Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Fakharia Shomar Khamis

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. FAKHARIA S. KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza sina budi kumshukuru Mheshimiwa Waziri kwa hotuba yake nzuri aliyoitoa na imetoa mwelekeo kwa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nasema mnyonge mnyongeni, lakini haki yake mpeni. Nimezungumza kwa kusema fumbo hilo; tunalizungumzia Jeshi. Jeshi wajibu wake ni kwenda Zanzibar na kuwepo Bara. Sasa kupelekwa Jeshi Zanzibar imekuwa hoja kubwa hapa ndani, kwa nini Jeshi limekwenda Zanzibar?
Mheshimiwa Waziri ukurasa wake wa 20 alizungumza hivi, nanukuu: “Kukamatwa kwa mabomu ya kutengenezwa kwa mkono katika maeneo mbalimbali ya Zanzibar.” Sasa kwanini majeshi yasiende? Atakayeyategua mabomu haya ni nani kama siyo Jeshi? Sasa haya mabomu kayatengeneza nani? Wakasema ni wananchi wa Zanzibar. Sasa ikiwa ni kweli jambo hilo limefanyika Zanzibar, wa kufanya shughuli hiyo ni majeshi; wa kuangalia ulinzi huo ni majeshi na mabomu yamelipuliwa Zanzibar. Tatizo liko wapi? Anayetaka kusema na aseme tu ili afurahishe roho yake na maamuzi yake, lakini ukweli ndiyo huo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kuzungumzia kuhusu mgao wa nafasi za ajira Zanzibar. Nakubali wanajeshi wanaajiriwa Zanzibar, lakini utaratibu unaotumiwa Mheshimiwa Waziri angalieni. Mnapeleka nafasi katika Mikoa, watu wanatafutwa katika mikoa, wanaajiriwa. Kwa nini msiende JKU kama mnavyokwenda JKT? Kwanza kule mtapata vijana tayari wameshapata elimu ya jeshi, wakakamavu, wameshajua nini wanakwenda kutenda; lakini kuchukua Mkoani, hamumjui mtu yupo vipi, lakini kwa sababu vipi aajiriwe! Nafikiri hilo mliangalie tena na mlipange tena. Bora vijana wetu wakimaliza, waende JKU wapate elimu ya ukakamavu na inakuwa rahisi kwenu kujua wapo vipi, afya yake ni vipi na uwezo wake uko vipi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nitakuja katika ukarabati wa ujenzi wa majengo ya jeshi Zanzibar. Kambi za Zanzibar zipo kwenye hali mbaya. Ukiangalia Mtoni, Mwanyanya, Mazizini na nyingine zote hazipo kwenye hali nzuri na sielewi toka zilipojengwa lini zimekarabatiwa. Nimeona katika kitabu chako ukurasa wa 37 umeelezea kwamba kuna nyumba kama 4,744; siyo mbaya hiyo kazi mtakayoifanya; na mmesema tayari kwa Pemba. Kama zipo nyumba 320 siyo mbaya; lakini kwa Unguja hali ndiyo mbaya. Kwa Unguja majeshi yetu pale ndiyo Zanzibar City. Sasa tunataka kama mlivyojenga nyumba 320 na Zanzibar tujue nyumba zetu mtazijenga lini? (Makofi)
Mheshimiwa Waziri, malipo ya wanajeshi wastaafu yanakuwa yana matatizo; matatizo yake ni nini? Inabidi lazima mwanajeshi aende Bara kutoka Zanzibar kufuatilia. Kwani Zanzibar hamwezi kuweka kituo kukawa na kituo kama Bara? Mwanajeshi kastaafu Zanzibar, anakwenda pale anahudumiwa, anapata malipo yake Zanzibar baada ya kuondoka. Maana akifika Bara kwanza humjui mtu, wala humwelewi mtu, hujui unaanzia wapi! Wakati mwingine huyo mwanajeshi hajapata nafasi hata ya kwenda huko. Mwenyewe yupo Zanzibar tu! Sasa mnampeleka Bara akafuate kiinua mgongo, akahangaike! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Waziri, asaidie Wizara kama inaweza kujigawa na Zanzibar wakawepo wafanyakazi na wakaweza kufanya kazi hiyo vizuri na kwa wepesi bila matatizo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho ni kuhusu uvamizi wa ujenzi wa nyumba karibu na kambi za Zanzibar. Kambi za Zanzibar zimevamiwa, zipo katikati ya mji. Kambi hizo kwa kweli ukiangalia Mtoni, Mazizini, Mwanyanya na nyingine kadhalika, pale linalofanywa ndani ya kambi wananchi wa pale wanajua, kinachotokea wananchi wa pale wanajua na inatakiwa ndani ya kambi kuwe kuna siri. Huwezi kuyajua mambo ya kambini.
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine inawezekana ikatokea madhara itakuwa rahisi kwa wale wananchi kupigwa. Itabidi wananchi wanaokaa karibu na kambi wapate elimu wajue jinsi ya kujihami, maana ukishakaa kambini na wewe ni sawa sawa na mwanajeshi, litakalotokea na wewe umo. Sasa mngechukua wakati wenu mkatoa elimu kwa watu waliokuwepo pale. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hayo, naunga mkono hoja.