Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Zaytun Seif Swai

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami naomba nikushukuru kwa fursa hii uliyonipa ya kuweza kutoa maoni yangu kwenye Mapendekezo haya ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa wa mwaka 2023/2024. Kama Mjumbe wa Kamati ya Bajeti nami nilishiriki katika uchambuzi huu na ninaunga mkono mapendekezo yote ya kamati yaliyotolewa. Nikianza na hali ya uchumi wa Taifa, naomba nianze kwa kuipongeza sana Serikali kwa juhudi zake za kuendeleza ukuaji wa uchumi chanya na tuko kwenye mwelekeo sahihi kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia hadi robo ya mwaka tulifikia ukuaji wa uchumi wa asilimia 5.4 kutoka asilimia Tano kipindi kama hichi mwaka jana. Ukiangalia nchi nyingi katika ulimwengu huu sasa mwaka 2021 walikuwa na ukuaji wa uchumi kwenda kwenye uelekeo hasi wa hadi wastani wa asilimia 3.1. Kwenye hili utaona kabisa jitihada kubwa zilizofanywa na Serikali yetu katika ku- maintain uelekeo mzuri wa ukuaji wa uchumi wa nchi yetu. Hii yote imechangiwa sana na juhudi za Serikali katika kukabiliana na majanga makubwa na changamoto za kidunia ikiwemo UVIKO-19, kwa hiyo ninaipongeza sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia Sheria ya Bajeti, Sura Namba 439 utaona uandaaji wa mapendekezo haya umetumia mambo mbalimbali ikiwemo Dira ya Taifa ya Maendeleo, Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya 2020, vilevile tumeangalia mikakati mbalimbali ambayo tumejiwekea kama Taifa ya maendeleo. Nitaomba nizungumzie jambo moja la mikakati ya Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia, juzi tu hapa, Rais wetu amezindua mkakati kabambe kwa ajili ya Taifa kuhakikisha Watanzania wote wanatumia nishati safi na salama kwa ajili ya kupikia. Nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa uamuzi huu na huu ndiyo mwelekeo wa kidunia. Ajenda hii ya nishati safi na salama kwa ajili ya kupikia ndiyo mjadala unaoendelea dunia nzima hivi sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais wetu alisema kwamba katika mkakati huo kama Watanzania basi Serikali itahakikisha kwamba Watanzania wote wanatumia nishati safi na salama hadi kufikia mwaka 2032. Kwa hiyo, hii ni dira ya miaka 10 kwa hiyo ninaimani kwamba mkakati huu lazima tuuone kwenye mpango wetu wa mwaka mmoja mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mheshimiwa Rais alienda mbali zaidi na kuzitaka taasisi zote zenye kulisha watu zaidi ya 300 kuweza kutumia nishati safi na salama ndani ya mwaka huu mmoja yaani 2023. Katika hotuba yake Mheshimiwa Rais aliahidi wananchi kwamba Serikali itatenga bajeti kwenye bajeti ya mwaka 2023/2024 zaidi ya Bilioni 23 kwa ajili ya Watanzania waweze kutumia nishati hizi safi na salama kwa ajili ya kupikia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepitia mapendekezo haya ya mpango na hotuba ya Mheshimiwa Waziri hapa, lakini sijaona reflection ya maagizo haya ya Mheshimiwa Rais kwenye mapendekezo haya ya mpango huu. Namuomba sana Mheshimiwa Waziri akileta mpango wake hapa wa mwaka 2023/2024, basi tuweze kuona mapendekezo haya ya matumizi ya nishati safi na salama kwa ajili ya kupikia yanaingizwa kwenye mpango huu wa Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Taifa tukiweza kutekeleza nishati safi na salama kwa ajili ya kupikia, basi tutaweza kuokoa maisha ya wananchi wetu wengi ambao wanafariki kwa ajili ya magonjwa ya mifumo ya afya. Vilevile tutaweza kuokoa fedha nyingi za kuwatibu wananchi hawa, pia tutaongeza nguvukazi kwa ajili ya kufanya maendeleo mengine ya Taifa. Vile vile tutaokoa muda wanaopoteza wananchi wetu hususani kinamama wanaopoteza kwenda kutafuta kuni porini na hivyo watatumia muda huo kwa ajili ya kufanya shughuli zingine za maendeleo na kujenga nchi. Vilevile tutaokoa muda wanaopoteza wananchi wetu hususan akina Mama wanapoenda kutafuta kuni porini na hivyo watatumia muda huo kwa ajili ya kufanya shughuli zingine za maendeleo na kujenga nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tutaweza kutunza mazingira yetu ambayo mpaka sasa tathmini zinatuambia kwamba tukihitaji tani moja ya mkaa lazima tutumie tani Saba za magogo. Hivyo, tunaona ni jinsi gani suala hili linavyoweza kuharibu mazingira yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nitoe maoni yangu kwenye ushirikiano uliopo kati ya Wizara zetu za kisekta na Wizara yetu ya Fedha. Tumejionea hapa mara kwa mara tunaona hakuna coordination ya kutosha kati ya Wizara ya Fedha na Wizara hizi za Kisekta. Kama nilivyotoka kueleza hapa, suala la nishati safi na salama unaweza kukuta limebebwa kwa uzito wake na Wizara ya Kisekta lakini halijaweza kuingizwa kwenye mpango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Vilevile kwenye suala la Royal Tour tumeona kazi kubwa iliyofanywa na Serikali yetu kwa ajili ya kuitangaza nchi yetu kwenye utalii, mpaka sasa hivi tunajivunia kuwa mahoteli yamejaa kwa sababu ya kulaza wageni wetu na booking mbalimbali za watalii tuliowapata lakini suala hili halijaingizwa kwenye mpango na ni suala ambalo hata Kamati kipindi kilichopita kwenye bajeti tulishauri Wizara. Kwa hiy,o lack of coordination ni jambo ambalo linazisumbua Wizara hizi, naomba sana Waziri pamoja na Serikali tuweze kuwa na mahusiano mazuri ili basi mikakati yetu yote ya Kitaifa iweze kuingia kwenye mipango yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kujaza mahoteli tu siyo suala ambalo tunatakiwa tujivunie sana. Mahoteli yakijaa ina maana watalii wetu wakifanya booking wanaweza wakaenda hata nchi jirani kwa sababu hoteli zetu zimejaa. Kwa hiyo, kama taifa naomba tuje na mpangomkakati wa kuweza kuongeza hoteli zenye hadhi ya kulaza wageni wetu na kwenye mpango wa 2023/2024, basi tuone mambo haya yakitekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona sekta hii ya utalii ilivyo na nguvu ya kunyanyua uchumi wa nchi na inachangia zaidi ya asilimia 17 ya Pato la Taifa lakini asilimia 25 ya fedha za kigeni, hivyo ni muhimu sana tuweze kujikita kwenye sekta hii ambayo ni muhimu sana kwa uchumi wa nchi yetu. Vilevile tuendelee kuongeza bajeti katika Wizara hii ili basi tuweze kuistawisha sekta hii zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na ninaunga mkono hoja. (Makofi)