Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Shamsi Vuai Nahodha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. SHAMSI VUAI NAHODHA: Mheshimiwa Spika, naomba niseme mambo matatu.

Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan anaendelea kuiongoza nchi yetu kwa hekima na busara ya hali ya juu sana, hivi karibuni Rais Samia aliamua fedha za mkopo wa UVIKO-19 zijadiliwe na kupangiwa matumizi yake katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, jambo hili limetupa sisi kama Wabunge heshima na hadhi tunayostahili, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais, vilevile Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ameonesha dhamira ya dhati ya kutekeleza kwa kitendo miradi ambayo iliasisiwa na mtangulizi wake marehemu Mheshimiwa John Pombe Magufuli. Mradi wa bwawa la umeme la Mwalimu Nyerere, Mradi wa Reli ya Kisasa, na ujenzi wa daraja la Busisi unaendelea kupatiwa fedha na inatekelezwa vizuri sana.

Mheshimiwa Spika, hali kadhalika Mheshimiwa Rais anaendelea kuzungumza na Viongozi wa Vyama vya Siasa ili kuzungumzia mustakabali wa Taifa letu na kuzungumzia maendeleo ya demokrasia, jambo hili ni muhimu sana katika kuleta umoja, maelewano na amani katika Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hapana shaka tunahitaji sana maridhiano na kama Biblia Takatifu inavyosema ni ‘heri wapatanishi maana hao wataitwa wana wa Mungu’. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili mwaka 1962 aliyekuwa Waziri Mkuu wa Singapore Lee Kuan Yew aliwahi kutembelea nchi ya Nigeria na Ghana na katika kitabu chake cha kutoka nchi maskini kwenda nchi tajiri alisema, aliona mambo ya kushangaza Nigeria na Ghana na aliporudi nyumbani kwao Singapore alifanya mkutano na Waandishi wa Habari na akasema maneno haya, ningepewa nafasi ya kuzishauri nchi za Bara la Afrika nini kifanye ili watokomeze umaskini basi ningewashauri mambo mawili: -

Kwanza, waimarishe kilimo kwa sababu wanazo fursa kubwa sana za kilimo, wanayo mito, wanayo maziwa, wanayo ardhi, wanayo hali ya hewa nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili, ningewashauri waimarishe utalii kwa sababu wanavyo vivutio vingi vya utalii. Ninachokiona sasa kinafanywa na Rais Samia Suluhu Hassan hapana shaka inadhihirisha anatekeleza mawazo na fikra hiyo iliyoelezwa na Ndugu Lee Kuan Yew. Hivi karibuni Serikali yetu Tukufu imeonesha dhamira ya dhati ya kutaka kuwekeza kwenye Kilimo na hasa kilimo cha umwagiliaji. Jambo hili ni jambo ambalo linanipa faraja sana kwa sababu nimekuwepo kwenye Bunge hili kwa takribani vipindi vitatu, zimekuwepo kelele za Waheshimiwa Wabunge kuitaka Serikali yetu Tukufu iwekeze kiasi cha kutosha katika kilimo cha umwagiliaji, kile kilio ambacho hakijasikilizwa ipasavyo na kusema kweli jambo hili limekuja katika wakati muafaka sana.

Mheshimiwa Spika, hivi sasa nchi yetu ina eneo lipatalo takribani hekta Milioni 22 linalofaa kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji maji, lakini kwa bahati mbaya sana mpaka sasa tumewekeza chini ya eneo la ekari 600,000 nadhani hazifiki 600,000. Kwa hiyo, ninaipongeza sana Serikali kwa mawazo hayo.

Mheshimiwa Spika, pamoja na wazo hilo la kuwekeza sana kwenye kilimo cha Umwagiliaji, ipo haya ya kuwekeza kwenye vyuo vya utafiti wa kilimo ili tuwapatie vijana wetu maarifa na ujuzi, katika masuala ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ambalo Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ameonesha dhamira na nia ya kutekeleza wazo la Lee Kuan Yew ni hili hivi karibuni alishiriki katika kipindi kiitwacho Royal Tour, kipindi chenye lengo la kuitangaza nchi yetu nje ya nchi, kwa ajili ya kuvutia watalii, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa hatua hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la tatu, mwaka 1978 aliyekuwa kiongozi wa China Ndugu Deng Xiaoping alizungumza na Rais Jimmy Carter wa Marekani na kumuomba aipatie nchi yake nafasi 5,000 za masomo kwa ajili ya vijana wake. Jimmy Carter alilikubali wazo hilo, akamwambia nimekubali wazo hilo lakini badala ya kukupatia nafasi 5,000 nitakupatia nafasi 100,000 na kuanzia hapo nchi ya China imeendelea kupeleka vijana wao nchini Marekani ili kuwapatia vijana wao ujuzi na maarifa.

Mheshimiwa Spika, China hii inayoonekana hivi leo ni matokeo ya uamuzi huo, ninaiomba Serikali yetu Tukufu tufanye kila linalowezekana tuwekeze katika sekta ya elimu hasa kama tunataka kuharakisha maendeleo ya Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, Mwanafalsafa mmoja wa zamani wa China aliwahi kusema, ukitaka maendeleo ya muda mfupi panda maua, na ukitaka maendeleo ya miaka 10 panda miti, lakini ukitaka maendeleo ya karne moja somesha watu wako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naishauri Serikali yetu Tukufu ifanye kila linalowezekana aghalau igharamie kuwapeleka vijana masomoni wapatao 1,000 vijana ambao walifanya vizuri sana katika masomo yao, napendekeza sisi hatuna uwezo wa kupeleka vijana wetu wengi Marekani lakini badala yake angalau tunaweza kuwapeleka vijana wetu Korea, China, India, mahali ambapo gharama za masomo zipo chini kidogo ukilinganisha na Marekani na nchi nyingine za Ulaya.

Mheshimiwa Spika, nalisema hili kwa sababu moja ya matatizo makubwa sana yanayolikabili BARA la Afrika ni ukosefu wa ujuzi na maarifa na kama Biblia Takatifu inavyosema watu wangu wanaangamia kwa kukosa maarifa. Nakushukuru sana. (Makofi)