Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru sana kunipa nafasi. Awali ya yote nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa jitihada za kuleta maendeleo katika nchi yetu. Pia nimpongeze Waziri mwenye dhamana kwa kuwasilisha mpango ambao kama utafuatwa utakuwa na manufaa ya siku za baadaye. Niipongeze Kamati ya Bajeti kwa mawazo yao mazuri sana ambayo wameishauri Serikali. Mimi naamini mawazo yaliyowasilishwa na Kamati ya Bajeti mengi ni yale ambayo Wabunge wengi wamekuwa wakiishauri Serikali lakini kwa bahati mbaya huwa hayatekelezwi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nianze mchango wangu kwenye sekta ya kilimo. Sekta ya kilimo ni sekta ambayo inawagusa wananchi wengi hapa nchini. Na Serikali kama inadhamira ya dhati kuwasaidia kundi kubwa la wakulima watakuwa na maendeleo makubwa sana na nchi itanufaika. Lakini kilimo ambacho tunakishauri kwa Serikali ni uwekezaji mkubwa ambao lazima Serikali iwe na dhamira ya dhati kuhakikisha wanatoka kwenye kilimo cha kubahatisha tuingie kwenye kilimo ambacho kina uhakika, cha umwagiliaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu ina maeneo mapana ambayo tuna maziwa na mito mikubwa ambayo haitumiki vizuri. Maeneo mengi yanafaa kwenye shughuli za kilimo lakini kwa bahati mbaya nchi yetu ilishakuwa na mabadiliko ya tabia nchi. Sasa kwa kuwa kuna mabadiliko ya tabia nchi, lazima Serikali ije na mkakati wa kutumia rasilimali zilizopo kwa ajili ya kuwasaidia wakulima ili waweze kulima kilimo ambacho kina uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matajiri wote duniani wanatengenezwa na Serikali. Kama Serikali haijawatengeneza matajiri, huwezi kuwapata. Matajiri hao ni hao hao Watanzania ambao wapo. Wanachohitaji ni uwezeshwaji. Rasilimali ya kwanza waliyonayo ni ardhi ambayo haijatumika vizuri kwa sababu taasisi nyingi za fedha hazitoi mikopo kwa wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naiomba sana Serikali kupitia Wizara ya Fedha, tuache mipango ile ambayo haitekelezeki. Tumeanzisha Benki ya Kilimo ambayo kimsingi haijamkaribia sana mkulima. Taasisi zile za fedha tunaomba ziandae mpango mkakati ambao utakuwa chini ya Wizara ya Fedha na Mipango kuhakikisha wanawawezesha wakulima ambao wanaweza wakatoa tija kwa kiwango kikubwa sana. Naomba hili mlifanyie kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine kwenye Sekta ya Kilimo ni kuwawezesha wakulima watoke kwenye kilimo cha jembe la mkono. Wakulima wengi wanalima kilimo cha kujikimu, wawezesheni wapewe zana za kisasa, sambamba na kuwawezesha kuwapa eneo la masoko, itawafanya wakulima wawe na manufaa na watu wengi watakimbilia kwenye Sekta ya Kilimo. Naomba hili Serikali ilifanyie kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo maeneo ambayo Serikali ikiwawezesha katika eneo la masoko, kwenye sekta ya kilimo kutakuwa na ukuaji mkubwa sana, Tumezungukwa na nchi ambazo uzalishaji wake ni mdogo...

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumpa taarifa mchangiaji kwamba pamoja na wakulima kutumia jembe la mkono, lakini wakulima hao hao kwenye korosho mwaka huu wamepata shilingi bilioni 300, kwenye tumbaku shilingi bilioni 600, kwenye pamba shilingi bilioni 275, lakini hawana matrekta. Pia mabenki hayo hayo yametangaza riba kutoka 15% mpaka 9% lakini kwa wakulima bado masharti ni makubwa sana. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Moshi Kakoso.

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa hiyo ambayo ameitoa Mheshimiwa Cherehani, ingawa bado pamoja na hiyo taarifa tunayopata, tija ni ndogo. Kipato wanachokipata wakulima bado hakitoshelezi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wetu kwa Serikali, tuwekeze kwa kiwango kikubwa kwenye sekta ya Kilimo. Pamoja na kwamba mwaka huu Serikali imetoa fedha kwa ajili ya kutoa ruzuku ya pembejeo, lakini kwenye maeneo ya kilimo cha umwagiliaji na uwezeshaji mkubwa kwenye sekta hiyo ya kilimo kutoka kwenye jembe la mkono kwenda kwenye kilimo cha kisasa ni muhimu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nashauri Serikali ni miradi inayowekezwa na Serikali kwenye sekta ya ujenzi. Nakubaliana na wachangiaji wenzangu ambao wamechangia kwamba Serikali iachane na mpango wa kuanzisha miradi midogo midogo hasa ya ujenzi wa barabara. Ujenzi huu utaifanya Serikali iwe inatumia gharama kubwa lakini tija yake inakuwa ndogo. Mwaka huu tulipitisha bajeti na mpango uliopita wa mwaka jana 2021, walionesha kila eneo kwamba wanaweza kupeleka Kilometa 25, kitu ambacho hakiwezekani. Ni lazima Serikali iwe na mpangilio wa maeneo ya kipaumbele cha kujenga miradi ya maendeleo. Tukifanya hivyo tutakuwa tumeisaidia sana Serikali kuliko kama ilivyo sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Shabiby ameishauri Serikali kujenga miradi ya maendeleo ya ushirikishaji wa PPP na ile ambayo imekuja Wizara ya Fedha ya EPC iliyopendekezwa. Tunaafikiana nayo, lakini hoja yetu hap ani kwamba iharakishe mpango mkakati kuliko iliyopo tu kwenye mipango ya kwenye makaratasi. Tunaishauri Serikali iharakishe mpango huu, utasaidia kufanya maboresho makubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo Serikali ni vyema ikapeleka miradi ya maendeleo ni kwenye maeneo ambayo yatakuwa yana return ya urejeshaji wa fedha zilizowekezwa kwa kiwango kikubwa. Tunajenga reli. Reli ambayo ina manufaa makubwa ni reli ya kutoka Tabora kwenda Kigoma; reli ya Kaliuwa - Mpanda – Karema. Hizo ndizo reli ambazo zina uwezo mkubwa kuweza kutoa manufaa makubwa sana. Serikali imewekeza uwekezaji mkubwa wa Bandari ya Karema.

Mheshimiwa Mwenekiti, sasa hivi wafanyabiashara wa DRC Congo walishaanza kusafirisha shaba kwa njia ya mashua ambayo inatuharakisha sisi tupokee kwamba ni fursa iliyopo, tuweze kuitumia vizuri. Kwa hiyo, tunaiomba Serikali mchango mkubwa wa uwekezaji wa reli uwekezwe kwenye reli ya kutoka Tabora kwenda Kigoma na kile kipande cha kutoka Uvinza kwenda Msongati hadi Burundi. Hata hivyo, reli ya Kaliuwa - Mpanda hadi Karema ni muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie miradi ya maji. Tuna miradi ya maji mingi midogo midogo ambayo haiwasaidii Watanzania. Tukichukulie mfano wa Mikoa ya Kigoma, Katavi na Rukwa, ni mikoa ambayo imezungukwa na maziwa. Kwa bahati mbaya, hakuna mradi mkubwa wowote unaounganisha miradi hii ya maji. Naomba tutumie fursa tulizonazo vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, nizungumzie suala la uvunaji wa hewa ya ukaa. Tanzania ina misitu mingi na Wizara tumeishauri mara kwa mara na kwa bahati mbaya hawajaitumia hii fursa vizuri. Wenzetu Kenya wanaitumia fursa ya uwekezaji mkubwa kwenye uvunaji wa hewa ya ukaa. Kwa nchi yetu sasa hivi tuna maeneo kama matatu; Mkoa wa Katavi, Kiteto, eneo la Mkoa wa Manyara na Ruvuma, wameanza uvunaji lakini kwa kiwango kidogo sana. Tunaomba sasa Serikali ije na sheria mpya ambayo itafanya mabadilko hata kwenye maeneo ya hifadhi za Taifa, tuweze kuvuna hewa ya ukaa kama wenzetu Kenya wanavyofanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tumekuwa tukitoa mawazo haya na kwa bahati mbaya sana Serikali haifanyii kazi. Naomba sana Mheshimiwa Waziri, itumie nafasi hiyo ili muweze kupata fedha nyingi ambazo wenzenu jirani Kenya wanazipata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwenye sekta ya utalii. Utalii ulielekezwa ukanda wa Kaskazini, lakini nchi yetu ina maeneo mengi ambayo yana vivutio vya utalii na kwa bahati mbaya havijatumika vizuri. Naomba na maeneo hayo yafanyiwe kazi. Ahsante.