Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

Hon. Jerry William Silaa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukonga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

MHE. JERRY W. SILAA - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA UWEKEZAJI WA MITAJI YA UMMA: Mheshimiwa Spika, awali ya yote niungane na wenzangu kukushukuru na kukupongeza wewe binafsi kwa kutoa muda wa kutosha wa ripoti za Kamati hizi tatu, kujadiliwa na Bunge kwa kipindi cha siku nne, tunakupongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili, niwashukuru sana Wabunge kwa michango yao. Tumepata michango ya jumla ya Wabunge 83. Katika hao Wabunge 19 wamechangia hoja mahususi ya Kamati ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma tokea Novemba mpaka leo. ukiondoa waliochangia Taarifa ya Hesabu za Serikali Kuu na Serikali za Mitaa pekee, wachangiaji Taarifa ya PAC waliyagusa mashirika ya umma.

Mheshimiwa Spika, wakati nawasilisha Taarifa ya Kamati, Kamati ilikuwa na mapendekezo nane, baada ya majadiliano Kamati imeboresha mapendekezo kwa michango ya Waheshimiwa Wabunge jumla ya mapendekezo matano hivyo kupelekea jumla ya mapendekezo kufika 13.

Mheshimiwa Spika, pamoja na majukumu ya Kamati yetu ya PIC ya kuangalia ufanisi na tija ya uwekezaji na pamoja kwamba ripoti za ukaguzi zinawasilishwa ila tunazitumia tu kwa ajili ya kukokotoa vigezo vya uwekezaji. Wenzetu wa PAC wana majukumu ya hoja za ukaguzi wa mashirika ya umma.

Mheshimiwa Spika, katika michango ya Waheshimiwa Wabunge, mashirika yafuatayo ambayo tunayasimamia uwekezaji wake, yametajwa na yameonekana yana hoja za ukaguzi wa mabilioni ya shilingi. Mashirika hayo ni pamoja na NHIF, TRA, DART, KADCO, TANROADS, MSD, TPA, TRC, TAMESA, GPSA, Bodi ya Mikopo, Ngorongoro Conservation, REA, DUWASA na TANESCO. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni dhahiri hoja za ukaguzi kwenye ripoti ya CAG ya mwaka wa fedha 2020/2021 ndio yamepelekea kutofikia lengo la makusanyo ya Msajili wa Hazina kwa maana katika lengo la kukusanya gawio la shilingi bilioni 308.82 sawa na asilimia 75 ya lengo ilikusanywa. Katika michango ya asilimia 15 ya mapato ghafi, ni jumla ya shilingi bilioni 202.2 tu sawa na asilimia 51 ya lengo ilikusanywa. Kama mashirika haya yangesimamia fedha vizuri, basi wangeokoa fedha za walipakodi, faida ingeongezeka na mchango kwenye Mfuko Mkuu wa Taifa ungeongezeka.

Mheshimiwa Spika, kabla ya kusoma maoni na mapendekezo ya maazimio ya Kamati, naomba kuzungumzia mambo mawili ambayo yamechangiwa sana na Waheshimiwa Wabunge, ili kama yataboreshwa inawezekana ile mianya ya uvujaji wa mapato, katika hela za umma na matumizi yasiyo ya lazima yanaweza kufikiwa. Maeneo hayo mawili la kwanza ni la mifumo. Wachangiaji wengi wamechangia mifumo mbalimbali na kwenye mifumo nimeona kuna maeneo mawili. Kwanza mifumo mingi ni dhaifu, utasikia POS inaongezwa muda fedha zinafutwa, labda GPSA wanakuwa hawana mifumo mizuri ya uwagizaji, TANePS haijibu majibu ya manunuzi. Kwa hiyo mifumo mingi iliyopo kwenye nchi yetu ni dhaifu.

Mheshimiwa Spika, mifumo inakuwa dhaifu kwa mambo mawili tu, moja, aidha, inapewa udhaifu kwa makusudi katika kutengeneza mianya ya upigaji wa fedha za umma. Kwa sababu mfumo unapokuwa madhubuti kama ilivyo mifumo yetu ya miamala ya simu, sijawahi kumsikia hata Mheshimiwa mmoja huku anasema hela zake zilizopo kwenye miamala ya simu zimepotea, zimevuja, zimefutwa au salio halionekani. Kwa hiyo mifumo inapokuwa dhaifu inawezekana ni kwa makusudi katika kutengeneza utaratibu wa uvujifu wa mapato na matumizi ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, eneo la pili, tuliwahi kulizungumza hapa Bungeni, ni Serikali kushindwa kufika mwisho wa mambo mawili. Moja, ni ujengaji wa mfumo wa public infrastructure kwa maana ya PKI ambao ndio mfumo unaweza kusaidia authentication ya transactions zote za kieletroniki kwenye mifumo hii ya mapato na matumizi.

Mheshimiwa Spika, la pili, kutokuwa na centralize ledger, kwa sababu ukisikia hapa kuna mtumishi ana malimbikizo ya mshahara na kuna mtumishi amestaafu amelipwa na kuna mapato yamekusanywa ghafi yameliwa, maana yake hakuna sehemu ya pamoja ambapo Taifa la Tanzania, nchi yetu, tunakuwa na centralized system ambayo inaweza kuona, vitendo kama hivi havifikiwi na kama vinafikiwa vinaweza kuonekana ni nani kafanya nini na lini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimesema niyaseme haya kwa utangulizi kwenye mifumo na tutakuwa na maazimio mahususi. La pili, ni Bodi za Wakurugenzi. Nadhani nilichangia pale nyuma siyo vyema kwa kuokoa muda, lakini Kamati inaomba kidhati kumpongeza Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, kwa nia yake na vitendo vyake ambavyo anaonyesha wazi, anaunga mkono si tu uwekezaji kwenye mashirika ya umma lakini sekta nzima ya uwekezaji kwenye Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, pale awali nilieleza kwamba kwenye uteuzi wa bodi Mheshimiwa Rais amewahi kunukuliwa hadharani akieleza ni jinsi gani anatimiza wajibu wake pale tu anapopelekewa uteuzi wa bodi. Kama nilivyoeleza pale awali jumla ya mashirika 23 kufikia Octoba 31, yalikuwa yana bodi zilizomaliza muda wake na hazijateuliwa. Kwa kudhibitisha kauli ile ya Mheshimiwa Rais, yako mashirika 12 yaliyopo kwenye Wizara tisa (9) ambayo tayari Mheshimiwa Rais ameshateua Wenyeviti wa Bodi na Wajumbe ambao ni mamlaka ya uteuzi wa Wizara kuteua, hawajateuliwa.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo, naomba kutoa mapendekezo 13 na kati ya hayo kama nilivyosema pale awali nane yalipendekezwa na Kamati na matano yametokana na michango ya Waheshimiwa Wabunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, moja, Taasisi kutokuwa na bodi za wakurugenzi kwa muda mrefu kutokana na kuchelewa kuteuliwa kwa Wajumbe wa Bodi:-

KWA KUWA mashirika mengi yanayotumia mitaji ya umma yameendeshwa bila kuwa na Bodi za Wakurugenzi kutokana na bodi zilizokuwepo kumaliza muda wake;

NA KWA KUWA hadi sasa kuna taasisi na mashirika 12 ambayo yana Wenyeviti wa Bodi na bila wajumbe na taasisi za mashirika 23 ambayo hayana kabisa Wenyeviti wala Wajumbe wa Bodi, jambo ambalo ni ukiukwaji wa misingi ya utawala bora katika uwekezaji wa mitaji ya umma na kwamba ni jambo linalokwamisha upatikanaji wa tija uwekezaji unaofanywa na Serikali;

KWA HIYO BASI Bunge linaazimia kwamba: -

(a) Serikali ikamilishe uteuzi wa wajumbe wa Bodi 12 kwenye Wizara tisa ambazo Mheshimiwa Rais ameshateua Wenyeviti ndani ya miezi 3. (Makofi)

(b) Serikali ikamilishe uteuzi wa Wajumbe wa Bodi 23 kwenye Wizara 12 ambazo hazina bodi ndani ya miezi sita.

(c) Serikali ihakikishe inatimiza utaratibu wa kuanza maandalizi ya uteuzi wa bodi miezi tisa kabla bodi hazijamaliza muda wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mbili, changamoto ya kupata vibali vya kuajiri: -

KWA KUWA mashirika ya umma yanayojiendesha kibiashara yanakabiliwa na changamoto ya upungufu wa watumishi katika kujiendesha kwake kutokana na kutegemea mchakato wa ajira unaoendeshwa na Sekretarieti ya Ajira ya Utumishi wa Umma katika kupata watumishi;

NA KWA KUWA changamoto hiyo inaathiri tija ya uwekezaji na manufaa yaliyotarajiwa kupatikana kutokana na kukosa watumishi wanaostahili kwa wakati, hata pale ambapo Shirika la Umma linakuwa na uwezo wa mapato wa kuwalipa mishahara;

KWA HIYO BASI Bunge linaazimia kwamba Serikali iweke utaratibu maalum wa kutoa vibali kwa taasisi zinazojiendesha kibiashara ili ziweze kuajiri zenyewe ajira ya moja kwa moja na kuweza kuendana na soko la ushindani kibiashara.

Mheshimiwa Spika, tatu, uwezo wa SGR kuzidi uwezo wa Bandari ya Dar es Salaam: -

KWA KUWA Bandari ya Dar es Salaam ina uwezo mdogo wa kupokea mizigo kulinganisha na uwezo wa SGR iliyoigharimu Serikali kwa uwekezaji mkubwa ilihali bandari hiyo ndio chanzo kikuu cha mizigo. Hii itachangia SGR isipate mzigo wa kutosha kwa ajili ya kusafirishwa pindi itakapokamilika;

NA KWA KUWA changamoto ya SGR kutopata mzigo wa kutosha kusafirishwa ni jambo linalokwamisha kupatikana kwa tija ya uwekezaji uliofanyika na kwamba mkwamo huo unaweza kutatuliwa kwa kuongeza Bandari ya Dar es Salaam na kujenga Bandari ya Bagamoyo;

KWA HIYO BASI Bunge linaazimia kwamba: -

(a) Serikali iharakishe utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo.

(b) Serikali iharakishe zoezi la kuongeza ufanisi wa Bandari ya Dar es Salaam ikiwa ni pamoja na kuongeza gati za kisasa katika Bandari ya Dar es Salaam na zoezi hilo likamilike kabla ya ujenzi wa reli ya SGR kukamilika. Hatua hii itasaidia SGR kupata mzigo wa kusafirisha na hivyo tija iliyokusudiwa kufikiwa.

Mheshimiwa Spika, nne, umuhimu wa Shirika la Maendeleo (NDC): -

KWA KUWA manufaa ya mradi wowote wa uwekezaji yanategemea kuanza kwa mradi lakini Mradi wa Mchuchuma na Liganga umechukua muda mrefu katika hatua za majadiliano ambayo kwa sasa yanaratibiwa na Kamati ya Majadiliano ya Serikalini (GNT);

NA KWA KUWA kutokukamilika kwa majadiliano hayo yanayoendelea kwa muda mrefu tangu kuanza kwake ni jambo linalochelewesha upatikanaji wa manufaa ya mradi huo;

KWA HIYO BASI Bunge linaazimia kwamba, Serikali ihakikishe kuwa mazungumzo yanayoendelea katika Kamati ya Majadiliano ya Serikali (GNT), yanafika mwisho ndani ya miezi mitatu au yapelekwe NDC, lengo ikiwa kuyamaliza na kupata tija inayokusudiwa katika miradi, kwa sababu Serikali imefanya mabadiliko makubwa katika taasisi hii ikiwemo kuipatia Bodi mpya ya Wakurugenzi pamoja na Menejimenti.

Mheshimiwa Spika, tano, mikopo chechefu (non- performing loans): -

KWA KUWA imebainika kuwa baadhi ya taasisi kama vile Benki ya Maendeleo (TIB) na Benki ya Biashara (TCB) zinakabiliwa na changamoto ya kuwa na kiasi kikubwa cha mikopo chechefu (non-performing loans);

NA KWA KUWA hali hiyo inaathiri mizania ya vitabu vya taasisi hizo jambo ambalo ni hatari kwa misingi ya kibiashara na uendeshaji wa taasisi zinazotumia mitaji ya umma;

KWA HIYO BASI Bunge linaazimia kwamba: -

(a) Serikali ifanye tathmini ya madeni hayo na kuhakikisha wanayaondoa kwenye vitabu vya benki hizo bila kuathiri ulipaji wa mikopo inayolipika (performing loans). Hatua hiyo itasaidia benki hizo kufanya kazi kwa ufanisi na kuleta tija inayokusudiwa.

(b) Serikali itengeneze mfumo fungamanishi kati ya Bodi ya Uhasibu (NBAA), Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), na Taasisi za Fedha na wafanyabiashara ili chanzo cha hesabu zote zinazotumiwa na wafanyabiashara kiwe kimoja. Hii itasaidia kukadiria kiwango halisi cha mkopo kinachoweza kulipika na mkopaji ili kupunguza mikopo chechefu.

Mheshimiwa Spika, sita, upungufu wa mtaji wa Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL):-

KWA KUWA Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL) inakabiliwa na changamoto ya mtaji hasi na changamoto ya uendeshaji wa biashara kutokana na utaratibu wa kukodisha ndege kutoka Wakala wa Ndege za Serikali (TGFA);

NA KWA KUWA utaratibu huo unaongeza madeni wanayodai yaani payables katika vitabu vya TGFA.

KWA HIYO BASI Bunge linaazimia kwamba, Wakala wa Ndege za Serikali Tanzania (TGFA) ikamilishe taratibu za kutekeleza agizo la Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, alipokuwa anapokea Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali tarehe 30 Machi, 2022 la kurudisha umiliki wa ndege kwa ATCL kwani ukiondoa tatizo hili ATCL ina uwezo wa kujiendesha kwa faida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, saba, kuiwezesha Benki ya Maendeleo ya Kilimo(TADB): -

KWA KUWA TADB ambayo ndio benki pekee inayohusika moja kwa moja na shughuli za kilimo, lakini haijapatiwa mtaji wa kutosha na kuendana na nia ya Serikali ya kuongeza tija kwenye kilimo, kuleta mageuzi ya kilimo na kulisaidia Taifa kufikia usalama wa chakula;

NA KWA KUWA pamoja na jitihada za Serikali kuipatia TADB kiasi cha shilingi milioni 208 mwaka 2021, bado kuna ahadi ya Serikali ambayo kama ingetekelezwa benki hii ingekuwa na mtaji wa jumla ya shilingi bilioni 760. Kutofikiwa kwa mtaji huu kunaathiri ufanisi na tija katika sekta ya kilimo;

KWA HIYO BASI Bunge linaazimia kwamba, Serikali itekeleze ahadi yake (commitment) waliyoitoa kwa TADB ya kuiongezea mtaji kiasi cha shilingi bilioni 100 kwa kila mwaka wa fedha, lengo likiwa ni kuongeza ufanisi katika sekta ya kilimo.

Mheshimiwa Spika, nane, kuathirika kwa kilimo cha pamba kutokana na maelekezo ya Serikali ya mwaka 2019 ya kuuza pamba kwa bei ya juu zaidi ya soko la dunia:-

KWA KUWA agizo la Serikali inayoitaka pamba kununuliwa kwa bei ya juu zaidi ya soko la dunia imeathiri uwezo wa wanunuzi wa pamba kwa kiasi cha shilingi bilioni 21.8, kiasi ambacho Serikali iliahidi kufidia deni hilo;

NA KWA KUWA deni hilo limeathiri taswira ya Bodi ya Pamba kwa wakulima na kuongeza changamoto katika biashara ya kilimo cha pamba;

KWA HIYO BASI Bunge linaazimia kwamba, Serikali iharakishe utekelezaji wa ahadi yake ya kulipa deni la pamba. Hatua hiyo itasaidia kuongeza ufanisi wa sekta hiyo na kurudisha taswira chanya ya Bodi ya Pamba.

Mheshimiwa Spika, tisa, mwingiliano wa majukumu kwa baadhi ya taasisi za umma:-

KWA KUWA mwaka 2017 Serikali iliamua majukumu ya Tanzania Air Port Authority ya kujenga viwanja vya ndege yahamie TANROADS;

NA KWA KUWA jambo hili ni kinyume cha viwango vya kimataifa na ni kinyume cha matakwa ya International Civil Aviation Organization (ICAO) ambayo Tanzania Air Port Authority ni mwanachama wake na ICAO inazitaka Mamlaka za Viwanja vya Ndege kusimamia shughuli zote za viwanja vya ndege ikiwemo ujenzi wa viwanja vyao;

KWA HIYO BASI Bunge linaazimia kwamba Serikali itekeleze haraka agizo la kurejesha jukumu la ujenzi wa viwanja vya ndege kwa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege (TAA) pamoja na rasilimali zake zote ikiwemo watumishi waliohama mwaka 2017. Hii ni muhimu kwa ajili ya kukidhi viwango vya kimataifa katika uendeshaji wa viwanja vya ndege. (Makofi)

(10) Matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA).

KWA KUWA, katika Mpango wa Tatu wa Maendeleo ya Taifa ya Miaka Mitano, Serikali inatekeleza mageuzi ya kidigitali yanayojumuisha teknolojia ya TEHAMA, kuwa nyenzo muhimu katika kuongeza ufanisi kwenye mifumo ya uzalishaji huduma na utawala;

NA KWA KUWA, mashirika mengi ya umma hayazingatii matumizi sahihi ya TEHAMA hali inayopelekea upotevu wa mapato na udanganyifu katika utoaji huduma zake;

KWA HIYO BASI, Bunge linaazimia kwamba: -

(a) Serikali ikamilishe mchakato wa public infrastructure (PKI)

(b) Serikali iunde mfumo wa taarifa ya pamoja (centralized ledger) kuondoa udanganyifu wa mifumo ya taasisi.

(c) Serikali ihakikishe inasimamia kikamilifu taasisi na mashirika ya umma kuimarisha mifumo ya TEHAMA. Hatua hizi zitasaidia kuongeza ufanisi wa utoaji huduma, ukusanyaji wa mapato, kupunguza matumizi yasiyo ya lazima na kudhibiti udanganyifu kwa lengo la kupata tija inayokusudiwa.

(11) Changamoto ya uendeshaji wa Kampuni ya Meli (Marine Services Company).

KWA KUWA, Kampuni ya Meli (MSC) iliyokuwa chini ya usimamizi wa Mamlaka ya Bandari kwa sasa imekuwa Kampuni huru inayojitegemea;

NA KWA KUWA, kitendo cha Mamlaka ya Bandari kuendelea kumiliki baadhi ya mali za (MSC) kunaathiri utendaji wa (MSC) ikiwa ni pamoja na uendeshaji wa mtaji wa umma uliowekwa (MSC);

KWA HIYO BASI, Bunge linaazimia kwamba Serikali iharakishe mali zote za (MSC) zilizopo Tanzania Port Authority zirejeshwe haraka sana (MSC) zikiwemo chelezo, karakana na nyinginezo.

(12) Matumizi ya TEHAMA katika Mfuko wa Taifa ya Bima ya Afya (NHIF).

KWA KUWA, Mfuko wa Bima ya Afya ya Taifa (NHIF) umeonesha udhaifu katika utoaji wa huduma zake jambo ambalo limepelekea Mfuko kupata hasara;

NA KWA KUWA, changamoto zilizojitokeza katika uendeshaji wa (NHIF) kwa kiasi kikubwa imetokana na kutokakuwa na mfumo thabiti wa TEHAMA inayotoa mianya ya kufanya udanganyifu kwa urahisi;

KWA HIYO BASI, Bunge linaazimia kwamba Serikali ihakikishe (NHIF) inaandaa mfumo madhubuti wa TEHAMA na kuanza kuutumia haraka iwezekanavyo kwa lengo la kuboresha utoaji wa huduma wa mfuko na kuziba mianya ya udanganyifu. (Makofi)

(13) Matumizi makubwa ya gharama za bima za Ndege kwa Shirika la Ndege la Taifa - ATCL.

KWA KUWA, Shirika la Taifa la ATCL linalazimika kununua Bima kutoka Shirika la Bima la Taifa (NIC) ambapo NIC ananunua Bima hizo kutoka kwa Wakala wa Nje ya Nchi kwa mfumo wa moja kwa moja single source;

NA KWA KUWA, changamoto zilizojitokeza ni kwa Shirika la Ndege kujikuta linanunua bima hizo kwa gharama kubwa hali inayopelekea kupunguza faida na tija kwa Shirika;

KWA HIYO BASI, Bunge linaazimia kwamba Serikali ielekeze ATCL na NIC kufanya zabuni shindanishi ili kupata wakala mwenye bei nafuu, huduma bora na ambaye atazingatia uwiano wa ndege, shirika anazomiliki, hii italeta ufanisi, tija na kupunguzia shirika gharama za matumizi.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, naafiki.