Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Amb. Dr. Bashiru Ally Kakurwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. BALOZI DKT. BASHIRU A. KAKURWA: Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba yake iliyogusa maeneo yote muhimu kuhusu mwelekeo wa maendeleo ya nchi yetu kisiasa, kiuchumi, kijamii na kiutamaduni. Kwa ufupi, utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM, kama inavyooneshwa katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, unaendelea vizuri sana ingawa kumezuka vikwazo ambavyo havikutarajiwa hususan mlipuko wa virusi vya corona, uhaba wa mvua na vita huko Ulaya Mashariki.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu utajikita kwenye eneo la hali ya uchumi nchini. Kuhusu hali ya uchumi, naishauri Serikali kuwalinda na kuwawezesha wazalishaji wadogo hasa katika sekta za viwanda, kilimo, mifugo na uvuvi. Ulinzi wa kisera na kisheria kwa wazalishaji wadogo ujikite zaidi kwenye maeneo ya ulinzi wa masoko dhidi ya walanguzi na wanyonyaji, ulinzi wa kazi za ubunifu na teknolojia na ulinzi wa rasilimali za ardhi na ikolojia zinazotumiwa na wazalishaji wadogo.

Aidha, wazalishaji wadogo wanahitaji pia kuwezeshwa na Serikali hasa kwenye masuala ya upatikanaji wa mitaji ya gharama nafuu, utafiti na mafunzo, upatikanaji wa pembejeo na ujenzi wa miundombinu ya uhifadhi wa mazao, usafirishaji, nishati na umwagiliaji.

Mheshimiwa Spika, hali ya kiuchumi kwa wazalisaji wadogo inaweza kudorora zaidi pengine kwa muda mrefu kutokana na athari za UVIKO-19, mabadiliko ya hali ya hewa na mfumuko wa bei ya mafuta duniani. Kwa muktadha huu, Serikali inatakiwa kufanya tathmini ya haraka ili kuweza kuchukua hatua za muda mfupi na mrefu za kulinda na kuwezesha sekta ya wazalishaji wadogo kulingana na mazingira yaliyopo sasa. Kwa kuwa sekta ya wazalishaji wadogo ndiyo mhimili wa uchumi wa nchi yetu hasa katika nyanja za ajira, usalama wa chakula, kodi na tozo na kwa kuwa kuna changamoto mpya zilizozuka ghafla katika sekta hii, ipo haja kwa Serikali kuchukua hatua za haraka kuilinda na kuiwezesha sekta ya wazalishaji wadogo kwa maslahi ya taifa.

Mheshimiwa Spika, kwa mchango huu naomba kuunga mkono hoja.