Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nimpongeze Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya.

Mheshimiwa Spika, pia nimpongeze Waziri Mkuu wetu kwa hotuba yake nzuri yenye matumaini makubwa kwa Watanzania na pia niishukuru Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa kutupa pesa nyingi za miradi mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, katika jimbo la Lushoto lina changamoto kama ifuatavyo; kwanza kuna changamoto ya vituo vitatu vya afya ambavyo ni Kata ya Gare, Kata ya Kwai na Kata ya Makanya. Kata zote hizi wananchi wameshaanza kujenga kwa kutumia nguvu zao wenyewe, kwa hiyo wanasubiri tu Serikali nayo iingize nguvu zake kwa kuwapa pesa kama vituo vingine hapa nchini vilivyopata pesa. Takribani ni miaka sita sasa vituo hivi havijapewa pesa yoyote, hivyo basi niiombe Serikali katika kipindi hiki cha bajeti Serikali itenge fedha za kumalizia vituo hivi ili kuunga mkono juhudi za wananchi wetu na kama unavyojua ni ahadi tulizowaahidi kwenye kampeni zetu.

Mheshimiwa Spika, pili ni changamoto ya maji; katika Jimbo la Lushoto lina kata 15 kati ya kata hizo zenye changamoto ya maji ni kama ifuatavyo; Kata ya Gare yote, Kata ya Kwai hasa Kijiji cha Kwemakame, Kata ya Makanya yote, Kata ya Kwekanga yote, Kata ya Kilole yote, Kata ya Ubiri yote, Kata ya Malibwi yote na Kata ya Migambo yote.

Mheshimiwa Spika, kama inavyofahamika ya kuwa barabara nazo ndiyo zenye kuchangia pato la Taifa, lakini barabara nyingi za vijijini zina hali mbaya, pamoja ya kwamba TARURA wanajitahidi sana, lakini bajeti yao ni ndogo, ushauri wangu Serikali iipatie TARURA pesa za kutosha ili ikatatue matatizo ya barabara hasa katika Jimbo la Lushoto kuna changamoto ya barabara zifuatazo; Dochi - Ngulwi hadi Mombo; Mbwei hadi Mavului; Kibao cha Mazumba - Ntambwe hadi Ngaloi; Kizara - Ngulu hadi Kwemashai – Kwelugogo; Mmanyai hadi Kwezinga na Kwekanga hadi Mlola.

Mheshimiwa Spika, tunaishukuru Serikali yetu tukufu kwa kusambaza umeme katika kila Kijiji pamoja ya kwamba kuna changamoto ya mkandarasi kutoendeleza mradi, kwa maana mradi umesimama, sambamba na hayo katika Jimbo la Lushoto mpaka sasa kuna vijiji zaidi ya 15 na vitongoji ambavyo vimepitiwa na umeme 26 havijapata umeme mpaka leo, na kusababisha kero kubwa sana kwa wananchi. Kwa hiyo niiombe Serikali katika kipindi hiki cha bajeti, Serikali itenge pesa ili vijiji hivyo pamoja na vitongoji vyake viweze kupata umeme.

Mheshimiwa Spika, kuna maboma mengi ya maabara yaliyojengwa kwa nguvu za wananchi lakini mpaka sasa maboma yale yanaanguka na katika Jimbo la Lushoto kuna maboma ya maabara zaidi ya 26 bado hayajaendelezwa. Niiombe Serikali itenge pesa za kutosha ili kwenda kumalizia maboma haya ya maabara yaliyoko nchi nzima ambayo yametumia nguvu za wananchi. Sambamba na hayo Serikali isisahau kujenga nyumba za walimu ili kuwapunguzia kuishi katika nyumba zisizo bora na hatarishi pamoja na kuongeza watumishi wa kada zote.

Mheshimiwa Spika, kama inavyofahamika kuwa Wilaya ya Lushoto ni ya wakulima wa matunda, lakini mazao haya hayajapewa ruzuku za pembejeo wakati ni mazao ambayo yanaingiza pesa katika Halmahauri zetu, niiombe Serikali iangalie upya ili kuwapatia pembejeo wakulima hawa, sambamba na hayo Lushoto inazalisha kahawa lakini zao hili linakufa kwa sababu wakulima hawajawahi kupewa pembejeo pamoja miche bora. Niiombe Serikali iende Wilayani Lushoto ikafufue zao hili kwa ajili ya kuongeza pato la Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, mwisho naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.