Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Kavejuru Eliadory Felix

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Buhigwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. KAVEJURU E. FELIX: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi hii adhimu ili niweze kutoa ushauri kwenye Mpango huu wa Maendeleo. Ushauri wangu utajikita katika maeneo matatu: Kwanza, ni kwenye zao la chikichi; pili, ni zao la kahawa; na kama muda utatosheleza basi nitakuwa na ushauri kwenye shughuli ya uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika nchi yetu idadi kubwa ya watu wamejiajiri kwenye kilimo. Asilimia 65 ambayo ukipiga hesabu kwa sasa hivi ambayo tumepata idadi ya milioni 61 ya Watanzania, kama asilimia 65 ndio inayoshughulika na kilimo, basi ukipiga hesabu kwa harakaharaka utakuta kwamba kilimo kimeajiri zaidi ya milioni 39.6.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa takwimu za mwaka jana 2021, Sekta hii ya Kilimo ilichangia kwenye pato la Taifa asilimia 26.1, ukilinganisha idadi ya wanaoshughulika na kilimo na kiwango kinachochangiwa kwenye pato la Taifa haviwiani kabisa. Hapa kuna gap, tunatakiwa tuangalie ni kitu gani kinachokosekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo mambo ya jumla ambayo bado tunatakiwa tuyafanyie kazi. Kwa kuwa idadi kubwa ya Watanzania wamejiajiri kwenye shughuli ya kilimo, basi Serikali inahitaji kuwa na jicho pevu la kuwekeza hasa hasa kwenye shughuli za kilimo na hasa kwa kuboresha miundombinu ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza na zao la chikichi; nchi yetu kwa mwaka imetumia zaidi ya bilioni 500 kuagiza mafuta. Mafuta mengine ambayo yanatokana na zao la chikichi ambalo tayari Mwenyezi Mungu amekwishatupa lipo Kigoma. Kigoma ina ardhi inayofaa kwa chikichi pamoja na Katavi. Nchi ya Malaysia ambapo tunaagiza mafuta walipata mbegu ya mchikichi kutoka Kigoma. Tunatumia zaidi ya bilioni 500 kuagiza mafuta ambayo tayari tungeweza kuzalisha Kigoma na hizo hela zingine zikatumika kwenye maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe ushauri, kwanza kabla ya kutoa ushauri nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi kubwa ambayo ameifanya kwa Mkoa wetu wa Kigoma. Amehamasisha wakulima wapanue mashamba, walime na kweli wamehamasika na wamelima zao la chikichi mashamba sasa ni makubwa. Kituo cha TARI kimezalisha mbegu na miche mizuri wamehamasika. Changamoto ambayo Serikali inatakiwa ikafanyie kazi ili tuokoe hayo mabilioni ni kuleta viwanda vya kati vitakavyoweza kuchakata zao hili la michikichi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, viwanda tulivyonavyo Kigoma ni vidogovidogo, kutokana na zao la chikichi, unapata mafuta haya ambayo ni ya kula tunayatumia kila siku, unapata chakula cha mifugo bado unapata malighafi ya kutengeneza samani za nyumbani na bidhaa nyinginyingi. Naomba kwenye Mpango huu wa Serikali, Wizara ya Kilimo ishirikiane na Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara kutafuta wawekezaji wa ndani na nje ili wajenge viwanda vya kuchakata mafuta katika Mkoa wetu wa Kigoma. Tukifanya hivyo tutakuwa tumeokoa fedha nyingi na nchi itakuwa na uwezo wa kupata mafuta yenyewe ya kuzalisha mafuta na kutosheleza mahitaji ya ndani na ziada tutapeleka kwenye nchi zingine, tutauza kama biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu ya pili, ni kwenye zao la kahawa. Kahawa ni zao la biashara ambalo linatuingizia fedha za kigeni. Katika nchi yetu ya Tanzania zaidi ya mikoa 16 inalima zao la kahawa. Tunashukuru kwa juhudi kubwa na tunamshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ruzuku ambayo ameiweka kwenye mbolea. Watu tunaolima kahawa ametugusa, tunasema mama ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zao hili bado halijapewa kipaumbele na ndiyo mwarobaini ambalo linaweza likatuingizia fedha za kigeni. Ukilinganisha na nchi zingine ambazo wanazalisha lakini kwa maeneo madogo, bado miche inayozalishwa na TARI na TaCRI bado ni midogo ukilinganisha na nchi jirani. Uganda kwa mwaka wanazalisha miche ya kisasa bora zadi ya milioni 61. Ethiopia ambayo ndio wazalishaji wa kwanza wanazalisha miche kwa mwaka zaidi ya milioni 121, lakini sisi Tanzania kwa mwaka huu ndio tumeongeza tumezalisha miche milioni 21. Hiki ni kiwango kidogo sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa tunayo maeneo makubwa na wananchi wamehamasika na tuna vijana wengi ambao wako mitaani, kama zao hili likiboresha, likawekewa pembejeo zote asilimia mia, sawa na korosho nina uhakika kwamba mapato yatakayotokana na kahawa yataongezeka na hela za kigeni zitaongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba mambo yafuatayo yafanyike, bado kwenye kilimo hicho hicho cha kahawa, tunahitaji kuwekeza kwenye tafiti. Naomba Mpango huu uoneshe ni namna gani ambavyo itawekeza kwenye tafiti za kupata miche bora na usambazaji wa matokeo yake ya utafiti na kwa kuwa kilimo ndio uti wa mgongo, basi Mpango unaokuja ni lazima, bora, vyema uoneshe namna gani ambavyo wakulima wataweza kupewa mafunzo pamoja na Maafisa Ugani ili uzalishaji uweze kuongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, soko la kahawa, watu wamehamasika wanalima kahawa lakini soko lake limekuwa likipanda na kushuka. Mkulima amekuwa akilima lakini bila kuwa na uhakika wa masoko. Tunaomba Mpango wa Serikali katika bajeti ijayo ituwekee masoko, ituonyeshe masoko ili wakulima wawe wanalima wakijua kwamba masoko ya zao hilo la kahawa ni wapi na wapi. Tukifanya hivyo, basi Taifa litaweza kuingiza fedha nyingi za kigeni na uchumi wetu utaongezeka, utakua ili tuweze kufikia asilimia nane kama ilivyoelekezwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu ya tatu ni kwenye uvuvi. Tanzania katika Bara la Afrika ndio nchi iliyopendelewa na Mwenyezi Mungu tukapewa maziwa yote makuu, matano yako Tanzania, tuna Ziwa Tanganyika, Victoria, Rukwa, Manyara, Eyasi na maziwa mengine madogo madogo. Hata hivyo, mchango unaotokana na shughuli za uvuvi bado ni mdogo. Mwaka 1954 na mwaka 1957, Serikali ya Kikoloni ya Uingereza ilikuwa na Kituo chake cha Utafiti, walifanya majaribio wakachukua samaki aina ya sangara kutoka katika Ziwa Tanganyika ambalo halikuwepo katika Ziwa Victoria, wakaenda kufanya majaribio wakapata katika Ziwa Victoria kwa mwaka 1954 na 1957. Leo tunashuhudia sasa sangara inatuingizia fedha nyingi sana kutoka kwenye Ziwa Victoria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwenye upande wa uvuvi tuna vituo vile vya TAFIRI, viwezeshwe wafanye tafiti kutokana na haya maziwa madogo madogo ambayo tunayo. Wafanye tafiti ikiwezekana kama sangara anaweza bado akaenda kupandwa kwenye maziwa mengine madogomadogo au migebuka, au samaki wengine ziende kupandikizwa kwenye maziwa mengine madogo madogo ambayo sasa hivi mchango wake wa kiuchumi kwenye upande wa uvuvi ni mdogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu nyingine ya nne ni kwenye biashara. Mkoa wetu wa Kigoma uko mpakani ile ni gateway ya biashara ambapo pale tunapakana na Wakongo ambao zaidi ya nusu ya watu wa Kongo wako kwenye ukanda wa mashariki. Tungeomba kwenye mkakati ujao Wizara ya Uchukuzi iwezeshe kutengeneza zile bandari za nchi kavu ile ya Katosho na kuhakikisha ukamilishaji wa meli katika Ziwa Tanganyika, zikamilike mapema ili mzunguko wa kibiashara ukamilike na uende vizuri ili ile SGR itakapokamilika tayari ile Kongo ya Kati kuanzia Kalemii, Bukavu, Bujimai, kuja mpaka huku Kindu wawe wamekwishazoea wote kuja kufanya biashara na Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)