Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Dr. Hamisi Andrea Kigwangalla

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa fursa hii nami nitoe mchango wangu kidogo kwenye Mpango wa Maendeleo wa Taifa letu kwa mwaka mmoja unaokuja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika dunia ya sasa tunayoishi, viongozi wa zama zetu sisi, tutapambana na changamoto nyingi. Ukisoma taarifa ya Benki ya Dunia wanaweka changamoto 20, of course ndani yake humo yapo na yale mambo ambayo sisi hatuyakubali hapa kwetu, lakini katika yale mambo ambayo sisi tunayakubali, angalau nizungumzie matatu makubwa katika hizo changamoto. Ya kwanza ikiwa ni mabadiliko ya tabia nchi, pili ni umasikini uliokithiri, na ya tatu ni ile inayohusiana na njaa. Amezungumza vizuri sana Mheshimiwa Reuben Kwagilwa changamoto inayohusiana na kukosekana na uhakika wa chakula mezani miongoni mwa watu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi tatu zinahusiana kwa ukaribu sana, moja, baada ya nyingine; zina connectivity ya ukaribu sana. Kwa mfano, changamoto ya mabadiliko ya tabia nchi inapelekea kukosa uhakika wa chakula kwa watu wetu ambao wanategemea kilimo cha jembe la mkono. Hii moja kwa moja inaenda kusababisha mfumuko mkubwa sana wa bei (inflation). Amezungumza Mheshimiwa Kwagilwa, sina haja ya kurudia. Kwa sababu umasikini uliokithiri ambao unapimwa na Benki ya Dunia kwa kigezo kipya cha Shilingi 5,052/= kwa siku ambacho kimetangazwa juzi tu; maana yake ni umasikini wa kukosa kukosa mahitaji ya kawaida, ya lazima ya kila siku (basic needs). Watu wengi wanakuwa wamekosa mahitaji yao ya msingi kama vile malazi ya uhakika, chakula cha uhakika na mavazi yenye heshima na staha inayostahili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda katika hizo changamoto tatu zilizopo hapo, nijikite zaidi kwenye changamoto ya mabadiliko ya tabia nchi. Katika zama tunazoishi kumekuwa na ongezeko kubwa sana la idadi kubwa sana ya watu katika Taifa letu, na juzi zimetangazwa figures mbalimbali za Sensa ya Watu na Makazi na ukizitazama kwa jicho la kisayansi utaona kwamba idadi ya watu, miaka thelathini ijayo itakuwa ime-double. Kama sensa safari hii inatangaza watu milioni 61, maana yake tutakuwa tumefika watu zaidi ya milioni 120 ifikapo mwaka takribani 2050 na kitu au 2060 huko. Hili lina-pose a very huge challenge kwa uongozi wa sasa na uongozi unaokuja kuhusiana na uhakika wa maisha yetu hapa nchini na duniani kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku za hivi karibuni nimeona kuna clip moja inazunguka kwenye mitandao ya kijamii ya watu ambao wanaendesha bodaboda wakiwa wamepakia mkaa. Ukiona zile bodaboda na kulikuwa kuna mtu alikuwa anaongea kwenye hiyo clip akizungungumzia suala la mkaa akisema Ruvu hiyo, Ruvu hiyo. Pale unajifunza mambo kadhaa yafuatayo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza, ni kwamba tuna changamoto kubwa ya nishati ukanda wa Pwani. Nami nikaamua kwenda kutazama figures kwa sababu nakumbuka niliwahi kufanya kazi katika Wizara ya Maliasili na Utalii, na niliwahi ku- commission utafiti wa mahitaji ya mkaa hapa nchini. Nilipoenda kutazama figure zangu, kwenye ripoti ambayo niliwahi kuletewa huko nyuma katika mapito yangu, nilishtuka sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jiji la Dar es Salaam peke yake, kwanza katika nchi kwa ujumla wake kwa mwaka mzima tunatumia tani 1,895,248 za mkaa na asilimia 50 ya tani hizi za mkaa zinatumika katika Jiji la Dar es Salaam. Kwa sababu wakazi wa Jiji la Dar es Salaam kwa zaidi ya asilimia 95 wanatumia mkaa. Hii ni biashara kubwa sana ambayo sidhani kama tunaitilia maanani sana kama nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, biashara ya mkaa kwa utafiti wa mwaka 2014 uliofanywa na Benki ya Dunia kwa hapa Tanzania ilionesha ni biashara ya Shilingi bilioni moja ya Kimarekani. Kwa utafiti niliou-commission mimi nikiwa Waziri kipindi hicho, kwa mwaka volume ya biashara ya mkaa ilikuwa ni ya shilingi trilioni 2.5 za Kitanzania. Kama asilimia 50 ya biashara hii iko kwenye Jiji la Dar es Salaam maana yake unazungumzia pesa inayozunguka zaidi ya shilingi trilioni 1.2. Kwa wakati ule tulikadiria kwamba kutokana na kiwango cha kukusanya mapato cha shilingi 250 kwa kila kilo ya mkaa inayokusanywa na Serikali kwa maana ya Wakala wa Huduma na Misitu, tungeweza kukusanya shilingi bilioni 575 kama biashara ya mkaa ikiwa properly regulated, ikasimamiwa vizuri, badala ya check points zilizopo sasa hivi ambazo ni kama tu zinahalalisha tu watu ambao tayari wameshafanya uharibifu kwenye misitu, kama ikiwa regulated, namna nzuri ya kuvuna na kukusanya mapato tunaweza tukatumia fedha hizi kwenda kuwekeza kwenye uzalishaji wa mkaa huu wa clean energy kama vile briquettes, hizi tofali zinazotengenezwa kwa pumba za mpunga na vitu vingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunaweza kutumia pesa hizi kwenda kuwekeza kwenye utumiaji endelevu wa misitu (sustainable use of our forest resources), lakini bahati mbaya sana tunakusanya chini ya Shilingi bilioni 30 kwa mwaka kutokana na mkaa. Hilo lilikuwa ni jambo langu la kwanza ambalo nilipenda kulizungumzia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, nilipenda kuzungumzia suala la kuanzishwa kwa mfuko wa kuhifadhi bei za mazao; sijui kama nimetafsiri Kiswahili kwa usahihi, lakini nazungumzia Price Stabilization Fund; kwamba kama Taifa tunahitaji kuwa na mfuko maalum wa kudhibiti bei za mazao hapa nchini. Pia mfuko huu utatuwezesha kununua chakula pindi chakula kipo chini kwa uhakika zaidi na kukigawa kwa wananchi kipindi ambapo chakula kimepungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilisema pale awali kwamba changamoto kubwa hapa nchini kwetu kwa watu wetu wa kawaida ni chakula na mahitaji ya msingi tu, wala watu wetu hawataki mambo makubwa sana. Sasa kama tutaweka utaratibu mzuri wa chakula, na pia ili tuwe na utaratibu mzuri wa kuhifadhi chakula, maana yake tunahitaji utaratibu mzuri wa kuhifadhi mazingira, kwa sababu watu wetu wanalima kwa jembe la mkono na wanategemea zaidi kilimo cha mvua za Mwenyezi Mungu. Sasa kama hakuna mvua kutokana na uharibifu wa mazingira, maana yake hatutaweza kupata chakula cha kutosha katika Taifa letu.

Kwa hiyo, nilikuwa napenda kumshauri Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango katika mapendekezo yake aliyoyaleta atazame sana eneo la mabadiliko ya tabia nchi, na eneo la kuanzisha Price Stabilization Fund ili bei za mazao zikishuka, mfuko unaweka pale, wakulima wanapata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano kwenye korosho tuliwapa matumaini wakulima wa korosho, bei zikapanda mpaka zikafika zaidi ya shilingi 2,600. Kawaulize, leo wanauza korosho yao kwa shilingi ngapi? Ni chini ya shilingi 2,000. Kwenye pamba tuliwapa matumaini wakulima wa pamba na wafanyabiashara wa pamba kwamba pamba inakwenda mpaka shilingi 2,000; kawaulize mwaka huu wameuza pamba yao kwa Shilingi ngapi; na kama wanunuzi walikuwepo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ambacho kitaweza kututoa kwenye hii changamoto ya kutatua matatizo ya wakulima kila mwaka ni kuwa na mfuko...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla, ahsante kengele ya pili.

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)