Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Masache Njelu Kasaka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lupa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia Mpango huu wa Bajeti wa Mwaka ujao wa Fedha kama ulivyowasilishwa na Waziri wa Fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye taarifa ambayo imeletwa hapa ya mpango tumeona ukuaji wa uchumi katika kipindi cha Januari mpaka Juni 2022. Tumeona uchumi wetu umekua kwa asilimia 5.2 katika nusu mwaka hii na kuna sekta ambazo zimeongoza katika ukuwaji huu ni sekta ya maji safi na maji taka ambayo imekua kwa asiliamia 10.7, bima asilimia 10, umeme asilimia 8.5, madini na mawe asilimia 7.1 na nyinginezo. Ukuaji huu kwa robo hii umekwenda vizuri lakini ukuaji huu hauendani sambamba na mfumuko wa bei ulivyo. Tunaona kipindi cha Agosti, 2022 mfumuko wa bei kwenye upande wa vyakula na vinywaji ilikuwa ni asilimia 7.8 ambapo hii ni ongezeko kubwa, ambapo kipindi cha Agosti mwaka uliopita mfumuko wa bei ulikuwa 3.6 kwa hiyo, mfumuko wa bei umekwenda mara mbili zaidi ya hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachotaka kusema ni nini? Nikwamba uchumi wetu unakua lakini auendi sambamba na mfumuko wa bei, kitu ambacho ni hatarishi sana kwenye uchumu wa nchi yetu. Nikiangalia kwenye mpango hapa hakuna namna yeyote ile yakuweza kukabili mfumuko huu wa bei. Tunaacha tu nature iweze ku-take place kitu ambacho ni kibaya, niombe sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha, uangalie wewe pamoja na Wachumi wa kwako ambao amekuzunguka, namna ambavyo tuwe na mipango endelevu ya kuhakikisha kwamba mfumuko wa bei huu tunaenda kwenda kuutatua kwakuwa na mipango ya muda mfupi na mipango ya muda mrefu, bila hivyo tutakuwa hatuwezi kufika kule tunakotaka kwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye mpango huu wa Bajeti, tumeona kwenye msimu wa 2021/2022 uzalishaji wa chakula ulikuwa tani milioni 17.4 na kwenye mpango huu wa bajeti wamekadiria mahitaji ya chakula ya kwetu sisi hapa ni tani milioni 15. Hata hivyo hawajaonesha namna ambavyo uzalishaji wa kwetu sisi utakavyokuwa. Sasa tuna mipango mingi ambayo inakwenda, tunawekeza kwenye kilimo lakini hatuna mpango wa kuonesha kwamba uwekezaji wetu huu utazalishia kiasi gani? Kitu ambacho kwenye uendeshaji wa uchumi wa kwetu tunakuwa tunakwenda kwa sababu tu tulitakiwa twende. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishauri tu Wizara fedha, pamoja na Wizara ya Kilimo, muweze kukaa muwe na mipango kuonyesha kwamba kiasi ambacho tunakwenda kuwekeza kwenye upande wa kilimo tunategemea uzalishaji wetu utakua kiasi hiki na matumizi yetu yatakuwa kiasi hiki na hii ziada itatuwezesha sasa kuweza kuuza nje, kama mnavyojua, fedha nyingi ambazo tumeweza kuwekeza kwenye bajeti ambayo imepita tunaimani utekelezaji kwenye kilimo ukienda vizuri uzalishaji utakua zaidi na ukikua zaidi hii ni fursa kwetu kwa hizi bidhaa zetu za mazao kwenda kuuza nje ya nchi na tukaweza kupata fedha za kutosha na badae uchumi wetu ukakua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishauri tukifanye kilimo chetu hiki kuwa cha kibiashara. Tumekuwa tunakizungumza kwa nadharia kwamba tunawekeza kwenye kilimo lakini tunaenda kufanya kilimo hiki kwa mazao ya kuweza kujikimu. Tutoke hapa tulipo twende kwenye mazao ya kibiashara ili haya tunayoyasema yaweza kwenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijielekeze pia kwenye upande wa Miundombinu. Naona hapa kwenye bajeti na kwenye mpango huu wa bajeti kuna mambo makubwa yameelekezwa kwenye miundombinu. Nichukulie mfano kwenye SGR tunajenga hapa, tunaishukuru Serikali ya Awamu ya Sita inaendelea kujenga na mambo yanaendelea vizuri lakini bado hatujawa na mpango endelevu kuweza kuhakikisha kwamba reli hii itaweza kuwa na tija kwetu sisi. Leo tunajenga reli hii kwenda Mwanza, kule Mwanza hakuna mzigo wa kututoa Dar es Salaam kutupeleka Mwanza, sasa hivi hapa ili reli iweze kutulipa, iweze kulipa tunapoweza kusafirisha mizigo mingi na ya kutosha na mizigo pekekee ambayo inaweza kututosheleza na uchumi wetu kuweza kukua ni kututoa Dar es salaam kwenda Kigoma na baadae DRC ndiyo inachukua mzigo wa asilimia Sabini ya unaopita Bandari ya Dar es salaam lakini sisi tumeelekeza reli yetu kwenda Mwanza kusafirisaha abiria badala ya kupeleka Kigoma ambapo tutapeleka kule mizigo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashauri Serikali iweze kupitia upya ione namna nzuri zaidi reli hii sasa tuwekeze nguvu ambayo itapeleka mizigo hii na badae itaweza kutusaidia. Hii ni reli ya kati lakini pia kwenye mpango tuone namna ambavyo tunaweza tukaiboresha reli yetu ya TAZARA. Reli ya TAZARA siyo kuboresha tu miundombinu peke yake. Reli hii tuone namna ambavyo, namna ya uwanzishwaji wake, namna uendeshwaji wake baina ya hizi nchi mbili. Tukiweza kutatua hili ndivyo ambavyo baadae tutaenda kwenye miundombinu na baadae tuone namna ambavyo itaweza kutusaidia. Kuna mizigo mingi inatoka hapa inaenda Zambia, kuna mizigo mingi inatoka Zambia shaba inatoka kule inakuja Dar-es-Salaam leo hii awatumia TAZARA wanatumia barabara, barabara hizo wanazotumia zinaishia kwenda kuharibu barabara zetu kwa malori haya na sisi tunakuwa hatunufaiki wakati reli tunayo na kusudi kubwa la reli lilikuwa kuhakikisha kwamba miundombinu hii inakua vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu muda wenyewe siyo rafiki. Nitakuandikia kwa maandishi ili niweze kuleta mchango wangu. Ahsante sana.