Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kupata nafasi hii muhimu sana kuweza kuchangia mada yetu iliyopo mezani.

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoifanya. Kazi anayofanya ni kubwa nasi Bunge tuendelee kumsaidia. Nichukue nafasi hii pia kuwapongeza Wenyeviti wa Kamati waliochakata taarifa hii hadi leo hii tunapojadili hapa kwenye Bunge hili kwa ajili ya kuweza kupata maamuzi na mwelekeo sahihi kwa Taarifa ya CAG.

Mheshimiwa Spika, nimpongeze pia sana CAG kwa sababu amefanya kazi kubwa. Taarifa yake ina zaidi ya kurasa 1,000. Ukipita, hakuna sehemu iliyo nzuri na muhimu na ambayo inaweza ikatia matumaini kwa Watanzania. Kwa kweli taarifa hii iko kwenye mitandano kwa Karne hii ya 21 ni taarifa muhimu sana. Watanzania wengi wanasoma siyo kwamba ni sisi tu tulioko hapa Bungeni, kwa kuwa wao pia wanasoma, wanasubiri mustakabali wa maamuzi yenye tija na malengo sahihi kwa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yapo mambo ya msingi sana japokuwa taarifa hii imeletwa kwetu kama Muhimili wa Bunge, kama chombo cha wananchi na kwa kuwa Watanzania wengi wanaisoma na kwa kuwa, Taarifa ya CAG inapokuja Bungeni, CAG ameshahangaika sana, tuna kila sababu ya kumpongeza kwa sababu mpaka ije kwetu ameomba vielelezo vyenye kumpa matumaini kwamba hoja hizi zinajifuta, zina usahihi na matumizi sahihi ya fedha zilizotajwa katika kurasa zote za taarifa ya CAG.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo basi, kwa kuwa alikuwa ameomba nyaraka za kuweza kuthibitisha matumizi sahihi na ikashindikana, hatimaye wakati anafunga taarifa zake amekuja kukitaka chombo hiki cha wananchi Bunge na Muhimili wa Serikali waweze kujadili na kuona maoni yake yanafanyiwa kazi. Kwa miaka kadhaa tukiwa Wabunge tumekuta taarifa za CAG zinapokuja zinajadiliwa hapa Bungeni na hatimaye hatua zinazochukuliwa zinakuwa pengine hazikidhi na kutosheleza yale matakwa sahihi ya Watanzania na malengo wanayokusudia. Nitazungumzia mifano michache.

Mheshimiwa Spika, CAG anapotoa taarifa hapa yeye ameshachambua vya kutosha hivyo. Mimi siungani na wale wanao sema kwamba tuunde chombo kifanye utafiti tena. Tunachotarajia ni kwamba baada ya taarifa hii sisi kuijadili na kuisoma na kuona madudu yalivyo, matatizo yaliyojitokeza na matumizi mabaya ya fedha za umma; lengo letu kama Bunge, ninalishauri Bunge letu nakulishawishi, kwamba pengine sisi, kwa sababu wananchi wana matumaini kwetu, tuwe na maamuzi ambayo yatatoa matumaini kwao. Kwanza kuwawajibisha wale wote waliohusika kwenye taarifa hii na ambao wanaichezea mali ya umma.

Mheshimiwa Spika, vipo vyombo vya kutosha katika nchi hii kuchukua nafasi kuchambua taarifa hizi kuleta baadhi ya taasisi ambazo tayari ama wahusika wa ngazi mbalimbali wamehusika kwa namna moja au nyingine kutufikisha hapa tulipo. Kwa sababu hizi ni kodi za Watanzania na Watanzania wanataka huduma na viongozi wa nchi kama Rais na waandamizi wengine wote wanahangaika kutafuta namna ambavyo matatizo ya Watanzania yanatatuliwa; hivyo kuna kila sababu ya sisi kama Bunge kuweza kufikia maamuzi magumu kwa ajili ya Watanzania.

Mheshimiwa Spika, kwa nini ninasema hivyo? labda nizungumze mifano michache. Mfano wa kwanza ni fedha za COVID 19. Tulisubiri magari ya ambulance tunakaribia mwaka, fedha hizo hazijaleta magari ya ambulance. Kichwani kwangu au kwenye mawazo yangu nawaza kwamba hata hizi fedha pengine za kununua hayo magari ingekuwa ni watu wanafanya mchezo wa Pwagu na Pwaguzi wanaweka kwenye akaunti ya deposit leo hii ina shilingi ngapi? Kwa nini manunuzi yanachukua muda mrefu kiasi hiki? Hatuoni kuwa kiasi cha fedha kilichotarajiwa kununua mitambo ya magari ya ambulance machine za X-rays na mitambo mingine ya kuchimba maji na mitambo mengine kwa manunuzi ya Umma yamechukua muda mrefu kiasi kwamba kuna mchezo wa kuchelewesha huduma kwa Watanzania?

Mheshimiwa Spika, hali hii inafanya Watanzania kutokuwa na imani na Bunge hili na kutuelewa vibaya. Kwa hiyo mimi nilikuwa nashukuru kama Mawaziri watakuja hapo, kila Waziri kwa kadri ya sekta anazosimamia na Wizara anayoisimamia aje na maelezo mahususi yatakayo wapa Watanzania Imani; kwanza ya kuchukua hatua lakini la pili kwa nini tunafika hapo, majibu yake yaweze kuridhisha Watanzania.

Mheshimiwa Spika, kwa nini nasema hivyo; kadri ambavyo CAG kila siku analeta taarifa hapa na sisi kila mwaka taarifa inapokuja tunakuwa tunachangia kwa kukwepa kwepa madhara yake ni kuwa tunamkatisha tamaa CAG na watendaji wake wote hadi ngazi ya chini. Kwa sababu yeye anafanya kazi ngumu na kazi ya kwenda kupekua watu na kazi ya kuleta taarifa hapa ni kazi ngumu, kazi ya kwenda kuandaa taarifa yenye ufafanuzi, wa kina na yenye kurasa zaidi ya elfu ni kazi ngumu.

Mheshimiwa Spika, wakati fulani, nchi hii ilipoingia kwenye tumbua tumbua hatukuielewa. Mimi nadhani hatukuielewa, sababu za kutumbua tumbua ilikuwa ni kwa kuwa wale waliokuwa wanapaswa kuchukua hatua hawakuchukua hatua kwa wakati unaofaa na kwa hivyo basi yule ambaye anamamlaka aliona ni nafuu nianze na yule aliyekaribu na mimi ili wale wengine waanze kuhofu kwamba kumbe mimi nisipochukua hatua kwa wakati basi wale wengine watachukua hatua na mimi naweza kufikiwa na janga hilo.

Mheshimiwa Spika, tutaishukuru sana Serikali, hasa Mawaziri, watakapo kuja, kwa sababu hivi punde tutahitimisha hoja hii, hivyo waje na kauli. kwa kwanza kuliomba Bunge maeneo ambayo wao wanahitaji msaada kwa Bunge, ushauri au hatua za kuchukua ili ziridhiwe kupitia sheria tulizopitisha. Pili, kuona ni kwa namna gani tatizo hili halijirudii. Tuanze na taasisi kadhaa ambazo kwa miaka mitatu taarifa zao zilikuwa chafu kupitia kwa Mkaguzi wetu (CAG), ili sisi pia kama Bunge tunapochukua hatua au tunapowapa wao nguvu kama Serikali basi nchi ipate unafuu na mafanikio wa yale ambayo Watanzania walio wengi wanatarajia.

Mheshimiwa Spika, hali nyingi zinajitiokeza kwa sababu ya uzembe, uadilifu na utimizwaji wa wajibu na majukumu. Haiwezekani tunachukua watendaji wabovu tunawazungusha kwenye nchi. kwamba anahama taasisi moja Kwenda nyingine ama halmashauri moja kwenda nyingine. Matatizo makubwa yanaendela katika nchi wakati nchi inawasomi wa kutosha. Ndani ya hiyo taasisi ambayo tunawahamisha hao watendaji wabovu, kuna watendaji wazuri lakini hawapewi nafasi kwa ajili ya kulindana pengine au kujenga mfumo ambao ni dhaifu katika nchi na mfumo ambao hauna tija kwa Tanzania nchi yetu. Na sisi ipo siku ama kupitia dhamana zetu tulizopewa tutalaumiwa na kulaaniwa; au kupitia nafasi zetu kwa wananchi, wananchi watakosa imani kwetu sisi kama Bunge na Serikali yao.

Mheshimwa Spika, kwa nini nasema hayo? fedha nyingi ukizijumlisha unafika mwisho hazijumlishiki, fedha ambazo tayari zimekosa matumizi na hazijaenda kutoa huduma.

MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

T A A R I F A

MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Mimi nilikuwa naomba nimpatie taarifa Mheshimiwa mzungumzaji kwamba anayosema ni sahihi. Nafikiri sisi kuhangaika na wale watendaji kule chini ni sawasawa na kufukuzana na nyuki. Sisi watu wetu ni hawa Mawaziri na Watendaji wengine Wakuu Serikalini.

SPIKA: Mheshimiwa Zacharia Paulo Issaay, unapokea taarifa hiyo?

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, mimi naipokea kwa mikono miwili (Makofi). Nchi hii ina mihimiri, mimi nikupongeze sana, sisi kubebeshwa mzigo kuhangaika kule chini, mimi naungana na mtu aliyenipa taarifa. Si muda wetu sasa hivi, sisi ni chombo na chombo hiki, kiungo chetu ni Serikali na Mawaziri, wao wachukue hatua, na wao wakichukua hatua nchi inapata unafuu.

Mheshimiwa Spika, kwa nini tunasema hivyo? Taarifa hii imechakatwa na kule halmashauri ilikotoka kuna mtu anaitwa mkaguzi wa ndani, na mkaguzi wa ndani atatakiwa apeleke vielelezo kwa wale ambao anawataka walete vithibitisho kwa ajili ya taarifa zenye utata. Kwa hiyo unapoenda kwenye ngazi ya halmashauri kwenye taarifa za halmashauri huko, zile halmashauri zinazofanya vibaya zilishapewa muda wa kupeleka nyaraka za utetezi ili mwisho wa siku hoja zao zifutwe. Hadi tunaletewa huku, walishashindwa, hawakupeleka.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa hawakupeleka Mkaguzi Mkuu (CAG) hawezi kuacha kazi yake, ni lazima alete taarifa yake kwetu sisi kama Bunge na chombo cha wananchi na muhimiri Serikalini kuelezea hali halisi ya taasisi zilivyo. Kwa hiyo kule zilishadaiwa zifutwe kwa nia ya kwamba nyaraka zipelekwe lakini zimeshindikana, hapa zimekuja mahakamani ili zihukumiwe, kwa sababu umepewa nafasi ya kutetea hukutetea umepewa muda hukutumia vizuri. Sasa ni wakati wa chombo hiki kuamua ili Watanzania wapate amani.

Mheshimiwa Spika, si kwamba tuna chuki sana na Mawaziri lakini kadri unavyochelewa kuchukua hatua basi tatizo linakuwa…

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, taarifa.

T A A R I F A

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, nilikuwa nataka nimpe taarifa mzungumzaji, kwamba ukweli sasa hivi inatakiwa tuchukue maamuzi magumu. Nitatoa mfano kidogo 2018, tuliingiziwa pesa za ujenzi wa Kituo cha Afya Nyang’wale tarehe 26 Mwezi wa 6, kufikia tarehe 1 mwezi wa 7 milioni 400 zikawa hazijulikani zilikokwenda, na hadi leo hii watu hao wako mtaani wanaendelea na shughuli zao kama kawaida. Nilikuwa nataka kumpa taarifa Mheshimiwa.

SPIKA: Mheshimiwa Zacharia Issaay, umepokea taarifa hiyo?

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, kwa mikono miwili. Fedha milioni 400 anazozizungumza mtoa taarifa ni kodi za Watanzania; na fedha hizo kwa kuwa hazionekani ziliko halafu bado wale watu wako wanaendelea; na tunatunga sheria hapa za utakatishaji wa fedha, matumizi mabaya ya fedha na Sheria nyingine nyingi kama vile za manunuzi halafu hatuzisimamii. Tunaendelea kupiga kelele na kodi za Watanzania zinatumika kulipa vikao hivi vya Bunge na gharama za uendeshaji wa Bunge, je tunaitendea haki nafasi yetu kweli?

Mheshimiwa Spika, mimi nadhani pamoja na sababu nyingi zilizowasilishwa na Waheshimiwa Wabunge, mimi niwapongeze sana Waheshimiwa Wabunge, katika kipindi hiki cha kujadili taarifa hii tumetendea haki nafasi zetu kwa hali ya juu sana. Hii ni kwa sababu sisi ndio tunaosubiriwa tuseme ili nchi ipone, na sisi ndio tunasubiriwa tuseme kwa niaba ya Watanzania milioni 60. Tunakwenda wapi kama endapo tunaanza kukwepa maamuzi magumu ambayo yataisafisha nchi na yataiweka nchi mahali pazuri?

Mheshimiwa Spika, mimi niwaombe Wabunge wenzangu tuungane kwenye hoja hizi na tutazame kwa kina maslahi mapana ya taifa letu, tuweze kuzungumza tukiwa Wabunge kama sehemu ya Watanzania na hatimaye maazimio tunayoazimia hapa kwa kuzingatia Sheria na Kanuni zetu za Bunge na Sheria nyingine za nchi yaweze kuwa na tija na kuhakikisha nchi yetu inapata ahueni na mafanikio ya maendeleo yanapatikana.

Mheshimiwa Spika, mengi yatazungumzwa lakini hatima yake, tunapo kwepa maamuzi magumu yote tuliyo yazungumza hayatakuwa na tija. Ili yale tuliyazungumza yawe na tija, na taarifa zimeletwa hapa na zimeeleza madudu ya kila sehemu, tuchambue kadhaa tuchukue hatua, tuweze kunoa Sheria inasema nini na wajibu wetu ni nini ili hatimaye nchi iweze kubadilika. Vinginevyo, kila mwaka CAG atahangaika kuleta taarifa hapa, taarifa zake atakazoleta hapa, hatutampa matumaini na hatutaona kama ni sehemu muhimu, na mwisho wa maamuzi yetu yatadharauliwa na Watanzania milioni 60.

Mheshimiwa Spika, nahitimisha kwa kuunga hoja mkono kwa asilimia mia moja, mchano wangu uishie hapo.