Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza, nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amenipa nafasi hii na uhai nilionao naamini uko mikononi mwake. Pia nichukue nafasi hii kukupongeza wewe Mwenyekiti, nafikiri makofi yaliyokupokea yanaonyesha jinsi gani Waheshimiwa Wabunge wanavyokuunga mkono. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa kweli mwanzo ni mzuri. Mimi niwatie moyo, songeni mbele, kazi yenu tunaiona, juhudi zenu tunaziona na sisi tuko nyuma yenu, tutawaunga mkono. Niwaombe Waheshimiwa Wabunge kwa kweli hawa bado ni vijana wanafanya kazi nzuri tuwaunge mkono tusibeze, huu ni mwanzo tu. Mtu anapofanya vizuri hata kama upo upande wa pili hebu muungeni mkono. Haya yote tunayoyafanya ni kwa ajili ya nchi yetu siyo kwa ajili ya wana CCM tu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee suala la afya. Ndugu zangu tuko hapa Bungeni kwa sababu afya zetu ni nzuri, Wizara ya Afya ndiyo kila kitu. Katika kuchangia kwangu niiombe Serikali wamekuwa wakileta bajeti kwenye vitabu lakini inapelekwa asilimia kidogo sana. Tuiombe sasa hivi Serikali tuwe makini sana, hili ni jambo muhimu ambalo linahitaji kuungwa mkono na kila mtu. Tunahitaji afya zetu ziwe nzuri ili tuweze kuwatumikia Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaposema kuingia kwenye nchi ya viwanda na uchumi wa kati lazima afya zetu ziwe nzuri. Hao Watanzania wawe na afya nzuri waweze kuzalisha, bila kuwa na afya nzuri hatuwezi tukafanikiwa hayo tunayoyalenga. Ili tuweze kufanikiwa kwenye kilimo chetu, kiwe kizuri lazima tuwe na afya nzuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Wizara hii tuiunge mkono na kama wengine walivyochangia kwa kweli namuunga mkono Mheshimiwa Bashe ambaye amesema Wabunge wote bila kujali tunatoka chama gani tuungane akinamama waweze kupatiwa bima za afya. Kwa kweli hili ni jambo muhimu, akinamama wengi wanakufa si kwa sababu ya magonjwa ni kwa sababu hawapatiwi huduma nzuri. Kwa mfano, kama kule kwetu Kyerwa hakuna huduma nzuri za afya, hali ni mbaya. Kule vijijini hali ni mbaya sana, hii mikoa ya huku pembezoni ndiyo kabisa unaweza ukafikiri Serikali haipo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano ukija kwetu Kyerwa kuna watumishi watano tu na hao wako wilayani, kwenye kata hakuna mtaalam hata mmoja. Hawa watu mnawahesabia wapi? Naiomba Serikali tusiangalie mijini tu twende mpaka vijijini na hao wataalam ambao wako maofisini wasikae makao makuu tu waende vijijini wakaone hali ilivyo. Mara nyingi wataalam wamekuwa wakiuliza huko vipi, fikeni mkaone hali ilivyo. Nimwombe Mheshimiwa Waziri Ummy Mwalimu na Ndugu yangu Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla wafike Kyerwa waone hali halisi ilivyo, hali ni mbaya sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye zahanati zetu hakuna dawa kabisa. Hawa wazee mnaosema wakate bima ya afya, wanakata bima ya afya, lakini ni aibu kwanza tumalize kitu kimoja. Huyu mzee unamwambia akakate bima ya afya, anakwenda anamwona Daktari anamwandikia, akishamwandikia anamwambia dawa hakuna, dawa muhimu Kyerwa asilimia kubwa hakuna.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Serikali, tunaposema hao wazee watibiwe bure, watoto wenye umri chini ya miaka mitano wapate huduma bure, akinamama wajawazito wapate huduma bure lazima tuhakikishe yale mahitaji yote yapo, tuhakikishe dawa zipo, huduma zote zipo siyo tunasema tunawapa huduma bure wakati hakuna vitendea kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine, tunalo tatizo la watumishi, hakuna watumishi, hakuna Madaktari. Kwa mfano, kule kwetu Kyerwa na naamini ni maeneo mengi hakuna Madaktari. Ndugu zangu, niwaombe na niiombe Serikali tusipange mipango mingi, hebu tupange mipango michache tuweze kuitimiza ndiyo twende kwenye mipango mingine. Tusiseme tutafanya vitu asilimia mia moja halafu mwisho wa siku tunakuja kufanya asilimia tano ni aibu. Kwa hiyo, niiombe sana Serikali ishughulike suala hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nataka niseme, huwezi ukazaa mtoto ukampa mtu mwingine akulelee. Mwenye uchungu na afya ya Mtanzania ni Wizara ya Afya. Huyu ndiye mzazi! Unampaje huyu mtoto mtu mwingine amjengee wodi, amletee vifaa? Haiwezekani! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaomba Waheshimiwa Wabunge, ifike wakati hizi sheria zinatungwa humu ndani tukazibadilishe. Mwenye uchungu ni Mheshimiwa Ummy Mwalimu na Wizara yake na Watendaji wenzake; huyu ndiye anayehudumia afya za Watanzania. Nawaomba Waheshimiwa Wabunge, hizi sheria tuzibadilishe, tusiseme kila kitu tumejaza huku TAMISEMI, kila kitu TAMISEMI, lakini mwisho wa siku afya za Watanzania zikiwa mbaya anayeulizwa ni nani? Ni Wizara ya Afya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana, Serikali tujipange vizuri, tufikishe madawa kwa wananchi. Hakuna madawa, tunahimiza hapa Watanzania wakate Bima ya Afya, dawa watazipata wapi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine, hawa wa MSD nasikia wanadai pesa kibao! Serikali iwapelekee pesa ili Watanzania waweze kupata madawa, kwa sababu hata tukisema tumejenga vituo, tumejenga maduka ya madawa, mwisho wa siku hawa MSD pesa watazitoa wapi? Sasa tunaomba Serikali ijipange, zamu hii Watanzania wale ambao wanapata huduma hizi bure wanapokwenda siyo anaandikiwa na Daktari cheti halafu mwisho wa siku anakwenda kununua dawa dukani; wengine hawana uwezo. Wakati mwingine tunaanza kwetu, sisi wenyewe Wabunge mbona hatuendi kununua dawa kwa pesa yetu? Si tumepewa Bima ya Afya na tunapata dawa? Lazima tusimame tuhakikishe tunawatetea wananchi wetu, tusiangalie mambo yetu wenyewe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine ni kuhusu vifo vya akinamama. Kuna maeneo mengine miundombinu ni mibovu, kama kule kwetu Kyerwa mtu unatoka tuseme labda Kaisho uende kutibiwa Hospitali ya Nyakahanga, ni mwendo mrefu, barabara mbovu, huyo mama kama ni mjamzito mimba itatoka tu. Kwa hiyo, naiomba Serikali, hivi vitu vyote hatuwezi tukavitenganisha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, namwomba Mheshimiwa Waziri, hata kama haihusiani na huko, ninachojua wewe ni Waziri wa Afya unashughulikia afya za Watanzania. Tunacho Kituo chetu cha Afya pale Nkwenda; hiki kituo tunaomba Mheshimiwa Waziri, bado kina upungufu, lakini hiki kituo tunaomba kiwe hospitali kamili. Hatuna Hospitali ya Wilaya, hospitali tunayoitegemea ni Hospitali ya Mission ambayo wananchi hawawezi kumudu gharama za matibabu, ni kubwa sana. Nilishaiandikia Serikali mwaka 2015 nilipokuwa hapa Bungeni kuiomba hii Hospitali ya Mission…
MWENYEKITI: Ahsante!
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.