Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Abdulhafar Idrissa Juma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtoni

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. ABDUL-HAFAR IDRISSA JUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuzungumza katika Bunge siku ya leo kuchangia bajeti hii ya Ofisi ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuipongeza bajeti hii. Bajeti hii imeakisi mwelekeo wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi na inavyokwenda kutekelezeka kabla ya mwaka 2025. Ilani yetu imeelekeza kuendelea kutafuta ahueni katika kila nyanja katika Taifa letu. Yale ambayo yamesemwa na Waziri Mkuu, kuanzia yale yaliyotekelezwa na yale ambayo yamepangwa kutekelezwa katika bajeti hii, sina mashaka yoyote chini ya Mama Samia, mwaka 2025 Ilani ya Chama cha Mapinduzi itakuwa imetekelezeka sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kuyasema hayo, yaliyozungumzwa katika bajeti hii, naomba nichangie kuhusiana suala la TASAF. Katika Jimbo langu la Mtoni, mimi ni mnufaika wa TASAF katika Shehia zote. Hivi karibuni Shehia mbili ambazo zilikuwa hazipo; Shehia ya Kwagoa na Shehia ya Sharifu Mussa zimeingizwa katika mradi huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda niishauri Serikali. Zipo changamoto katika kupata wanufaika wa TASAF katika maeneo yetu kwa sababu ya kijiografia. Umaskini wa Zanzibar haufanani na umasikini wa mtu wa Kigoma. Umaskini wa Zanzibar haufanani na umasikini wa Tanga na maeneo mengine. Umasikini unapishana kutokana na mazingira.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa wasaidizi wetu katika TASAF kama watatafsiri mtu kumiliki tv ya chogo kule Zanzibar hafai kuwa katika TASAF, wanaweza wakakuta Wazanzibar wengi hawana sifa hiyo, lakini ni watu masikini ambao wanastahiki kusaidiwa na Mfuko wa TASAF. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika jimbo langu, japo mchakato wa rufaa za TASAF unaendelea, lakini wapo ambao wameenguliwa kwa sababu vyoo vyao wamekuta kuna masinki.

Mheshimiwa Naibu Spika, labda niwakumbushe wenzetu, sisi kule Zanzibar unaweza ukanunua TV mpya, badala ya kuuza TV uliyokuwa nayo ukamgawia mtu ambaye unadhani anastahiki kugawiwa. Sasa mimi niwakumbushe wenzetu, umasikini huu unapishana. Nashauri wenzetu katika TASAF, wakiwa wanafanya tathmini ya kutafuta watu wenye kustahiki kusaidiwa na mfuko huu wa TASAF, waugawe umasikini kutokana na mazingira yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kwetu Zanzibar hatulimi. Ukimkuta mtu masikini hasa katika jimbo langu ni masikini kweli kweli, anahitaji msaada wa Serikali. Hatuna ardhi ya kulima, jimbo langu kwa ardhi ni ndogo. Ukikuta hana uwezo wa kufanya biashara, huyo anastahiki na TASAF.

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kushauri kwamba pamoja na mambo mazuri, wamechukuliwa baadhi yao, wanaendelea kupewa na wananufaika na msaada huu wa TASAF lakini mgawanyo wa masuala ya kuutafsiri umasikini, watafsiri umasikini kwa mazingira yake. Mazingira yanatofautisha umasikini wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda pia nizungumzie suala la UKIMWI katika bajeti ya Waziri Mkuu. Kwanza naipongeza Serikali yetu chini ya Mheshimiwa Mama Samia, wameendelea kuhakikisha upatikanaji wa ARV nchi nzima. Mimi ni Mjumbe wa Kamati inayoshughulikia masuala ya UKIMWI, hakuna mahali tulipokwenda tumekuwa ARV hazipatikani, zinapatikana kwa asilimia 100.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda katika bajeti hii tuendelee kuiboresha tuhakikishe zinapatikana mashine za kupima viral load katika maeneo yale ambayo yanatoa huduma CTC. Ili kupima ufanisi wa ARV katika mwili wa mtu ambaye anatumia vidonge hivi, ni lazima tupime virusi kwa kutumia viral load.

Mheshimiwa Naibu Spika, yapo maeneo tumeyaona hayana mashine zenye uwezo wa kupima viral load. Katika bajeti hii ya Waziri Mkuu, mambo yake mazuri sana, lakini yaongeze nyama kwa kuhakikisha mashine za viral load zinapatikana. Tunatambua Tanzania wapo waathirika wa virusi vya UKIMWI takribani milioni 1.7, sasa kwa nini tusihakikishe tunakuwa na viral load zitakazowafanya wasihame kutoka eneo moja kwenda eneo lingine ili kupata huduma hii kwa ajili ya kusaidia wananchi wetu?

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu kwa dhamira ya kuongeza bajeti katika fungu la maendeleo kwa fedha za ndani. Hata hivyo naomba dhamira hii iendane na kutekelezwa. Mwaka wa fedha unaokwisha huu walitenge shilingi bilioni moja, mwaka huu wametenga shilingi 1,880,000,000, lakini shilingi bilioni moja iliyopita, changamoto ipo, hazijatoka zote. Sasa dhamira ni nzuri ya kuongeza bajeti, lakini dhamira iende ikatekelezeke ili wenzetu wa Tume ya Taifa ya Kupambana na Virusi vya UKIMWI wawe na uwezo wa kuhakikisha tunafikia zile 95 tano kufikia mwaka 2030. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimalizie kwa kuzungumzia maradhi yasiyoambukiza. Nashauri tena jambo hili kupitia bajeti ya Waziri Mkuu. Maradhi yasiyoambukiza kwa sasa ndiyo yanayoongoza kuua Watanzania. Maradhi yasiyoambukiza ndiyo maradhi ambayo yanafilisi familia zetu, maradhi yasiyoambukiza ndiyo yanayoleta unyonge kwa ndugu zetu. Sasa basi, ninaishauri sana Serikali yetu ione tunavyoweza kuanzisha Tume ya Kupambana na Maradhi Yasiyoambukiza kama ambavyo tumeanzisha Tume ya UKIMWI.

Mheshimiwa Naibu Spika, shilingi ngapi tunazipoteza kila siku kuhakikisha watu wenye maradhi ya figo wanasafishwa damu. Shilingi ngapi zinapotea kila siku watu kwa ajili ya kuchukua vidongo vya pressure? Maradhi yasiyoambukiza ni tabia zetu tu, namna tunavyoishi, namna tunavyokaa muda mrefu na kupigwa na viyoyozi mrefu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukiweza kuanzisha Tume inaleta hamasa na kuleta uelewa mkubwa kama Tume ya Kupambana na UKIMWI. Leo wote humu ndani tunajua namna gani virusi ya UKIMWI vinaambukizwa, lakini tukibainika tuna virusi vya UKIMWI, tuna amani na tunatumaini kwa sababu tunajua Serikali imeandaa dawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba Tume hii ianzishwe ili kuongeza hamasa na kutambua maradhi yasiyoambukiza.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya haya, naunga mkono hoja hii. Nashukuru sana (Makofi)