Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Joseph Zacharius Kamonga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ludewa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ili nichangie Mpango wa Maendeleo ya Taifa. Nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Fedha na wataalam wake ambao wameshirikiana katika kuainisha vipaumbele mbalimbali. Katika kipaumbele ambacho kimenivutia zaidi ni kuona kwamba sasa Mchuchuma na Liganga inapaswa ianze kufanya kazi. Hili sio kwamba limeandikwa huku, niwe shuhuda hapa, hata kule jimboni kwangu wananchi wanaendelewa kuhakikiwa kwa ajili ya kulipwa fidia na maeneo yaliyosalia nayo yanaendelea kufanyiwa uthamini kwa ajili ya ulipaji fidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kumashukuru sana Mheshimiwa Rais wetu, Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuidhinisha hizo bilioni 11 kwa ajili ya kuwalipa fidia wananchi wa Nkomang’ombe, Iwela, Kipangala, Mundindi, Amani na wengine ambao walikuwa na mashamba yao kwenye ile miradi. Kwa hiyo niishukuru sana Serikali na niombe sasa baada ya uhakiki tu, wananchi wale waweze kulipwa fedha zao na miradi ianze kama ambavyo Serikali imeweka kipaumbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa napiga hesabu ndogo hapa, ule Mradi uliokwama wa makaa ya mawe, sasa hivi makaa ya mawe yamepanda sana bei duniani. Tani moja inafika mpaka USD 350 kwenye Soko la Dunia, lakini kwa ndani ni USD 50. Sasa ule mradi ulikuwa una mpango wa kuzalisha tani milioni tatu za makaa ya mawe ambazo ukizidisha tu kwa hizi USD 50 unaona kwa mwaka Serikali ingekuwa inapata karibu trilioni mbili kutokana na makaa ya mawe. Hizi ni fedha nyingi sana ambazo zingetusaidia sana kuepukana na zile kodi ambazo ni kero ambazo tunazianzisha na wananchi wanatulalamikia. Nadhani wazo sasa la kuona hii miradi ianze ni la msingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile upande wa Liganga, ule mradi ulikuwa umekusudia kuzalisha tani milioni 2.9 na kwenye Soko la Dunia kile chuma ghafi kwa tani moja ni USD 81.5. Kwa hiyo ukichukua hiyo, ukizidisha mara tani milioni 2.9 utaona kuna trilioni tatu na point ambazo Serikali ingelikuwa inazipata kutokana na uzalishaji wa chuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumechelewa sana kuanza hii miradi, uchumi wetu umechelewa, lakini kwa kitendo cha kuingiza kwenye Mpango sasa, naomba Bunge hili liweze kuunga mkono Mpango huu na tuisimamie Serikali kuhakikisha kwamba miradi hii inaanza ili tuweze kuingiza mapato mengi kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiacha hizo fedha pia kuna fursa nyingine nyingi, sasa hivi kuna changamoto kubwa sana ya ajira, sasa miradi hii ina uwezo wa kuajiri Watanzania hata milioni kumi ajira zile za moja kwa moja na bado kuna wale watakaokuwa wanapata ajira za udereva, wale watakuwa wanajiajiri kwenye kuanzisha garage, watakaoanzisha vituo vya mafuta na nyumba za kulala wageni, kwa hiyo tutatengeneza ajira nyingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukipitia takwimu za sensa ya watu na makazi ambazo Mheshimiwa Rais wetu amezisoma hivi karibuni, utaona Mkoa wa Njombe una idadi ndogo ya watu. Idadi ile siyo kwamba ndiyo watu wote walioko Njombe. Hii ni ishara kwamba Njombe watu wanazaliwa na kuhamia maeneo mengine. Kwa hiyo tunavyofanya decentralizations ya hizi projects, tunavyotawanya hii miradi tunasaidia vilevile ku-control ule mtawanyiko wa watu nchini, watu wasisongamane uelekeo mmoja. Kwa hiyo hawa watu milioni kumi wakipelekwa kule kwenye hizi ajira kwa kweli tutakuwa tumeinua sana uchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na miradi hii, lazima ionekane pia kwenye miundombinu ya barabara, kuna ile barabara inayoanzia Itoni – Ludewa - Manda, nashukuru sana Serikali wameidhinisha bilioni 95 upande wa Itoni mpaka Lusitu na bilioni 179 kutoka Lusitu mpaka Mawendi, lakini barabara hii haijafika Makao Makuu ya Wilaya na haijafika kwenye Mgodi wa Makaa ya Mawe ambapo ni kilometa 68 na haijafika Manda ambako kuna bandari ambayo nayo ingeweza kuunganisha usafiri wa mizigo kwa sababu tuna meli ya mizigo ambayo haina mzigo pale Ziwa Nyasa. Kwa hiyo barabara hii ikikamilika hata meli hii itaweza kufanya kazi vizuri na itapata mzigo wa kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna barabara pia inayounganisha Liganga na Mchuchuma, kwenye uwekezaji huu dhamira na Mheshimiwa Rais, ionekane pia katika kuandaa mazingira ya miundombinu ya barabara na Kiwanja cha Ndege cha pale Njombe. Vilevile kutoka Mkiu – Liganga - Madaba na ile Liganga na Mchuchuma ni kilometa 70. Kuunganishwa kwa barabara hizi ni ishara tosha kwamba miradi sasa itakuwa inaanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile pale Mlima Kimelembe sasa hivi kuna wachimbaji wengine wadogo ambao wanashindwa kusafirisha makaa ya mawe, tulikuwa tunahangaika bilioni sita ili ule mlima uweze kukatwa, lakini kwa mapato haya kama iwapo tutakata mlima, tani milioni tatu za makaa ya mawe zitasafiri, mapato yake ni trilioni mbili kwa nini tujiulize mara tatu kutoa bilioni sita kwa ajili ya kukata mlima? Kwa nini tujiulize kupata hiyo bilioni mia moja kwa ajili ya kukamilisha barabara? Kwa hiyo hoja ya msingi hapa ni dhamira, hivyo ni muhimu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya pili sasa niende kwenye kilimo. Ninaipongeza Serikali kwa kuendelea kutoa kipaumbele kwenye mipango yake kwenye sekta ya kilimo ni jambo zuri, vilevile kilimo kinakwenda sambamba na kuongeza thamani kwa mazao, viwanda mbalimbali ili kuongeza ajira kutokana na crisis ya ajira. Kwa hiyo, tuone pia namna ya kuongeza thamani ya mazao vile viwanda ili kuongeza thamani ya mazao kwa ajili ya kuongeza ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Serikali imetoa fedha nyingi kwenye sekta ya kilimo lakini bado nako kuna upungufu wa watumishi. Nitatoa mfano, kule Jimboni kwangu ninavyo Vijiji 77 lakini ninao watumishi wapatao 48 tu, kwa hiyo ilikuwa ni muhimu sana hizi fedha tunazopeleka na hii miradi ambayo imepokelewa vizuri kule na wananchi tuongeze pia wataalam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ninaipongeza Serikali kwa kutoa ruzuku kwenye mbolea. Najua mwanzo ni mgumu na niwashukuru wataalam, Mheshimiwa Waziri, Naibu wake na wataalam wake kuna mtu anaitwa Ngairo, yule bwana anapokea simu saa 24, nampongeza sana, ila sasa ule udongo kule kwetu Ludewa unahitaji mifuko mitatu ya mbolea. Hivi asubuhi nimepata taarifa, nimshukuru Mheshimiwa Waziri wa Kilimo, kuna ghala la pale Ludewa Kijijini kuna mbolea wananchi wanagawiwa, lakini foleni ni kubwa siyo tatizo, ila ombi lao ni kwamba, ekari moja inahitaji mifuko mitatu, mfuko mmoja wa dap wanapandia na mifuko miwili ya urea kwa ajili ya kukuzia. Kwa udongo ule ukiweka mbolea mifuko miwili huwezi kupata mazao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakulima wetu kutokana na wao kusomea field wamekuwa wataalam saa nyingine kuliko hata wataalam wa kilimo, wanaweza kukabiliana na mazingira yao. Kwa hiyo, niiombe sana Serikali tuweze kuwasikiliza hawa wananchi badala ya kuwapa mifuko miwili tuweze kuwapa mifuko mitatu ya mbolea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa, tumeanza sasa na changamoto na nimekiri kwamba Wizara inajitahidi, lakini tuongeze kasi ya kuwasimamia hawa mawakala ili waweke vituo maeneo yale ambayo ni catchment areas zenye wakulima wengi waweze kupata mbolea kwa wakati bila usumbufu ili tuweze kufidia hii changamoto ya mazao ya chakula ambayo imejitokeza kutokana na bei ya mbolea kupanda sana mwaka huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukifanya hivi na tukaendelea kuboresha barabara za vijijini hakika tutakuwa tumemkomboa mkulima. Kwa sababu, ataweza kutoa

mazao yake shambani kuyapeleka kwenye soko kwa ajili ya kujipatia kipato. Na hii itaendelea kuwapa hamasa wakulima kuweza kulima zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la mifugo na lenyewe pia kwa kuwa Wilaya yangu kwa mfano, nitatoa mfano Jimbo langu la Ludewa tunakwenda sasa kupata miradi mikubwa kutakuwa na uhitaji mkubwa sana wa maziwa, nyama, mayai na vitu kama hivyo. Sasa niiombe Wizara ya Mifugo itusaidie kule kuna vyama vya ushirika vya wafugaji, lakini hawana madume bora kwa ajili ya kuboresha ile mbegu ya ng’ombe wa mawziwa waliyonayo. Kwa sababu Ludewa mpaka sasa kwa takwimu ambazo nilizipata inaonesha kuna ng’ombe wa nyama 33,000 kwa hiyo, hawawezi kutosheleza. Kwa hiyo, tungeweza kuanzisha ranches kule Ibumi na wataalam wa kilimo walishaomba maeneo ya mashamba zile block farming na hizi ranch kule eneo la Ibumi, Masimavalafu tunahitaji sana usaidizi wa Serikali ili kuweza kufikia malengo yetu ya kuongeza idadi ya mifugo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naona kengele imegonga na mambo yangu sikumaliza. Niunge mkono hoja, nakushukuru sana. (Makofi)