Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Kilumbe Shabani Ng'enda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kigoma Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweke mchango wangu kwenye mpango huu wa maendeleo wa mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama uelewa wangu uko pamoja na wenzangu ni kwamba, kadiri tunavyojadili mpango huu tunajaribu kuona vipaumbele katika mpango wetu vitakavyosababishia kuweka sura ya bajeti yetu inayokuja ya 2023/2024.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huko nyuma, miaka mitano iliyopita, ukiangalia maendeleo ya Taifa letu yalijielekeza katika kuwekeza nguvu kubwa kwenye viwanda na suala zima la madini. Na sasa ukiangalia mwelekeo tulionao sasa na hasa ukiangalia bajeti tuliyoipitisha ni kwamba muelekeo mkubwa sasa tumejielekeza katika kilimo, na hili ni jambo jema sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na niseme, hata tulipokuwa tumeamua kujielekeza katika viwanda na kuweka nguvu kubwa katika viwanda, viwanda tulivyovikusudia si vingi vilivyowekwa. Viwanda tulivyovikusudia ni viwanda vya kuchakata mazao ya wakulima na wafugaji ili kuyaongezea thamani ili tuweze kuwatoa watu wetu katika umasikini. Hata hivyo viwanda vilivyoibuka vingi vikawa ni vya kutengeneza nondo, saruji, kutengeneza malumalu, sijui kutengeneza nini, mambo chungu nzima ambayo kwa kweli, haya add value ya mazao ya wakulima, wafugaji na wavuvi. Kwa hiyo, ulikuja msemo wa wenzetu ambao wako nje, yaani maana ya nje ya Serikali, wana-challenge wakasema tumejielekeza katika maendeleo ya vitu kuliko maendeleo ya watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, msemo huu ulichukua nafasi kubwa sana ya mijadala, lakini tulikuwa right. Maendeleo ya vitu waliyokuawa wanayasema, kwamba tulijielekeza katika kutengeneza barabara, kujenga shule, hospitali na viwanja vya ndege. Tulifanya hivi kwa sababu, hata kama ukitaka kuwasaidia watu kuwainua kiuchumi kama miundombinu si rafiki basi hao wakulima wako hawawezi kupata soko zuri la mazao, hao watu wako kama hawana hospitali hawawezi kuwa na afya nzuri na kuweza kumudu uhindani kwenye uchumi, kwa hiyo tulikuwa tuko right.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nafikiri sasa ni lazima tujielekeze sasa katika maendeleo ya watu. Kazi tuliyoichukua kwa kipindi kirefu, ya miundombinu, shule, sijui hospitali na nini, kwa kweli naweza kusema tumepiga hatua kubwa sana tukijilinganisha na nchi nyingine za Afrika, hatua ni kubwa sana. Nchi zote za jirani zetu hapa hakuna nchi inayoweza ikajilinganisha na sisi katika miundombinu. Tumekopa, tumefanyaje tukasema tutengeneze mazingira yatakayowafanya watu wetu, wakulima wetu waweze kufikisha mazao sokoni, watu wetu waweze kufika mahali kupata huduma za afya nzuri, waweze kupata elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa huko tunakotaka kwenda kusaidia maendeleo ya watu ni kupi? Ndio kitu ambacho nataka nikizungumzie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja. Tunataka wakulima wetu wapate bei nzuri za mazao ili kipato chao kiongezeke maendeleo ya watu yainuke. Kwa hiyo, mpango huu lazima utuelekeze katika namna gani tutawatoa wananchi katika kuwahimiza limeni, baada ya kulima halafu kufika mahali mazao yanaoza hayapati soko. Lazima mpango huu utueleze tunafanyaje? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vilevile mpango huu utueleze namna gani tunawasaidia wasomi wetu ambao wamesoma, hawajapata ajira lakini wanataka kuchangia katika uchumi wa Taifa, mpango huu ni lazima utueleze. Na huu katika kutueleza ni kwamba, watu wengi wanayo mipango mizuri ya kukuza uchumi na kuendeleza Taifa lao lakini hawana mitaji. Wakienda benki si rafiki katika kutoa mitaji kwa watu wanaoanza. Kwa hiyo ni lazima tufike mahali tuseme ni namna gani tunaelekeza benki zetu na vyombo vya fedha kuwezesha watu wetu ambao wana elimu, wana ujuzi, wana maarifa, lakini hawana mitaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kuhusu mikopo nafuu. Tumeweka mikopo ya vijana wanawake na walemavu asilimia 10 ya Halmashauri. Ni kiasi kidogo sana. Leo tunataka tuone kwenye bajeti yetu itakayokuja tuweke fedha kwa ajili ya kuongeza mfuko wa wanawake na vijana, tusitegemee asilimia 10 za Halmashauri tu, haziwezi kututoa mahali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimeona Wizara ya Mifugo na Uvuvi wamekuja na mpango mzuri sana wa kusaidia kuinua watu na hasa kwenye uvuvi. Wamekuja na mikopo isiyokuwa na riba ya maboti za uvuvi, mashine, vifaa vya kuhifadhia samaki na rada. Mimi naomba sana tunapokwensa kwenye bajeti inayokuja hebu tuweke fedha za kutosha hapa, uvuvi unaweza ukasaidia kuongeza Pato la Taifa kwa kiasi kikubwa sana. Tunayo maziwa makubwa kama ziwa letu ya Tanganyika pale lakini imefika mahali ambapo uvuvi hauchangii pato la Taifa kwa kiasi kikubwa, ni kwa sababu hatujawawezesha na hawawezi kwenda benki. Hata hivyo fedha hizi zilizotengwa na Serikali kwa ajili ya boti na vifaa hivyo ni chache sana, tunaomba kwenye bajeti hii inayokuja tutazame namna ya kuongeza fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu wafanyabiashara. Wafanyabiashara nao lazima tuwasaidie; na katika kuwasaidia ni kwamba, hivi kweli jamani bado tunafikiri ni muhimu kuwa na VAT ya asilimia 18? Mbona huu ni mzigo mkubwa sana? Hebu tuweke VAT kidogo iweze kulipika sana. vilevile mfumo wa VAT, kama ni watu wote wafanyabiashara wawe VAT registered kwa sababu gani; wale waliosajiliwa kule kwenye VAT wanaumia kuliko wale ambao hawakusajiliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi nilikuwa nashauri… aah, muda umeisha?

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Malizia sentensi yako.

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ambalo ningemalizia katika hilo ni kwamba, Halmashauri zetu zimeonesha, kwa mujibu wa Taarifa ya CAG zimekusanya vizuri fedha asilimia 94 kuliko hata Serikali Kuu kupitia TRA ambapo kwenye malengo wenyewe walifikia asilimia 86.6. Katika hali hii tuwaongezee nguvu, na katika kuwaongezea nguvu bajeti inayokuja Madiwani na Wenyeviti wa Mitaa tuwaongezee fedha wapate namna ya kusimamia vizuri Halmashauri zetu. Ahsante sana. (Makofi)