Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Shamsi Vuai Nahodha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. SHAMSI VUAI NAHODHA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii ya kuwa mchangiaji wa mwanzo katika Wizara hii, Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa.
Mheshimiwa Spika, majeshi ya ulinzi yana mchango mkubwa sana siyo katika kudumisha amani tu na usalama lakini katika kukuza uchumi, maendeleo na ustawi wa nchi. Nchi ambazo zimefanikiwa sana katika kuleta maendeleo ya watu wao wameyatumia vizuri sana majeshi yao ya ulinzi, mfano mzuri nchi kama Marekani, China na India walifanya uamuzi mahsusi wa kujinyima na kuwekeza kwenye masuala ya uzalishaji hasa mashirika ya uzalishaji yanayoongozwa na Jeshi. Matokeo yake basi masuala ya utafiti wa mambo muhimu sana wa mataifa hayo yanayohusiana na uchumi, tiba na elimu yamefanywa na wanajeshi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, najua Tanzania na hasa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa bajeti wanayopewa ni ndogo sana, lakini kutokana na dhamira aliyoionesha Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na tunakumbuka hivi karibuni alisema anatamani sana Jeshi la Ulinzi lifanye kazi zinazohusiana na masuala ya uzalishaji kwa kadri inavyowezekana. Kwa maana hiyo basi, tunaiomba Serikali ili tuweze kutimiza dhamira hiyo ya Mheshimiwa Rais tujinyime, lakini tufanye kila lililo katika uwezo wetu kuwekeza katika jambo hilo.
Mheshimiwa Spika, Jeshi la Ulinzi wa Tanzania lina uwezo mkubwa sana wa kufanya shughuli ambazo hivi sasa katika nchi yetu zinafanywa na makampuni ya watu binafsi na wakati mwingine makampuni yanayotoka nje ya nchi. Sisi tunajua Jeshi letu la Ulinzi lina uwezo mkubwa sana wa kutengeneza madaraja, kuweka njia kubwa za umeme.
Mheshimiwa Spika, huwa ninasikitika sana ninapoona ziko shughuli ambazo Jeshi la Wananchi wa Tanzania wanaweza kuzifanya vizuri tena kwa weledi mkubwa lakini wanapewa watu binafsi. Wakati mwingine tunafanya jambo la hatari sana kiulinzi na usalama, nitatoa mfano.
Mheshimiwa Spika, niliwahi kutembelea nchi moja lakini sitaitaja Ulaya tukawa tunaangalia na wale wenyeji nikawauliza mbona barabara zenu ziko hivi pana sana, akaniambia hamjui sisi likitokea la kutokea nchi ikiingia kwa mfano kwenye vita barabara hizi zinafungwa na zinageuka kuwa njia za kupitia ndege za kijeshi.
Mheshimiwa Spika, sasa sisemi tunaweza tukafikia huko, lakini inasikitisha utakuta kampuni ya ujenzi kutoka nje inakuja katika nchi yetu inajenga barabara na madaraja Jeshi la Wananchi wa Tanzania halishirikishwi, halijui! Hatari yake kiulinzi na usalama ikitokea hali ya hatari kuna baadhi ya madaraja hata vifaru haviwezi kupita. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, wakati mwingine njia hizi za umeme tunawapa kazi makampuni kutoka nje yanaweka njia kubwa za umeme jambo ambalo ni hatari sana, Jeshi la Ulinzi na wataalam wake hawashirikishwi, mimi nasema hili ni jambo la hatari sana. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, jambo la tatu ambalo Jeshi wanaweza kutoa mchango mkubwa iwapo watapewa fedha za kutosha. Wanajeshi wetu wapo na tunao wataalam kidogo katika masuala ya teknolojia ya habari na napenda kusema katika dunia ya leo, nafasi ya Jeshi kutumia silaha kubwa kama vifaru kwenda kwenye vita naiona katika karne hii na karne inayokuja inaweza ikapungua sana, lakini karne itakayokuja kuna uwezekano mkubwa sana wa mataifa mbalimbali watatumia cyber katika kuzishambulia nchi wanazotaka kuzishambulia na kwa maana hiyo Jeshi letu lijiandae kwenye eneo hilo. Ndiyo maana nasema Serikali ifanye kila linalowezekana iisaidie Wizara ya Ulinzi kuhakikisha kwamba wataalam wetu wa jeshi wanafunzwa ipasavyo katika masuala ya teknolojia ya habari na cyber kwa ujumla wake. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, najua tutasema hatuna fedha labda nitoe ushauri kidogo wa namna ya kupata fedha. Najua bajeti hii haitoshi, lakini zipo Wizara ambazo zinaweza kufanya maamuzi ya makusudi kabisa kuunga mkono shughuli ambazo zinafanywa na Jeshi kwa sababu shughuli zao pia zinasaidiwa na Jeshi. Kwa mfano, Wizara ya Biashara na Viwanda washirikiane na Jeshi, Wizara ya Elimu, Sayansi, Ufundi na Teknolojia ishirikiane na Jeshi, isishirikiane tu kwa maneno, hata inapowezekana watoe fedha kulisaidia Jeshi. Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ishirikiane na Wizara ya Ulinzi na kila inapowezekana wanaweza kutoa fedha katika kuunga mkono miradi ambayo inatekelezwa na Jeshi letu la Wananchi wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho ninalotaka kuchangia ni kwamba kwa muda mrefu vijana wetu wamekuwa wakipewa mafunzo katika Jeshi la Kujenga Taifa, lakini vijana hawa baada ya muda wao wa kujitolea unapomalizika wanarudi kwenye mitaa. Hili ni jambo la hatari. Vijana hawa tayari tumeshawapa mafunzo ya kijeshi na kwa bahati mbaya sana hatuna utaratibu wa kufanya tathmini wanaporudi uraiani vijana hawa wanafanya nini. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nadhani sasa wakati umefika kwa Wizara ya Ulinzi kwanza ifanye utafiti na tathmini vijana hawa wanaporudi uraiani wanafanya nini. Lakini la pili Wizara iweke taarifa maalum ya vijana waliopitia Jeshi la Kujenga Taifa ili zikitokea nafasi katika Halmashauri zetu za kazi za ufundi, kazi za vibarua wanaangalia vijana wetu ambao wamepitia kwenye Jeshi la Kujenga Taifa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, mwisho, najua tuna ukosefu wa fedha lakini nadhani wakati umefika wa kuviimarisha vyuo vya ufundi vilivyopo katika Jeshi la Kujenga Taifa ili viweze kutoa mafunzo mazuri kwa vijana wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Nakushukuru sana.