Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Katani Ahmadi Katani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tandahimba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nichukue fursa hii kumshukuru Allah Azza wa Jallah kwa kunipa afya njema, lakini nikushuru wewe pia kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikupongeze kwa kuipeleka Kamati ya Bajeti kule Mtwara hususan walipokwenda kwenye Bandari ya Mtwara. Ukisoma mapendekezo ya Mpango, Kamati ya Bajeti kuna mambo imependekeza kuhusu Bandari ya Mtwara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeweza kuboresha Bandari zetu zote za Mtwara, Dar es Salaam na Tanga kwa zaidi ya bilioni 328 leo kwenye mpango huu ambao unapendekezwa, nimeona Waziri wa Fedha amefanya kazi nzuri sana kwenye Mradi ule wa Liganga na Mchuchuma, lakini wakati tunaweka mpango huu wa Liganga na Mchuchuma tumesahau reli ambayo itasafirisha hayo makaa ya mawe na bidhaa nyingine ambayo reli hii inakwenda Mtwara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inanipa mashaka kama Waziri amesahau au la. Mapendekezo yangu kwenye jambo hili kwa sababu Serikali ina nia njema ya kutanua wigo wa biashara na kutoa fursa, basi wanapoleta mpango sasa tuone reli hii ya kutoka Mtwara Kwenda Mbambabay nayo inakuwepo kwenye mpango wetu huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona pia Kamati ya Bajeti imependekeza vizuri kwenye Mpango hususan kwenye suala la zao la korosho kwenye kuongeza thamani. Leo bei ya korosho ukiitazama haiwezi kuwa na tija kwa mkulima kwa bei ya 1,800, 1,900. Kamati ya Bajeti imependekeza kuongeza thamani. Hata hivyo, wakati imependekeza kuongeza thamani, ni Serikali hii hii iliuza viwanda vya kubangua korosho. Leo tunashauri tena turejeshe viwanda ambavyo ndio mwarobaini wa kuongeza thamani kwenye korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye mkataba wa kuuza viwanda vile ambavyo vimeuzwa zaidi ya viwanda vitano, mkataba ulikuwa wazi, ulikuwa unasema wanunuzi wa viwanda vile wanapaswa kubangua korosho. Matokeo yake vile viwanda havijaenda kubangua korosho hata kipindi kile cha hayati Daktari Magufuli aliposema askari waende wabangue korosho wamekwenda pale Lindi, viwanda vilivyouzwa kwa bei chee hakuna hata malighafi ya viwanda mle ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapendekezo yangu kwa Serikali kwa jambo hili kwa sababu alionunua viwanda wamevunja mikataba. Moja Serikali ichukue vile viwanda, wapitie makubaliano ya Serikali ya kuuza viwanda na hao walionunua waweze kurejesha viwanda mikononi mwa Serikali ili tunaposema tunataka kuiongezea soko korosho, basi tuwe tuna viwanda tayari vya kubangua korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza pia kwenye Wizara hii ya Kilimo, walikuwa na mpango mzuri, tulikuwa na mapendekezo ya kujenga viwanda vikubwa vitano. Walisema wanajenga Pwani, Mtwara, Tunduru, Ruangwa, leo fedha zile wamechukua bilioni 210. Mheshimiwa Bashe anakumbuka vizuri, sasa kwa sababu amerudi kwenye Wizara hii tunataka tuone sasa tunaleta viwanda maeneo yanayolima korosho, hii ndio tija kwa mkulima. Kama juzi wakulima wanaona kwamba mfanyabiashara mmoja anakwenda Marekani kilo moja ya korosho iliyobanguliwa inauzwa kwa dola 40 zaidi ya Sh.90,000 ya kitanzania, maana yake imeongezwa thamani na ni ukweli usiopingika kwamba kama tutakuwa na viwanda vya kubangua korosho leo mkulima wa Mikoa wa Kusini, Lindi Mtwara na Ruvuma hawa watu watakuwa multi- trillionaire.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matajiri wanaozungumzwa wa Tanzania wa kwanza atatokea Mtwara kama tutaboresha viwanda vya kubangua korosho. Ni matarajio yangu kwenye mpango huo Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Waziri wa Kilimo wapo hapa. Wanapokuja sasa kwenye mpango wenyewe tuone mkakati madhubuti wa Serikali unaoelezea namna ya kumsaidia mkulima aidha wa korosho, kahawa kwa sababu bei hizo ukienda Songea kule bei ya kahawa na yenyewe ni kama ya korosho, haieleweki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namna pekee ni kuwekeza kwenye kubangua, kuwekeza kwenye viwanda. Ushauri wangu kwa Serikali, Wizara ya Kilimo na Waziri wa Fedha ambaye ni msikivu, kama aliweza kuiongezea fedha Bajeti ya Wizara ya Kilimo mwaka jana, nadhani bajeti ijayo anaweza akaiongezea mara tatu ili tuone tija kwenye sekta ya kilimo inakaa sawasawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kule kwetu tunalo Bonde la Mto Ruvuma na hapa Mheshimiwa Waziri wa Kilimo nataka anisikilize sana. Ameweka mipango yake vizuri kwenye Sekta ya Umwagiliaji, lakini ametusahau watu ambao tuna bonde lenye floor ya maji wakati wote. Ukija Jimboni kwangu nina Bonde pale Namahonga la Nacha, ukienda Mchichira nina Bonde pale la Ng’apa. Mabonde yale ni mazuri kwa uwekezaji huu wa umwagiliaji unaosema. Nione kwenye mpango sasa na sisi watu wa Mtwara tupo. Kaka yangu Chikota nadhani ana bonde ambalo naye ukitazama ukanda ule unakwenda mpaka Ruvuma. Kuna jambo wanaweza wakalifanya kwenye umwagiliaji na tukazalisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda hata Mtama kuna mabonde pale, wasitusahau watuweke kwenye mpango tuone bajeti ya 2023/2024, sisi watu wa Kusini kwenye Sekta ya Umwagiliaji tupo kwa sababu maji tunayo. Hakuna sababu ya kuona kwamba umwagiliaji unawekaweka tu maeneo ya Tabora huko ambako hakuna maji. Watuletee sisi ambao tuna maji tumsaidie uzalishaji, Taifa lipate vitu vizuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado najikita hapo hapo kwenye sekta ya kilimo. Mheshimiwa Waziri kuna jambo amelifikiria ambalo ni jema sana la kuwasajili wakulima. Jambo hili ukilizungumza na hakuna bajeti ya kufanya jambo hili tutazungumza story miaka 10 na hatutaweza kusajili wakulima. Mheshimiwa Waziri akiwaambia watu wa Bodi wasajili wakulima watamwambia wanaotaka kutumika kule ni Maafisa Kilimo hawana fedha za kuwawezesha kwa ajili ya mafuta ya kwenda mashambani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tandahimba peke yake inao zaidi ya wakulima Laki Moja na kitu, ili uweze kwenda kuwasajili wale inapaswa ufanye kazi mahsusi kabisa ambayo haina tofauti na Sensa. Sasa kwa sasabau umeamua kumsaidia mkulima niombe kwenye Mpango unaokuja nione umeweka package kabisa inayokwenda kufanya kazi ya kusajili wakulima ili unapoteleta mbolea yako ya ruzuku usipigwe mchanga wa macho. Utakuwa na takwimu sahihi utamjua Katani huyo ambaye ana namba ya NIDA, ana cheti cha kuzaliwa kila kitu ambacho umekitaka lakini ukiweke kwenye mpango, ukizungumza nadharia tutarudi tena hapa tunazungumza habari ya kusajili wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapendekezo yangu kwako Waziri wa Kilimo na Waziri wa Fedha upo wekeni bajeti ya fedha tuende tusajili wakulima. Tuwasaidie kwenye mazingira tunapotoa pembejeo za Serikali watu wasiweze kuwarubuni, watu wasiweze kuwaibia na mtaona mnapoweka projections’ kwamba mnataka korosho mzalishe tani Laki Saba, Laki Nane kama mtakuwa mmesajili wakulima, kwakweli mtakuwa hamuwezi kuibiwa pembejeo lakini hata mnapopanga mipango yenu mtakuwa mnapanga mipango ya kulima ambayo mnaijua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Mapendekezo yangu machache yalikuwa ni hayo. (Makofi)