Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. George Boniface Simbachawene

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibakwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa nami ni mara yangu ya kwanza kuzungumza ndani ya Bunge lako Tukufu, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kunijalia afya na uhai mpaka kufika siku ya leo, lakini kwa namna ya pekee sana nimshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuniamini na kunipa jukumu hili la kuwa Waziri katika Ofisi ya Waziri Mkuu ninaeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu nataka nimuhakikishie Mheshimiwa Rais kwamba kazi hii nitaifanya kwa umahiri mkubwa, kwa uadilifu mkubwa na jitihada zote katika kuhakikisha kwamba namsaidia Mheshimiwa Waziri Mkuu katika kazi yake iweze kuwa na mafanikio makubwa.

Mheshimiwa Spika, ninamshukuru tena Makamu wa Rais Dkt. Philip Isdor Mpango kwa namna ambavyo anamsaidia Mheshimiwa Rais pia anatusaidia na Waheshimiwa Mawaziri katika kutekeleza majukumu yetu.

Mheshimiwa Spika, pia nimshukuru sana Rais wa Zanzibar Dkt. Hussein Ali Mwinyi kwa namna alivyofanya mageuzi makubwa kule Zanzibar na kufanya Zanzibar iwe kama inavyoonekana sasa katika hali nzuri kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu ambae ndiyo mwenye hoja hii ambayo iko mbele tu nianze kabisa kwa kuiunga hoja hii mkono kwa ailimia 100 na ninawasihi na kuwaomba Waheshimiwa Wabunge wote kama ambavyo mmekuwa mkifanya tuendelee kuiunga mkono hoja hii, maana hoja hii Mheshimiwa Waziri Mkuu pia anashika Fungu la Bunge na kwa hivyo tusipoiunga mkono sijui tutaendeleaje na shughuli zetu hapa, kwa hivyo niwaombe na niwasihi pia tuunge mkono hoja hii ili mambo yetu yaweze kwenda sawa sawa.

Mheshimiwa Spika, nami naamini katika hili ni pande zote na hata wenzetu wa Upinzani walio wachache watatusaidia katika kuunga mkono hoja ili shughuli ziweze kufanyika na tutekeleze majukumu yetu ambayo wananchi wametuleta humu ndani.

Mheshimiwa Spika, ninakupongeza wewe kwa namna unavyoliongoza Bunge pia Mwenyekiti wetu wa Kamati ambapo mimi ninadondokea katika Kamati mbili. Kamati ya Katiba na Sheria na Kamati ya UKIMWI na magonjwa yasiyo ambukiza, Wenyeviti wangu hawa wawili pamoja na Wajumbe wa Kamati hizi tumeshirikiana nao vizuri sana katika maandalizi yote ya bajeti hii na hata katika hotuba walioitoa yote yale ambayo wameyasema niseme kwa ujumla wake kwa kuwa siyo rahisi kuyajibu moja moja tunayachukua yote na tutaendelea kufanyanao kazi kwa pamoja na kuhakikisha kwamba yale wanayotushauri, yale wanayosimamia yote tunayatekeleza kadri Mungu atakavyoweza kutujalia.

Mheshimiwa Spika, baadhi ya mambo yanayosemwa hapa mengi yanadondokea katika taarifa za Kamati, nianze tu kupongeza taarifa zote na kwamba baadhi ya hoja ambazo zimezungumzwa na hasa Kamati ya Katiba na Sheria, Mheshimiwa Joseph Kizito Mhagama alikuwa na maelezo ambayo yalibeba ujumbe wa Kamati na kutoa maoni mbalimbali kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nami nitayajibu kwa mujibu wa Kanuni (99) (2) Kanuni za Kudumu za Bunge Toleo la Januari mwaka 2016 ambaye inaruhusu kujadili utekelezaji wa bajeti za Wizara.

Mheshimiwa Spika, hoja ya kwanza ilikuwa ni suala la kupanua wigo wa wapiga kura, idadi inayopiga kura ni wachache, kwa hiyo Kamati ina maoni kwamba lazima kazi ifanyike ili kuweza kupeleka elimu na kutia hamasa ya wanachi wengi kupiga kura kadri inavyowezekana, hili tunalichukua pia Kifungu cha Sheria Na. 4(c) cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi Sura 343 kinatoa jukumu hili kwa Tume ya Uchaguzi kuhakikisha kwamba inatoa elimu kwa wapiga kura na kuhakikisha kwamba idadi ya wapiga kura inaongezeka na kuwa ya kutosha kulingana na idadi ya population ya nchi.

Mheshimiwa Spika, pia hakujafungwa taasisi na asasi za kiraia na viongozi mbalimbali wa kijamii msisitizo wangu hapa na wenyewe tuchukue jukumu la kuhakikisha kwamba tunawaelimisha wananchi wetu umuhimu wa kushiriki katika zoezi la kupiga kura, kwa sababu ndiyo mahala pekee ambapo kwa maoni na uchaguzi wao wanakuwa na maoni yao ya jumla nini wanataka katika Taifa lao litokee.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine la pili, ambalo ni maoni ya Kamati ni kuhuishwa kwa daftari la wapigakura. Sheria ya uchaguzi Sura 343 ya Tume ya Uchaguzi inapaswa kuboresha daftari hili mara mbili kila baada ya uchaguzi na kabla ya uchaguzi unaofuata na jambo hili limekuwa likifanyika na kwa hivyo niendelee kusisitiza tu kuendelea kufanyika kwa jambo hili kwa maana ni jambo la msingi kuhakikisha kwamba daftari hili linaboreshwa kila mara.

Mheshimiwa Spika, pia ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa itoe elimu kwa Wasimamizi na Wasaidizi wa Uchaguzi kwa Vyama vya Siasa na wagombea kuhusu sheria zinazosimamia uchaguzi. Sheria ya Vyama vya Siasa Sura Na. 258, Ofisi ya Msajili inajukumu la kutoa elimu hii kwa umma, kwa Wagombea, kwa Vyama vya Siasa ili kuhakikisha kwamba demokrasia inasimamiwa katika misingi ya kisheria lakini na kudumisha amani.

Mheshimiwa Spika, eneo la Nne ilikuwa ni kuhuisha taarifa za vyama vya siasa katika register za kisheria, hili ilizungumzwa na Kamati niendelee kusema tu ofisi ya Msajili huwa inapaswa kufanya kazi hiyo, jambo muhimu hapa ni kwa vyama vyenyewe vya siasa kuhakikisha kwamba vinatoa taarifa zao kwa wakati kwa Msajili ili ziweze kuingizwa kwenye record na madaftari hayo.

Mheshimiwa Spika, pia eneo lingine la tano ilikuwa ni Ofisi ya Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali kuendelea kuimarishwa lakini pia kasoro ndogondogo za usajili wa mapato, nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge na Kamati kwamba tutaendelea kuboresha na kuhakikisha kwamba maduhuli yanakusanywa lakini pia kuboresha ofisi hii, Serikali imetenga fedha kiasi katika bajeti iliyopita kiasi cha Shilingi Bilioni 2.5 ambazo Serikali imeahidi kuzitoa katika mwezi huu wa Aprili, lakini Mkandarasi amekwishapatikana na shughuli ya ujenzi inaendelea na katika bajeti hii ya mwaka 2022/2023 Shilingi Bilioni 1.8 zimetengwa kwa ajili hiyo.

Mheshimiwa Spika, masuala mbalimbali yanayohusiana na masuala ya Kamati ya UKIMWI yalisemwa hapa na Kamati na yaliwasilishwa na Mwenyekiti wake Mheshimiwa Toufiq kama ambavyo Naibu Waziri Ummy Nderiananga amejaribu kuelezea na nimpongeze sana kwa majibu mazuri, hili ni jembe langu nalitegemea sana, msimuone mkimya lakini ni mashine kubwa sana hiyo, mimi ninamuita chawa wangu wa nguvu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Naibu Waziri Nderiananga amejaribu kueleza vizuri niongeze kusema tu kwamba tutajitahidi sana kufanya mapitio ya Mkakati wa Nne wa Kitaifa katika kuhakikisha kwamba mapato ya mfuko huu wa UKIMWI yanakuwa ya kutabirika, kwa hiyo, tutajitahidi sana.

Mheshimiwa Spika, katika kufanya hivyo tutaendea pia na Serikali itaendelea kutoa fedha kama ilivyoahidiwa ile Shilingi Bilioni Moja ambapo mwezi Aprili itatolewa hiyo fedha lakini pia bajeti iliyotengwa kwa ajili ya magonjwa yasiyoambukiza ya Shilingi Bilioni 10.9 ndiyo fedha iliyotengwa katika bajeti ya mwaka 2022/2023 ambayo ni sawa na ongezeko la asilimia 83, hii ni hatua kubwa ambayo itatusaidia.

Mheshimiwa Spika, eneo jingine ni eneo la matumizi udhibiti wa madawa ya kulevya. Baada ya mafanikio makubwa yaliyofanywa na taasisi hii inayozuia na kudhibiti madawa ya kulevya hasa madawa ya viwandani, kimbilio kubwa la watumiaji wa madawa ya kulevya hapa nchini limeenda zaidi kwenye matumizi ya madawa yanayolimwa hapa nchini kama bangi. Hali hii ya matumizi ya bangi hapa nchini kwa kweli inatishia amani na mimi nafikiri ipo haja kila mmoja akatimiza wajibu wake.

Mheshimiwa Spika, namna ambavyo tunalichukulia jambo hili na namna ambavyo hali ilivyo huko mtaani bangi inaonekana kama ni sigara ya kawaida au ni kama ni kitu cha kawaida, wote hapa ndani wengi ni wazazi na tuna watoto wetu na jambo hili tunalijua hata kwa kuangalia ama ni kwa jirani yako ama mahala popote mnapopita katika vijiji vyetu na mitaa yetu, hali si nzuri.

Mheshimiwa Spika, ninatoa rai sisi kama viongozi pamoja na kushirikiana na taasisi iliyopewa jukumu hilo lakini viongozi wa dini, taasisi sizizo za Serikali tushirikiane katika kukomesha matumizi ya madawa ya kulevya, sio ajabu kwa kweli kwa sasa ukajikuta pengine matumizi ya madawa hayo yanafanywa pengine hata na watu wenye nafasi kubwa. Hali hii ikiendelea tutakuwa na Taifa gani kesho.

Mheshimiwa Spika, hii nimeamua leo kuzima ukimya kwa sababu kwa kiasi fulani nanaifahamu hali hii, hali sio nzuri. Nitoe rai kwa wadau wote na hasa sisi viongozi kuhakikisha kwamba tunalizungumza jambo hili hadharani. Imekuwa kama ni fashion na hasa, sasa unakuta matumizi haya yanafanywa na watoto wa kike zaidi kuliko hata watoto wa kiume, hali ni mbaya sana.

Mheshimiwa Spika, niliona niliseme hili na hili haliwezi kupelekewa lawama kwa mtu mmoja kwanza kuna mafanikio makubwa ya kudhibiti ambayo yamefanywa na taasisi yetu, lakini wamekimbilia kwenye haya yanayolimwa ambayo yanapatikana ndani ya nchi na kwa hivyo tushirikiane katika kuhakikisha kwamba tunapelekea elimu ya madhara yanayotokana na madawa ya kulevya.

Mheshimiwa Spika, ukiwa na kijana wako anayevuta bangi leo ujue baada ya miaka 10 mpaka 15 huna mtu wa maana tena. Kwa hiyo, madhara haya ni madhara kwa familia lakini kwa madhara kwa Taifa pia. Nilidhani niseme haya kwa sababu hatuna namna na zaidi ya kusema na kuomba ushirikiano kwa wadau mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, tarehe 23 na tarehe 24 Machi nilikwenda Geneva kwenye mkutano wa Umoja wa Mataifa wa Haki za Binadamu, nilipokuwa kule kabla ya mkutano na hata baada ya mkutano moja ya kati ya mambo niliyokuwa nakutana nayo na wadau wengi walikuwa katika ule mkutano ni namna walivyo na tamaa ya kufika Tanzania lakini kuona Tanzania inayoongozwa na Rais Mwanamke. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata maelezo yangu ndani ya Baraza lile la Haki za Binadamu kila Mjumbe aliyesimama kuchangia juu ya Tanzania alikuwa anasifia juu ya hatua zilizochukuliwa na Rais Samia Suluhu Hassan katika masuala ya kulinda haki za binadamu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka nikuhakikishie huko nje tunavyoonekana siyo kama tunavyojifikiria, heshima yetu imekuwa kubwa. Nami nataka niseme pengine kuongozwa na mwanamke kuna baraka zake kwa sababu mimi siyo mara ya kwanza kusafiri na kuwakilisha nchi yangu kwenye taasisi za Kimataifa, tulikuwa tukipata taabu kidogo kuelezea baadhi ya mambo lakini sasa unakuta mtu anakuelezea yeye mazuri yaliyopo Tanzania.

Mheshimiwa Spika, ninataka nisema kwamba Rais wetu Samia Suluhu Hassan ametupa unafuu na wepesi katika kuilezea Tanzania, pia amekuwa na bahati katika kuifanya Tanzania iwe branded kama ni Taifa la watu wastaarabu, Taifa linaloendelea na ndiyo maana hata taasisi nyingine kama Taasisi ya Africa Development Bank ambayo imetoa nishani kwake, tuzo kwa Rais wetu kwa sababu ya kusimamia ujenzi wa miundombinu, hii ni zawadi na tuzo kwa Taifa zima, Rais anapewa kama nembo tu, lakini tunasifiwa kwa sababu ya mafanikio makubwa ambayo Serikali ya Chama cha Mapinduzi imefanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nitoe rai kwa Waheshimiwa Wabunge pamoja na changamoto tunazozipata na tunazozipitia katika kipindi hiki cha majanga mbalimbali ya dunia, ambayo Tanzania hatupo peke yetu tusivunje umoja wetu, tusivunje mshikamano wetu, tuendelee kushirikiana, tuendelee kupendana na kuhakikisha kwamba zile changamoto tunajadiliana na kukubaliana pamoja ili tuweze kusonga mbele kwa mafanikio makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema maneno haya, nimalizie kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu nimuahidi Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba nitatoa ushirikiano na kufanyakazi kumsaidia na kuanzia kwa wakati huu ambao ninasimama hapa ninaanza na hili la kuunga mkono hoja yako Mheshimiwa Waziri Mkuu, na ninaamini Waheshimiwa Wabunge wote watakuunga mkono Mheshimiwa Waziri Mkuu, hongera sana kwa hotuba nzuri uliyoitoa.

Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)