majukumu yangu ya kila siku. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa ajili ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa jinsi anavyoendelea kumpa hekima, busara na maarifa ya kuliongoza Taifa letu. Nina hakika tunaona ni kwa jinsi gani anavyoendelea kuupiga mwingi kwenye maeneo mbalimbali, yaani kwenye sekta mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nitumie nafasi hii kuishukuru sana Serikali ya Chama cha Mapinduzi ambayo inaongozwa na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kwa jinsi ambavyo imeendelea kuyapa kipaumbele masuala mbalimbali ya watu wenye ulemavu. Tukianzia kwenye Hotuba ya Ofisi ya Waziri Mkuu, ilieleza mambo mengi kwenye eneo la watu wenye ulemavu; na pia kwenye Hotuba hii ya TAMISEMI, imeeleza mambo mengi ambayo yanatarajiwa kufanyika na yale ambayo yameshafanyika.

Mheshimiwa Spika, mojawapo ambalo lilikuwa ni changamoto kubwa kwenye maeneo ya shule zetu, ni uzio. Shule nyingi zilikuwa hazina uzio ambapo sasa ilikuwa inasababisha kuhatarisha maisha ya watoto mbalimbali na hasa ikizingatiwa kwamba, watoto wengi kwenye maeneo hayo unakuta ni walemavu wa akili, pia kuna watoto wenye ualbino, kwa hiyo, ilikuwa ni changamoto kubwa. Naipongeza sana Serikali kwa kutenga fedha kwa ajili ya kuhakikisha kwamba changamoto hii inaenda kutoweka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia, naipongeza na kuishukuru sana Serikali kwa kutenga fedha kwa ajili ya kujenga mabweni kwenye shule za watoto wenye ulemavu. Kwenye maeneo mengi watoto wanashindwa kwenda shule kwa sababu ya umbali, lakini sasa uwepo wa mabweni haya utawezesha watoto wengi wenye ulemavu kuweza kusoma na hatimaye kuwa na uhakika wa masomo yao kwa kadiri ambavyo wanaendelea. Kwa kweli sisi kama watu wenye ulemavu Tanzania, tunaishukuru sana Serikali na tunaendelea kuiombea mipango hii iweze kutekelezeka kwa wakati kama ambavyo imepangwa.

Mheshimiwa Spika, katika hotuba hii pia limeongelewa suala zima la utambuzi wa watu wenye ulemavu. Pale ambapo suala hili la kuwatambua watu wenye ulemavu limefanyika imekuwa ni vizuri kwa sababu, wanapotambuliwa inakuwa pia ni rahisi kufahamu na mahitaji yake. Hotuba imeeleza wazi kwamba, wamewatambua na hatimaye wameweza kuwapatia mahitaji mbalimbali miongoni mwa wale waliotambuliwa. Hivyo pia, nikiwa kama mwakilishi wao, ninawashukuru sana na kuishukuru sana Serikali ya Chama cha Mapinduzi chini ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, limeendelea zoezi la uandikishwaji watoto kwa maana ya kuanzia elimu ya awali, msingi na kuendelea; na tunaona kabisa kwamba idadi ya uandikishwaji inaongezeka. Ilikuwa ni kilio cha muda mrefu na changamoto kubwa kwamba, watoto wengi wenye ulemavu walikuwa hawaendi shule, lakini kwa trend hii inayoendelea, tunaona kabisa kwamba kundi hili la watu wenye ulemavu hawaachwi nyuma na hatimaye na wao wanaenda kupata elimu kama watoto wengine. Ninaishukuru sana Serikali ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Spika, pamoja na pongezi hizi, yako mambo mengi ambayo yamefanyika kwa mujibu wa hotuba hii, na kwa kadiri ya ambavyo tunayaona sisi watu wenye ulemavu. Kipekee kabisa nilete salamu nyingi za watu wenye ulemavu kwa Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan. Tunamshukuru Rais wetu kwa sababu aliweza kutualika Ikulu ya Chamwino, tukakaa naye, tukazungumza naye, tukawasilisha changamoto zetu mbalimbali ambazo kwa kweli, Mheshimiwa Rais changamoto zile, nyingi zimeshaanza kufanyiwa kazi na nyingine zimeshapata suluhisho na nyingine ziko katika hatua ya utekelezaji. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na pongezi hizo kuna baadhi ya changamoto ambazo ninaomba niziwasilishe mbele ya Serikali. Changamoto ya kwanza ni utolewaji wa mafuta ya watu wenye ualbino kwenye Halmashauri zetu. Hii imekuwa ni changamoto ya muda mrefu; miongozo ipo, kanuni zinaongea wazi, lakini suala hili halitekelezeki kwenye Halmashauri zetu. Nimekuwa nikipokea simu mbalimbali kutoka kwa watu wenye ulemavu wakilalamikia suala hili kwamba, Halmashauri hazitoi mafuta haya.

Mheshimiwa Spika, nimekuwa nikisema kwamba mahitaji ya watu wenye ulemavu ni kama chakula. Vile ambavyo binadamu mwingine anahitaji kula, hivyo, mahitaji haya ni ya muhimu sana kwa kundi hili la watu wenye ulemavu. Naiomba Serikali, suala hili liweze kutekelezeka kwa maana ya kwamba, Halmashauri ziweze kutenga, kununua na kusambaza mafuta haya kwa watu wenye ualbino. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mbali na hilo, namwomba Waziri anapokuja kuhitimisha, basi aweze kulielezea suala hili kwa kina, ni kwa nini halitekelezeki? Pia, niseme wazi kwamba, maelezo ya Mheshimiwa Waziri yasiponitosheleza, nitashika shilingi yake na nitaondoka na huo mshahara wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vile vile ieleweke wazi kwamba familia nyingi ama watu wenye ulemavu walio wengi wanaishi kwenye kipato cha chini sana kiasi cha kushindwa kumudu matibabu yao. Naishauri na kuiomba Serikali iweze kufanya zoezi ambalo lilifanyika kwa wazee, kuwatambua na kuwapatia vitambulisho wale ambao hawana uwezo wa kupata matibabu ili basi, vitambulisho vile viwawezeshe kutibiwa kwa urahisi.

Mheshimiwa Spika, suala hili ni muhimu sana kwa sababu, wengi wanapata changamoto kubwa. Sasa unakuta mtu anakupigia simu, Mbunge nisaidie matitabu; na idadi ilivyo kubwa unajikuta unashindwa kusaidia kwa ukamilifu wake kwa wale ambao wana uhitaji. Hivyo, naiomba Serikali iweze kuwatambua watu wote ambao wanashindwa kumudu matibabu kama ilivyofanya kwa wazee. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia kabisa, kwa sababu muda umekuwa siyo rafiki, niwahamasishe watu wenye ulemavu kujitokeza kwa wingi kuweza kuhesabiwa, lakini pia elimu hii kwa wale viongozi wa watu wenye ulemavu waweze kuitoa kwa wenzao. Kwa maana kuhesabiwa ni muhimu, yamkini mambo mengi hayatekelezeki kwa sababu Serikali haina idadi yetu kamili. Hivyo, niwaombe sana watu wenye ulemavu wajitokeze kuhesabiwa; na pia watu ambao wanaishi na watu wenye ulemavu wasiwafiche kuhesabiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa nafasi. (Makofi)