Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Khalifa Mohammed Issa

Sex

Male

Party

ACT

Constituent

Mtambwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. KHALIFA MOHAMED ISSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Awali ya yote namshukuru Mwenye Mungu Mtukufu kwa kutujalia uzima na afya katika mwezi huu Mtukufu wa Ramadhan na kuweza kutekeleza nguzo hii muhimu katika dini ya Uislam. Pia nakushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia mchana huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba hii haiwezi kupita bure kama sikumshukuru sana Mama yetu Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mheshimiwa Samia kwa kweli amekijaa kiti chake na amekuwa ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania bila kujali siasa, itikadi za vyama, wapinzani na chama Tawala. Kwa hiyo, Mheshimiwa anakusudia, na ni dhamira ambayo tunaiona wazi kabisa ya kuliunganisha Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli sasa nimekuwa mshabiki wake mkubwa wa kusikiliza hotuba zake. Ninafuatilia ratiba zake, nafuatilia hotuba zake. Hotuba zake zote zinaonesha anataka kuiunganisha nchi, na anazungumzia utengamano wa wananchi wote bila kujali itikadi zao. Hivyo basi, mfano mkubwa katika kipindi kifupi cha mwaka mmoja hiki, Mheshimiwa Rais ameshakutana na viongozi wa vyama vya upinzani. Pia karibuni hivi, alikuwa katika Mkutano wa TSD; karibuni pia alikuwa akipokea taarifa ya kikosi kazi ambacho amekiunda na ameyakaribisha mapendekezo yote kwa mikono miwili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba wasaidizi wake wasimwangushe. Nia njema hii ambayo Mheshimiwa Rais ameionesha ya kuliunganisha Taifa, basi taifa hili ni letu sote, tuna tofauti ya mawazo yaheshimiwe, naye ndiyo mwelekeo anakwenda nao. Kwa hiyo, ningetoa tena wito kwa wasaidizi wake Mawaziri, wamsaidie kutufikisha pale ambapo tunataka. Tuna mambo mengi kwa sababu mapendekezo yanakusanywa, anapelekewa. Sina haja ya kwenda huko, najua kuna muda mfupi wa kutekeleza mambo, kuna muda wa kati na kuna muda mrefu. Kwa hiyo, tuwaachie mambo haya yachakatwe yapelekwe ili yatolewe maamuzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuondoka hapo, nami nipate fursa ya kuzungumzia hali ya maisha ya wananchi kwa ujumla. Kwa kweli hili halitaki tochi, halitaki taa ya mwangaza mkali wa kuona hali halisi ya maisha ya wananchi wetu. Kwa kweli purchasing power ya wananchi imepungua sana kwa sababu mifumuko hii ya bei ya vitu mbalimbali na upandaji wa mafuta.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimefanya utafiti mdogo katika masoko yetu haya hapa Dodoma ambapo mahitaji yetu mengi tunakwenda kuchukua. Utavikuta vitu vipo kwa wingi sana katika masoko; ukitaka vyakula vya maganda hivi, mboga mboga, matunda na bidhaa nyingine, lakini ukimwuliza muuzaji, atakwambia unaweza ukakaa kutwa nzima ukauza shilingi 2,000/= au shlingi 3,000/=. Watu wanavitaka vitu, lakini bei ni kubwa na mifukoni kunakuwa hamna kitu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hili jambo ni la kuzingatiwa mno. Biongozi wetu na wataalam wetu wakae waone kwa namna gani watamnusuru huyu mwananchi hasa wa kipato cha chini kuweza kumudu maisha yake na kipato chake na chakula chake walau cha siku nzima.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikitoka hapo nizungumzie hali ya UKIMWI katika nchi, kwa sababu mimi ni Mjumbe wa Kamati yako ya Mambo ya UKIMWI, Dawa za Kulevya, Magonjwa yasiyoambukiza pamoja na TB. Kwa kweli hali ya UKIMWI katika nchi yetu, bado UKIMWI upo katika nchi na wananchi waelewe UKIMWI bado ndio ule ule unaua. Kwa hiyo, ipo haja ya Serikali, wananchi na jamii kwa jumla kuweza kupiga vita hivi ili tuweze kuvishinda walau tumudu kutokupata maambukizi mapya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu inakisiwa tu, na mpaka takwimu za Desemba, 2020 tuna watu ambao wanaishi na virusi vya UKIMWI karibia 1,700,000, ingawa ukiangalia trend ile toka miaka ya 2004 huko mpaka sasa, ile graph linakuwa declined, linapungua pungua yale maambukizi mapya.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo kuna rika muhimu kweli kweli ambalo linapata maambukizi mapya. Hili ni group la vijana wetu ambao wana umri kuanzia miaka 15 mpaka 24. Vijana hawa wanachangia asilimia 40 ya watu wote ambao wana maambukizi. Katika vijana ambao wana umri huo, vijana wa kike kwa asilimia 80 katika maambukizi hayo, wao wanaongoza vijana wasichana; na hao wasichana katika group hili ndio ambao wapo katika vyuo vikuu, wapo katika Shule za Sekondari nakadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, wasichana hawa ndio target kubwa ya wanaume wakwera, Mheshimiwa Mwenyekiti wangu wa Kamati ya UKIMWI ana neno lake analitumia kwa hawa wanaume ambao wanawanyemelea vijana hawa. Ukiangalia, ni dhahiri kwamba hata hapa Dodoma ukifuata nyendo fulani fulani hivi unaweza kuona vijana hawa wadogo ndio ambao wameingia katika ushawishi huu mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, wajumbe wenzangu wa kamati hii ya mambo ya UKIMWI tulipokuwa katika ziara ya kukagua maendeleo, tulikuwa katika mkoa mmoja huko sitaki niutaje, lakini walipokwenda kufanya utafiti katika maeneo yao, walikaribishwa pale. Ajabu ni kwamba, unapewa option; walipofika wakapewa option, kama unataka kula ndizi na ganda lake au unataka ule ndizi ganda ukiwa umelitoa? Kwa hiyo, kuna viwango; ukitaka ule na ganda lake, basi ni shilingi 10,000/=, lakini ukitaka ulitoe lile ganda, basi kuna shilingi 15,000/=. Kwa hiyo, hii ni hatari ambayo Serikali pamoja na jamii na wazee, lazima tushirikiane tuwalinde vijana hawa. Hawa vijana ni wetu na kwa kweli tusi… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Hiyo ya pili, malizia sekunde moja.

MHE. KHALIFA MOHAMED ISSA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kwa ufupi mimi niseme tu kwamba kuna magonjwa haya yasiyo ya kuambukiza pia, ni janga, kwa hiyo…

NAIBU SPIKA: Ahsante.