Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kupata na mimi fursa ya kuchangia katika mapendekezo ya mpango wetu huu. Nianze kwa kuwapa pole wananchi wa Mbeya kwa ajali mbaya ya gari ambayo imetokea kwenye Mlima Iwambi mteremko wa kwenda Mbalizi, ambayo imesababisha vifo ikiwemo familia ya Katibu wa BAKWATA wa Mkoa, lakini hayo ni matokeo ya utekelezaji wa shughuli ambao unachelewa. Hilo eneo ilikuwa barabara ipanuliwe lakini mpaka leo haijapanuliwa. Kwa hiyo, tunapojadili hii mipango tuangilie vilevile athari zinazotokea kutokana na kucheleweshwa kwa utekelezaji wa hii mipango. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile niwape pole wananchi wa Kagera na Watanzania kwa ujumla kwa ajali ya Precision Air ambayo imetokea na kupoteza Watanzania wenzetu. Pia ninapenda kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa utekelezaji wa Ilani. Ilani ya Chama cha Mapinduzi imetekelezwa vizuri, maeneo mengi ukiangalia hata miradi ya kimkakati kwa kweli imeibadilisha nchi yetu kwa kiasi kibwa. Naweza kusema hata brand ya Tanzania kwa kweli imebadilika kwa kiasi kikubwa. Hata wageni wanapokuja tumeshuhudia wageni wanatoka nchi mbalimbali hata Wabunge kutoka Mataifa mengine wamekuwa wakisifia wanavyoiona Tanzania inavyobadilika kwa haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo ukiangalia huu mpango wetu kwa kweli mapendekezo ni mazuri lakini yamekaa kinadharia mno. Ukiangalia uhalisia haupo kwa sababu haielezi ya kwamba tutajipima vipi? Dhima ya mpango ni kujenga uchumi shindani na viwanda kwa maendeleo ya watu, hiyo dhima ibebeba vyote hivyo lakini ukianza kuangalia huu mpango huoni sisi ya kwamba je tumeji position vipi kwenye ushindani kwenye Ukanda huu wa East Africa, kwenye ukanda wa SADC na kidunia, na hiyo ndiyo inatakiwa mpango ukae namna hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kama walivyosema wenzangu kuna upungufu mkubwa wa governance structure ya Wizara ya Fedha, ni bora ikarudishwa Tume ya Mipango ili iwe nje ya Wizara ya Fedha iweze ku coordinate Wizara zote, ili mipango ya Wizara zote iweze kupitia sehemu moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia leo sidhani kama kuna coordination ya aina hiyo, inawezekana kama ipo lakini haionekani na bila kuwa na hiyo na bila kurudisha ile BRN (Big Results Now), kwa kweli tutakuwa tunapanga mipango hapa na hakuna anayeifuatilia na hatujui ni nini kinachotokea. Tutampa wakati mgumu sana Mheshimiwa Rais kujua Serikali yake ina perform vipi, hata Chama cha Mapinduzi kurudi kwa wananchi nachi itakuwa ni kazi kubwa mno. Nayasema haya, tumekuwa tukizungumzia monitoring and evaluation kwa muda mrefu iko wapi? Bila kuangalia nini tulichokipanga na tunafanya nini inatuletea changamoto kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia tunazungumzia Deni la Taifa, tunasema Deni la taifa ni himilivu, kwa kiasi kikubwa utazungumza ndiyo kwa kuwaambia watu kwamba Deni la Taifa ni himilivu, kwa sababu hata modes naye kasema ni positive kwa hiyo ametu-evaluate vizuri. Lakini ukiangalia kwenye ripoti hii ya leo ule ukomo wa deni ukilinganisha na mauzo ya nje tumefikia kwenye mstari wa njano tunaenda kwenye mstari mwekundu. Maana yake nini? Maana yake ni nini? Ni kwamba tunakopa lakini uwezo wa kulipa hii mikopo ya kigeni inawezekana ikatushinda, sasa hili siyo jambo zuri kwa nchi yetu! Tulitaka tuone katika huu mpango measures gani umechukua ili ku- address hilo pesa za kigeni zipatikane nyingi ili nchi iweze kuendelea. Hizo fursa zipo lakini kwa sababu hatuna Tume ya Mipango hizo fursa huwezi kuziona. Kwa vile, mtu wa Madini fursa zipo anafanya yeye mwenyewe, mtu wa maliasili anafanya yeye mwenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia hata kwenye kilimo bajeti imeenda nzuri sana lakini je, Wizara ya Kilimo ndiyo itaenda kulima? Hapana ni binafsi! Ile bajeti kubwa ungeiweka benki, watu wakaenda kuchukua mikopo wakajenga mabwawa badala ya Serikali kuanza kufanyakazi ambazo zinatakiwa zifanywe na sekta binafsi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia yote hayo, Mheshimiwa Rais katoa Trilioni Moja zikakopeshe wakulima; Je, zimekwenda? hazijaenda Trilioni Moja! Kama kungekuwa na ubunifu, Je, kuna watu wabunifu hakuna! Ilitakiwa kuwe na watu wabunifu ya kwamba hii Trilioni Moja tuitumie namna gani na siyo ametoa fedha taslimu Hapana! Yeye inakuwa ni window ili watu waweze ku- access zile pesa ziende kwenye sekta ya kilimo tuweze kuzalisha na kilimo kitaibadilisha Tanzania kwa kiasi kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapendekezo yangu kwenye kilimo ni kwamba tungeondoa masoko kwenye Kilimo. Masoko ikiwezekana yakajitegemee tusichanganye uzalishaji na masoko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii bei ya kahawa haiendi vizuri kwa sababu gani, kahawa Tanzania siyo kwamba tunashindana na Brazil Hapana! Bali kahawa ya kwetu tunashindana kwa ajili ya ubora wa kahawa ya Tanzania. Lakini ni nani amekwenda kuuza huo ubora? Hakuna! Kwa hiyo, mtu anaenda sokoni hajui atauza kwa kiasi gani. Wakulima walijaribu wasiende sokoni lakini bei ya kahawa inaendelea kuporomoka, hiyo maana yake nini? inapunguza uwezo wa Taifa kwenye pesa za Kigeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuomba sana Bunge lako liielekeze Serikali iweze kutatua matatizo haya kwa haraka na haya matatizo yanaweza kutatuliwa kukiwa na checks and balances kwenye Wizara zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naangalia suala la mikopo kwa watu binafsi. Makusanyo ya ndani kwa Halmashauri ni Bilioni 860, asilimia 10 ni Bilioni 86, hizo asilimia 10 ni kwa ajili ya kuwakopesha vijana na wakina mama, siyo pesa ndogo! Mtaji wa Benki ni Bilioni 15. Hizi pesa zingepelekwa kwa wataalam tukaangalia tukawasaidia wakina mama pamoja na vijana Tanzania inaweza kubadilika ndani ya miaka Mitatu na wewe ukashangaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bilioni 86 ni leo, mwaka kesho tena zipo zingine zitaenda kwenye hiyo Mfuko. Changanya na hiyo Mifuko mingine ambayo iko kwenye Wizara zingine, kwa kuwa Mkopo siyo kumpa mtu hela! Mkopo ni kumsaidia mtu aweze kuzalisha, mkopo ni kumsaidia mtu aondoke kwenye umaskini awe tajiri. Sasa hatuwezi kuwasaidia vijana wetu, wamekuwa wakichukua hizi fedha za mikopo lakini unakuta siku ya marejesho wanakimbia na sisi tunaotoka mipakani wengine wanakimbilia mpaka nchi jirani. Kwa hiyo, ningeomba hili lichukuliwe kwa uzito wake na tusianze mambo mapya wakati mambo mazuri yapo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, innovation haina maana uanze na kitu kipya. TAZARA inafanya nini! Trillions of money zimelala ardhini! TAZAMA pipeline, Tanzania ina asilimia 33 imelala inafanya nini! Magari yanaua watu wetu barabarani badala yake mafuta yangesukumwa yakaenda Nyanda za Juu Kusini, kukawa na Dry Port pale Mbeya wakachukua mafuta kutoka hapo! Lakini unaweza kuyasafirisha hayo mafuta yakaenda mpaka Malawi na Zambia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiwa na mtazamo wa namna hiyo ndiyo sababu ni bora tukawa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Njeza muda wako umekwisha, ahsante.

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru sana naunga mkono hoja. (Makofi)