Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Samweli Xaday Hhayuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia Mpango wetu wa Taifa wa Mwaka 2023/2024. Kwenye wasilisho ambalo Mheshimiwa Waziri amelifanya ameainisha sekta ambazo zinafanya vizuri. Kati ya sekta tano ambazo zinafanya kazi vizuri ameongelea suala la Sekta za Maji, Fedha na Bima, Uchimbaji wa Madini na Mawe na Sekta ya Huduma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kwenye sekta zetu za msingi za uzalishaji hapa hazipo. Ukigusa kwenye upande ambao unatusumbua kwenye suala la mfumuko wa bei inayoongoza ni sehemu ya vyakula na viinywaji, ni asilimia 7.8. inamaanisha nini? Vyakula hivi vingi tunaweza kulima wenyewe. Kwa mwaka uliopita haukuwa mzuri kwa sababu tunategemea mvua za Mwenyezi Mungu. Mheshimiwa Kwagirwa aliongelea kidogo suala la kujaribu kwenda kupunguza tension ya gharama za maisha ya wananchi wetu huko vijijini kwa vyakula ambavyo viko kwenye maghala yetu ili vipelekwe kwa wananchi ili kupunguza mfumuko wa bei kwenye eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasisitiza ni muhimu sana kwa sababu kama mfumuko ni mkubwa kiasi hiki inaathiri uchumi wetu, Serikali ichukue hatua sasa bila kuchelewa. Kilimo kinachangia asilimia 26 kwenye pato la Taifa, lakini imeajiri zaidi ya Watanzania asilimia 65, ni watu wengi. Ili tuweze kulikwamua Taifa hili lazima eneo hilo tuliangalie kwa umakini mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuongeza bajeti ya kilimo kutoka Shilingi bilioni 294 mpaka Shilingi bilioni 954. Naamini kwamba changamoto hii ya ukuaji wa uchumi na intervention hii itakayofanyika katika kilimo itaenda kutusaidia. Tunamwamini Mheshimiwa Bashe kwa umahiri wake na hatua anazozichukua. Kwa sasa tunaenda kwenye msimu wa kilimo, wakulima wengi wanalia kwenye suala la pembejeo, masuala ya mbegu bora, naomba eneo hili tulisimamie vizuri. Wale wataalam wetu wa kilimo watoke maofisini sasa waende wakakae na wakulima kuona namna ya kuweza kuwasaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto kubwa tuliyonayo ni mbegu, natoa mfano kwetu Hanang tunaotegemea sana kilimo cha shayiri na ngano, mpaka sasa haujawekwa utaratibu mzuri wa kupata mbegu bora ya ngano. Hata hivyo, mara nyingi kila msimu unapoanza tunahangaika sana na mbegu ya shayiri ambayo mara nyingi wakulima wetu wamekuwa wakiingia mikataba na makampuni yanayozalisha vinywaji aina ya bia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba eneo hili lisimamiwe vizuri. Fedha zilizowekwa huku ni nyingi hizi fedha zilete tija kwenye ukuaji wa uchumi wa nchi yetu. Hata hivyo ili wakulima waweze kuzalisha ni muhimu sana kuwawezesha wakulima kwa mitaji. Benki yetu ya kilimo iweze kuwakopesha wakulima. Kwa sasa wanatoa mikopo lakini masharti bado ni magumu sana. Tumeanzisha Vyama vya Ushirika wa Kilimo na Masoko (AMCOS), nyingi ambazo zimeanzishwa lakini wakitaka kuanzisha mikataba ili waweze kukopa kwenye hizi benki bado kuna kitu wanaita mkataba wa utatu. Lazima kuwe na mkataba baina ya benki, wakulima wenyewe kupitia AMCOS zao na wale ambao watakuja kununua bidhaa hizo baada ya kuzalishwa. Serikali itengeneze mfumo wa hizi AMCOS zetu kuaminika bila kuhitaji nani atanunua bidhaa baada ya hapo, vinginevyo isaidie wakulima hawa kupata masoko ya mazao watakayozalisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nigusie eneo la mifugo. Wafugaji kwenye nchi yetu wengi wamekuwa kama wakimbizi, kila sehemu wanawindwa, kila sehemu kuna mwingiliano baina ya wakulima na wafugaji na kila sehemu wanawindwa. Katika kila sehemu wameonekana kama ni watu wakorofi, mtu yeyote bila kumpa elimu iliyostahiki ama kumtengea nafasi stahiki kwenye jamii lazima ataonekana mkorofi kwa sababu ataitafuta nafasi yake kwa namna anavyoona yeye. Ni muhimu sana kwa nchi hii, kuwatengenezea wafugaji utaratibu mahususi ili wafuge na hatimaye tuwape elimu waweze ku-transform mifugo yao kuwa ya kisasa na hatimaye wafuge ufugaji wenye tija kwao…

MHE. ZUBEIRI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

T A A R I F A

MHE. ZUBEIRI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nathamini sana mchango wa mchangiaji anayechangia, amegusa sehemu anasema kwamba wafugaji kwenye nchi hii wanaonekana ni wakorofi, lakini sio tu kwamba wanaonekana ni wakorofi, nature ya wafugaji ni wakorofi na wao kuua kwao ni jambo la kawaida.

MWENYEKITI: Hiyo sio taarifa. Endelea na mchango wako. (Makofi)

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana naomba niendelee. Nilichokuwa namaanisha wafugaji lazima tuwatengee eneo lao na tutengeneze mazingira, tuna mifugo mingi nchi hii, tuone namna gani inaweza kutuletea tija. Haileti maana yoyote, tuna ng’ombe wengi, mbuzi wengi, kondoo na kuku wengi, lakini bado tuagize nyama kutoka nje. Tuwajengee uwezo tutengeneze namna ya kuchakata mazao yanayotokana na mifugo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni eneo la ardhi; kilimo na mifugo yote inahitaji ardhi. Nimesema kabla kwenye Bunge hili kwamba ni muhimu ardhi yetu tuipange vizuri ili kila mtu aweze kupata sehemu ambako ataendeshea shughuli zake. Tupate ardhi kwa ajili ya kilimo, mifugo na shughuli nyingine ikiwemo viwanda. Ni muhimu sana kuipanga ardhi yetu vizuri na tutaondoa mwingiliano na migogoro mingine ambayo inajitiokeza kati ya wakulima na wafugaji na jamii nyingine. Tukiipanga ardhi yetu vizuri, tunaweza tukawa kwenye baadhi ya vijiji tukatengeneza ranches ndogondogo sio lazima tuwe na ranches kubwa ili tuweze kuwaweka wakulima wetu vizuri na hatimaye tuwaweke wafugaji vizuri ili shughuli zao ziweze kuleta tija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ardhi tukiitumia vizuri kwenye jamii yetu, mwenye ardhi anamkodisha asiye na ardhi ili alime, mwenye ardhi anamkodisha mfugaji ili aweze kulisha mifugo yake lakini pia kuna ile biashara ya kuuziana viwanja na kuuziana mashamba. Tukiirasimisha ardhi yetu yote, kwenye eneo hilo Serikali inaweza kutengeneza mapato. Tukiihusisha hata Serikali yetu mpaka hata ngazi ya kijiji, zile shughuli zinazofanyika kule tukaona namna ambavyo tunaweza kupata mapato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni muhimu sana ardhi tukiipanga na kuitumia vizuri italeta tija kubwa kwenye shughuli zetu za ukuaji wa uchumi. Hata hivyo, niombe kwenye eneo hili kuna ardhi ambayo tayari imeshapangwa, ardhi ambayo imelekezwa kwa ajili ya ranches kwa ajili ya mifugo, vilevile mashamba makubwa ambayo yapo kwa ajili ya kilimo. Maeneo hayo yatumike kimkakati ili yaweze kuleta tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa mfano wa ardhi ambayo iko ndani ya Jimbo langu la Hanang. Ardhi hii tuliwapa wawekezaji zaidi ya ekari 43,000, zaidi ya miaka
18 hatuoni tija sisi kama Wanahanang na Watanzania hawaoni tija yoyote.

Mheshimiwa Spika, maeneo kama haya nchi hii ni mengi, ninachoomba Mheshimiwa Waziri wa Kilimo nimekuwa nikiongea na wewe mara kwa mara nakushukuru kwa ushirikiano unaonipa. Ninachoomba zile kazi ambazo umeshaanza ya kutwaa ardhi ile ambayo haitumiki, kamilisha Ndugu yangu ili Wananchi wa Hanang’ waweze kufaidi ardhi ambayo iko kwenye maeneo yao, lakini ifanywe kwa nchi nzima ili ardhi zetu zilizolala ziweze kutumika kwa ajili ya uzalishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee kidogo kwenye upande wa utekelezaji wa miradi, ukuaji wetu wa uchumi inanyoongoza ni sekta ya maji lakini tunayo miradi mingi ya maji. Nashukuru sana Mheshimiwa Rais ametenga fedha kwenye eneo hilo, lakini kuna ucheleweshaji mkubwa wa utekelezaji wa miradi. Ukichelewesha mradi maana yake huduma zile ziliozotarajiwa zinachelewa, maendeleo yaliyotarajiwa kwa wananchi yanachelewa na inawezekana hiyo kazi tumewapa Wakandarasi tukiamini kwamba hiyo kazi wataifanya vizuri, tunaomba eneo hilo lisimamiwe kwa ukaribu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana ninaunga mkono hoja. (Makofi)