Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi jioni hii kuchangia bajeti ya Waziri Mkuu. Kwanza napenda niishukuru Serikali kwa namna ambavyo Rais wetu amehangaika na kutupatia pesa kwa ajili ya kujenga majengo ya madarasa katika shule za sekondari. Jimbo letu tulipata takribani madarasa 51 ambayo yamewezesha shule zile kuonekana kama mpya, lakini pamoja na upya huo, kuna changamoto kwenye shule za msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama alivyozungumza mwenzangu Mheshimiwa Hassan Kingu, shule zetu zimechakaa. Pamoja na kuchakaa, watoto ni wengi sana. Nitatoa mfano mmoja kwenye Kata yangu ya Mtina ambayo ina shule saba. Tunahitaji madarasa 72. Shule ya Tupendane ina madarasa matano, lakini tunahitaji nane, ambayo yamepungua ni matatu. Shule ya Angalia ina madarasa nane, inahitaji madarasa 20, upungufu ni madarasa 12. Shule ya Azimio kuna madarasa saba, tunahitaji madarasa 21 na upungufu ni madarasa 14. Shule ya Mtina ina madarasa nane, tunahitaji madarasa 23 na upungufu ni madarasa15. Shule ya Semeni ina madarasa saba, yanahitajika madarasa 23 na upungufu ni madarsa 16. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa utaona mfano halisi, tumetoa tatizo kwenye shule za sekondari, lakini shule za msingi ni changamoto kubwa sana. Huo mfano ni kwenye kata moja tu kati ya kata 15. Kwa hiyo, tunahitaji zaidi ya madarasa 300 kwenye shule za msingi. Naomba sana tumwombe mama kama alivyofanya kwenye shule za sekondari, ahangaike atutafute pesa kwa ajili ya madarsa kwenye shule za msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na madarasa hayo, tuna upungufu mkubwa wa walimu. Kwenye shule za sekondari tumejenga madarasa mengi, lakini walimu hakuna. Pia katika sekta hiyo tunashukuru tumetangaziwa kutakuwa na ajira ya wafanyakazi 32,000, LAKINI kuna changamoto kubwa ambayo imezungumzwa na mwenzangu Mbunge wa Liwale, kwamba tunapata watumishi wengi lakini baada ya muda fulani wote wanahama kwa maana kwamba, maeneo yote ya Kusini yanakuwa ni sehemu za kuchukulia check number. Akishapata permanent employment, maana yake anahama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nina mapendekezo ambayo kidogo yanaweza yakatusaidia kupunguza hizi movements za wafanyakazi katika maeneo mbalimbali. Mnapopanga hao watumishi au mnavyoajiri, basi tuangalie kiukanda au kila Halmashauri au wilaya ipewe idadi ya kuajiri hawa wafanyakazi kulingana na mahitaji ambayo yapo. Tukifanya hivyo kila mmoja ataendelea kukaa katika maeneo yake ambayo ameajiriwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli kumtoa mtu Kagera kumpeleka Tunduru inakuwa ni mtihani mkubwa sana. Japo ni Tanzania, lakini mazingira yanatofautiana. Kwa hiyo, tunaomba sana kwenye ajira hii ya 32,000 Wizara ya Utumishi ijitahidi kugawa idadi hii katika maeneo mbalimbali kulingana na wilaya kwa sababu, huko vijijini kote tuna wasomi wamejaa; tuna walimu, watu wa afya, Maafisa Ugani na kada mbalimbali, degree zimejaa siku hizi vijijini. Sasa ajira hii tukiigawa kulingana na wilaya au Halmashauri, basi kila wilaya tutapata angalau wafanyakazi kadhaa ambao wataweza kufanya kazi katika maeneo hayo yanayohusika.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi inavyoonekana, watumishi wengi wanatoka katika sehemu moja, maeneo mengine kunakuwa watumishi hawapo, sasa tunakuwa tunawanyima haki ya kuendelea kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nilipenda niongelee katika bajeti hii ni suala la kilimo. Kwetu Kusini, mfumo wa stakabadhi ghalani kwa kweli, umekuwa ni mkombozi mkubwa katika kumkomboa mkulima. Kwenye korosho tumefanikiwa, kwenye ufuta tumefanikiwa na sasa tunaomba Serikali, kuna maeneo tunateleza kwenye mazao mchanganyiko. Kwa mfano, choroko, uzalishaji ni mdogo sana. Naamini kama tungeacha kununua choroko kwa mtindo holela, mapato yangekuwa ni makubwa kwa wakulima, lakini tunapopeleka choroko kwenye mfumo wa stakabadhi ghalani na choroko zenyewe ni chache, kwa kweli inaleta kero. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati huo huo haya mazao madogo madogo basi tuyaangalie kiukanda. Kama mbaazi, stakabadhi ghalani inafanyika Tunduru, basi hata wenzetu wa Mtwara, Nanyumbu na Masasi wafanye stakabadhi ghalani. Hii inasababisha mbaazi za Tunduru kwenda Nanyumbu na kuinyima mapato Halmashauri ya Tunduru. Kwa hiyo, stakabadhi kwa sababu ni sheria, naamini kwenye maeneo ambayo wamekubali hii sheria, iendelee kutumika basi kwenye mazao yote, itumike kwenye mfumo wa stakabadhi ghalani ili kila mmoja aone wanakwenda sambamba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo ningependa sana kulizungumzia ni tembo. Naomba sana, Waziri wa Maliasili simwoni; Tunduru tembo wamekuwa wengi sasa. Kipindi hiki ni cha mavuno ya wakulima, tembo saa hizi ndiyo wanashamiri, watu hawalali.

Tunaiomba Serikali kama walivyotoa ahadi siku za nyuma, pelekeni vikosi vya dharura katika maeneo ya Tunduru, tuna shida sana Mbati, leo hii wameingia kwenye nyumba za watu. Tuna shida Mpanji, Misyaje, Marumba, Imani na Kazamoyo. Tembo wamekuwa ni wengi na wale wanatokea sehemu ya Msumbiji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba sana Serikali iangalie kwa jicho la huruma, mazao ya wananchi wa Tunduru yanateketea kwa tembo, yanaliwa. Naomba tupeleke askari wa dharura ili waweze kudhibiti wale tembo wasiendelee kudhuru mazao ya wananchi na wananchi wenyewe wanadhurika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni suala la afya. Kwenye Jimbo langu kuna vituo vya afya vitatu. Naishukuru Serikali, Halmashauri ya Wilaya inajenga kituo kingine pale Nalasi na Serikali kupitia fedha zilizotolewa na Mheshimiwa Rais, tumepata shilingi milioni 250. Tunajenga kituo kingine cha afya katika Tarafa ya Lukumbule, lakini tuna kituo cha afya cha muda mrefu, kimejengwa tangu miaka ya 1980, majengo yake yamechakaa, hakuna operation inayofanyika, hakuna chochote zaidi ya yale majengo ambayo yapo mpaka sasa. Naomba sana Halmashauri… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)