Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Stella Simon Fiyao

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika mpango huu na hasa katika mapendekezo ya Mpango wa mwaka 2023/2024.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaendelea mbele sana, kuna wakati ni vyema tukaenda sawa na Watanzania na tukatoa ufafanuzi mzuri ili Watanzania wakatuelewa, hasa tunaposema uchumi wa Tanzania umekua, tuwe tunawafafanulia wananchi, huo uchumi umekua kwa namna gani? Kwa sababu uhalisia wa kile tunachokisema na ukienda kwa hali za Watanzania huko uraiani, ni mbaya kila kunapoitwa leo, zinazidi kuwa mbaya. Kwa hiyo, Watanzania hawaelewi wanaposikia uchumi umekua, wanajiuliza huo uchumi unakua kwa namna gani? Kwenye makaratasi au mifukoni kwao? Kwa hiyo, kuna wakati tuwe tunawafafanulia Watanzania ili wawe wanaelewa maana halisi ya uchumi kukua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda huko uraiani, sasa hivi hata Mtanzania aliyekuwa ana uwezo wa kula milo mitatu, sasa hivi hata kula mlo mmoja ni shida. Hali ni mbaya, biashara haziendi, hali siyo nzuri kiukweli. Kama Taifa, lazima tufike mahali tuwafafanulie Watanzania huo uchumi tunaosema umekua, ni kwa namna gani, ili tuwe tunaenda sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala zima la nishati, hasa katika mpango huu. Katika mpango huu nataka kujua Mpango hasa wa Taifa ni upi katika suala zima la kukabiliana na changamoto kubwa ya umeme ambayo ipo huko mikoani kwetu? Naweza nikasema hata wa Mikoa kama Dodoma na maeneo mengine wanaweza wasinielewe, lakini uhalisia sisi tunaujua wananchi wa Mikoa ya Mbeya na Songwe, hali ya nishati ya umeme ni mbaya sana na kwa wakati mwingine unaua mpaka uchumi wa Wana-Songwe. Sasa katika kufuatilia mpango sijaona kabisa kwamba Wizara ina mkakati gani wa kukabiliana na changamoto kubwa hii ya umeme ambayo imekuwa ni shida kwa wananchi wetu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia mpango, ni vyema tukaja na mikakati, lakini ukisoma katika ule ukurasa wa 122 kipengele (f), utaona wanasema, “kuongeza uzalishaji wa umeme kutoka vyanzo mbalimbali, kujenga na kukarabati miundombinu ya usafirishaji na usambazaji wa umeme. Hizi ni sababu za kawaida ambazo hata mtoto mdogo huko Songwe anazijua. Sisi Wanasongwe tunataka mkakati, kwa sababu kiukweli umeme umechangia kuzorotesha uchumi wa Wanasongwe isivyokuwa kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Songwe tulianza mgao kabla ya mgao. Suala la kukatika umeme Songwe ni hali ya kawaida mpaka masaa 24 umeme hakuna. Uchumi wa Wanasongwe unakufa. Wananchi wadogo wadogo ambao wamejiwekeza wanashindwa kuendeleza maisha yao kwa sababu tu yakukosa umeme. Hivi tunawaweka kwenye kundi gani hawa wananchi wa Mkoa wa Songwe? Tunaua uchumi wa Wanasongwe. Hasa ukizingatia tunavyozungumzia Mkoa wa Songwe, ule Mkoa ni langu kuu la SADC; Mataifa mengi yanaingia kwa kupitia Mkoa wa Songwe hasa Mji wa Tunduma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, fikiria unaenda katika lango la SADC masaa 24 Mji ni giza. Hebu fikiria! Tunaposema Tunduma ama Songwe ni lango, tunamaanisha. Mwananchi yeyote au mgeni yeyote anapoingia kupitia mpaka wa Tunduma, anapofika Tunduma, tafsiri yake ile, ndiyo anaiona sura halisi ya Tanzania. Sasa kama sura halisi ya Tanzania ina uwezo wa kukaa giza masaa 24, tunaeneza picha gani kwa wageni ambao wanaingia katika nchi yetu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii haikai sawa. Kuna wakati najiuliza, hivi Serikali inapotuambia kwamba ina uwezo wakuzalisha umeme na kuuza nchi nyingine, inamaanisha nini? Au tunawadanganya Watanzania! Kwa sababu huwezi kuzalisha umeme ambao una uwezo wa kwenda kuuza kwenye Mataifa mengine ikiwa watoto wako ndani tu umeme hauwatoshi. Hii tunamaanisha nini? Tuache kuwadanganya Watanzania. Tuongelee uhalisia, tatizo ni nini ambalo linapelekea umeme kukosekana kila kunapoitwa leo? Vingine tujiulize, kwamba Dodoma na Songwe imekuwaje? Hii si ni Tanzania moja! Mbeya na Dodoma si ni Tanzania moja! Sasa inakuwaje? Kwamba tumewaweka wananchi kwenye mataba! (Makofi)

Mheshimniwa Mwenyekiti, ukienda leo Mkoa wa Songwe kilio kikubwa cha wananchi ni umeme. Hawana amani, wananchi wanashindwa kuzalisha, wanashindwa kuendeleza biashara zao, wanashindwa kuendeleza viwanda kwa sababu ya umeme. Kwenye mpango huu nilitarajia Wizara, ituambie...

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpe taarifa mzungumzaji, kwamba huu mgao wa umeme ni nchi nzima, hata Nyang’hwale huwa tunakosa. Asiseme kwamba kuna ubaguzi na matabaka. Umeme mgao upo kwa nchi nzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nampa taarifa, ahsante sana. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Stella, taarifa hiyo.

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, hii taarifa ninaipokea kwa mikono miwili. Shida wanayokutana nayo wananchi wa huko Nyang’hwale, ndiyo wanayokutana nayo wananchi wa Mkoa wa Songwe kwenye lango kuu la SADC, ni ajabu. Tufike mahali tuambiane ukweli hapa. Wananchi huko hawatuelewi. Tuambieni kwa nini mnatuletea taarifa tofauti, kama tuna uwezo wa kuzalisha umeme wa kuuza nje ya nchi, kwanini ndani usitutoshe? Hii ina maana gani? Ina maana gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali za wananchi wetu ni mbaya, mbaya sana, tunaua uchumi wa Wanasongwe. Hatuwezi kuvumilia kuona hiki kitu kinaeandelea, lakini wakati huo kwenye mpango hatuoni ukija na mikakati madhubuti ya kukabiliana na hili tatizo la umeme. Ili tuende sawa, ni vyema Wizara ya Fedha ikatuletea mpango madhubuti wa wa kukabiliana na changamoto hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii tunazungumzia viwanda. Hivi kiwanda kipi kinaweza kuendeshwa bila umeme? Kipi hicho kiwanda? Kiwanda kipi? Labda kama tutatumia generator na solar tuambiane hapa, lakini kama tunategemea huu umeme; ndiyo maana kuna wakati wananchi wanahoji kwamba hata hiyo reli ya SGR, hivi itategemea huu huu umeme uu kuna umeme mwingine? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tufike mahali tuambiane ukweli, na tuombe Wizara ya Fedha ije na mpango madhubuti ni namna gani imejipanga kukabiliana na changamoto kubwa ya umeme ndani ya Taifa letu? Ahsante sana. (Makofi)