Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Innocent Edward Kalogeris

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na mimi nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja ambayo iko mbele yetu. Nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mama yetu Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa ambayo anaitenda akiwa kama Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Nakumbuka katika Bunge lililopita nilisema kwamba mama huyu anatosha, na ni kielelezo tosha kwamba tumeshuhudia utendaji wake wa kazi uliotukuka. Sasa hivi majimboni mambo mazuri, sisi Wabunge tuko vizuri tukiamini kabisa kwamba utendaji wake wa kazi unatusaidia katika kutekeleza majukumu yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi kubwa ambayo anaitenda ndani na nje ya Bunge, akiwa kama Mtendaji Mkuu wa shughuli za Serikali katika utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi. Na nimpongeze kwa bajeti nzuri ambayo ameileta imesheheni katika kila sehemu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaamini ikipita na tunaamini itapita, na kwamba italeta matokeo mazuri katika utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya chama changu.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya pongezi hizi nijikite moja kwa moja katika kuchangia hoja. Cha kwanza, nichangie hoja katika hotuba yake namba 57 ukurasa wa 33 ambayo inaonekana itakuwa mwarobaini wa migogoro ya wakulima na wafugaji. Tumeona hapa Serikali imepanga katika mwaka huu wa fedha kutengeneza mashamba darasa katika Wilaya ya Handeni na Longido. Niiombe Serikali, Mkoa wa Morogoro vile vile ni Mkoa ambao una migogoro mikubwa ya wakulima na wafugaji, lakini una ardhi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba katika mwaka ujao wa fedha au mwaka huu wa fedha wangeweka utaratibu wa kutengeneza mashamba darasa katika Mkoa mzima wa Morogoro na ikiwezekana Mkoa wa Pwani ili wale wafugaji wenyeji walioko pale wapate utaalamu wa kutengeneza haya mashamba darasa, ili wawe na utaratibu kwamba, Januari atalisha hapa, Februari atalisha hapa, Machi atalisha hapa, mpaka mwaka mzima unapita na kuacha kwenda kuzurura ovyo kuchunga na kuingia katika migogoro ya wakulima na wafugaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii kukupongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi kubwa ambayo uliifanya katika utunzaji wa mazingira Kitaifa katika Mbuga ya Ngorongoro. Ninaamini kabisa Ngorongoro ni urithi katika Taifa hili, kuendelea kuiachia watu wakaivamia, tutakuwa tunapoteza urithi huo, lakini kubwa zaidi tutapoteza fedha nyingi za kigeni ambazo zinasaidia katika kuendesha nchi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Waziri Mkuu katika hili alilolifanya kama Waziri Mkuu, na ninaamini alishirikiana na Wizara ya Maliasili na Utalii pamoja na Wizara ya Mazingira, sasa hivi tujielekeze katika kukabiliana na janga lingine la migogoro ya wakulima na wafugaji katika maeneo mbalimbali katika mkoa huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaamini kama tumeweza kupata hekta 500,000 ambazo Serikali imezipata Handeni, Tanzania bado ina maeneo makubwa ambayo tunaweza kwenda kuyapima na kuwapeleka wafugaji wakakaa huko wakanusuru mifugo yao katika kipindi cha kiangazi na tukaondokana na migogoro mikubwa ya wakulima ambayo haina sababu. Hili ni janga kubwa huko tuendako kama Serikali haitalisimamia na kulichukulia kwa umakini.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaamini Mheshimiwa Waziri Mkuu akiamua na timu yake; Wizara ya Mifugo, Wizara ya Ardhi, wanaweza waka-allocate maeneo mbalimbali katika Tanzania yetu kama vile tulivyofanya Handeni tukapeleka huko nako wafugaji wengine wakakaa wakajengewa miundombinu ya barabara, maji na nyumba. Leo hii tunaambiwa kwamba tumepata ardhi, tumepata nyumba na tayari 101 zimeshajengwa kati ya nyumba 300; visima vinne vimeshachimbwa kati ya visima 13. Naamini Serikali ikiamua inaweza. Naomba Mheshimiwa Waziri Mkuu kama watu walivyokuwa wanapiga kelele kwamba tunafanyaje katika kunusuru mifugo? Tunafanyaje katika kuondoa migogoro ya wakulima na wafugaji? Naamini kama hii Serikali itashughulikia hili, itakuwa imetusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nikwambie, kuwaachia Wakuu wa Wilaya na Wakuu wa Mikoa kushughulikia migogoro ya wakulima na wafugaji, haitawezekana kabisa kwa sababu hili tayari limeshakuwa janga kubwa na hawana uwezo nalo. Kinachotokea sasa hivi, tutakuja kufika mahali tutagombana kati ya wachuguliwa na watendaji wa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nije katika suala la barabara. Tumefanya mambo mengi, naipongeza Serikali yangu kwa kazi kubwa iliyoifanya. Kuna suala la TARURA, tulipata shilingi bilioni 1.5. Naomba na ninaielekeza Serikali, ikiwezekaa TARURA waongezewe fedha ili waweze kujenga madaraja huko vijijini. Kwa baadaye, naiomba Serikali ikiwezekana kuwe na special program kwa majimbo na wilaya zilizokuwa pembezoni ili ziongezewe fedha zaidi katika kutekeleza majukumu yake ya kutengeneza barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile naipongeza Serikali kwa suala la TANROADS. Tumepata lami katika Barabara ya Bigwa – Kisaki yenye kilometa 15, tunasubiri mkandarasi tu, muda wowote aanze kazi. Pia kuna barabara yenye kilometa
63 kutoka Kiloka kwenda Mvuha, tayari tunatarajia kuitangaza. Ombi langu kwa Serikali, barabara ya Bigwa – Kisaki yenye kilometa 140 kwenye mradi wa umeme, lakini vilevile kwenye hifadhi ya Mwalimu Nyerere, ni hifadhi ambayo utalii wake utaweza kuwa mkubwa kama tukifika katika kilometa zilizobakia 40. Naiomba Serikali kushughulikia hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali katika suala la afya. Wilaya ya Morogoro Vijijini, hospitali yao imekamilika; vituo vya afya, sita vipo; changamoto zetu, nianze na kimkoa. Mheshimiwa Mbunge wa Morogoro Mjini amezungumzia Hospitali ya Rufaa ya Mkoa; Morogoro ni katikati, lakini hakuna Hospitali ya Rufaa, tuna Hospitali ya Mkoa. Tunaiomba Serikali itujengee Hospitali ya Rufaa Mkoa wa Morogoro ili tuweze kunusuru maisha ya watu katika ajali za barabarani zinazotokea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile tuna changamoto ya uhitaji wa vifaa tiba na dawa na majengo ya OPD katika Halmashauri ya Morogoro vijijini…

(Hapa, kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante Mheshimiwa kwa mchango mzuri wa Morogoro na maeneo mengine.

MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)