Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

Hon. Kilumbe Shabani Ng'enda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kigoma Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia, na zaidi namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha kuendelea kuwa na afya ya kutumikia Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijasema yale ninayokusudia kuwa ni mchango wangu katika eneo hili, napenda nichukue nafasi hii kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Kigoma Mjini kumshukuru sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mama yetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa ziara nzuri yenye matumaini na iliyotutia nguvu sisi wawakilishi wa wananchi pamoja na Watumishi wa Serikali katika Mkoa wa Kigoma. Ametufungua katika mambo mengi, ameelekeza mambo mengi ambayo kwa kweli yanakwenda kuipa Kigoma sura mpya ya maendeleo. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais na tunamwombea afya njema yeye pamoja na wanaomsaidia ili waweze kutimiza matarajio ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nizishukuru sana Kamati zote tatu zilizowasilisha hoja zake hapa Bungeni. Katika kuzishukuru, nipeleke shukurani vilevile kwa CAG kwa ofisi yake ya kufanya kazi nzuri ya kutupa miwani ya kutazama mambo mengine ambayo yanafanyika kwenye utendaji na sisi huwa hatuyaoni mpaka tuletewe na yeye.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kujielekeza katika kuzungumzia hasa mapendekezo yaliyotolewa na Kamati ya LAAC na PAC. Nianze na LAAC. Ushauri na mapendekezo haya yametolewa katika ukurasa wa 19 hadi 24 wa taarifa yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wamezungumzia uwekezaji wenye tija. Uwekezaji wenye tija maana yake Halmashauri zetu zinapowekeza, ziwekeze katika maeneo ambayo zinakwenda kupata tija, zinaongezea mapato na mapato yale yanasaidia hata halmashauri zenyewe kuweza kufanya miradi ya maendeleo kutokana na fedha wanazokusanya kwa makusanyo ya halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, imeonekana hapa kuna miradi mingine watu wanafuata mkumbo tu, kwamba madhali halmashauri fulani wana stendi na sisi stendi; madhali wana soko, na sisi soko; basi ni miradi kama hiyo. Kwa ujumla niseme, kwenye eneo hili napenda kuishauri Serikali kwamba zipo halmashauri ambazo zinakuwa na matatizo ya kubuni miradi na kuisimamia kutokana tatizo la wataalamu.

Mheshmiwa Mwenyekiti, nichukue Manispaa yangu ya Kigoma Ujiji. Manispaa ya Kigoma Ujiji ni miongoni mwa Manispaa ambazo zina makusanyo madogo, kiasi kama cha Shilingi bilioni tatu kwa mwaka, kiasi ambacho unaweza ukasema ni kidogo sana. Halmashauri hii ina tatizo kubwa la wataalamu. Ukienda kwenye wahasibu ni tatizo, ukienda kwenye wakaguzi; Manispaa nzima ina mkaguzi mmoja, yaani afanye kazi zote za ukaguzi zinazotakiwa kufanywa, wahandisi ni tatizo, valuer ni tatizo. Kwa hiyo, tuiombe Serikali iwezeshe halmashauri zetu kupata wataalamu ili waweze kubuni miradi na kuisimamia vizuri, hapo tutaweza kusaidia kuongezeka kwa mapato ya halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine, wamesema hasara zitokanazo na taasisi za Serikali. Zipo hasara ambazo Halmashauri zinapata kutokana na taasisi za Serikali. Moja ya taasisi iliyotajwa ni MSD. MSD inatajwa kwa sababu inalipwa fedha kwa ajili ya kuleta vifaa vya hospitali; vitanda vya hospitali na madawa, baada ya kulipwa fedha wanachukua miezi mitatu, minne, mitano, sita hawajaleta vifaa hivyo. Kwa hiyo, wanaitia hasara halmashauri.

Mheshiniwa Mwenyekiti, kuna taasisi kama TEMESA, hawa yaani sijui niseme, ingekuwa ni mamlaka yangu, ningeweza kuangalia: Je, inastahili kuendelea kuwepo au isiwepo? Yaani hawa ukienda, unataka kukagua magari, unataka kutengeneza gari, hawana wataalamu, hawana vipuri, waende tena kwenye maduka ya watu binafsi wakatafute vipuri hivi, gharama ya TEMESA inakuwa gharama kubwa kuliko gereji za watu binafsi. Kwa hiyo, lazima serikali iangalie eneo hili. Tumeweka kwa nia njema, lakini tusipoangalia litakuwa mzigo kwa Serikali na mpaka sasa TEMESA ni mzigo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, GPSA; yapo malalamiko ya Idara za Serikali chungu mzima, zimeingiza pesa GPSA, kwa ajili ya kulipia magari, mwaka mzima mpaka leo hawajapata magari. Mwezi Novemba kuna taasisi zimeingiza pesa, mwezi Novemba huu hawajapata magari. Magari hayo yalitakiwa kuja kufanya kazi kwa ajili ya kuongeza tija kwenye Serikali, lakini GPSA wamepewa, hivi Serikali wanakwama wapi Ukienda gereji TOYOTA ukiwapa oda miezi mitatu wamekuletea gari, mwaka mzima GPSA hawajaleta gari.?

Mheshimiwa Mwenyekiti, taasisi nyingine iliyoyatajwa ni NHIF. NHIF imetajwa kwa maana ya kwamba uko mfumo ambao nataka niishauri Serikali waone jinsi ya kuubadilisha. NHIF inaingia mkataba na hospitali za Serikali na binafsi kwa ajili ya kuhudumia wateja wao ili wao waweze kuwalipa. Wanapokwenda kuhakiki malipo, NHIF wanaamua haya tutalipa haya hatulipi labda kuna kasoro fulani fulani na wakishaamua wao ndiyo wa mwisho. Haiwezekani, tukawa na mamlaka ambayo yenyewe inaingia mkataba na watu na wakitofautiana yenyewe ndiyo yenye mamlaka ya mwisho ya kuamua, nikulipe au nisikulipe. Hata mikataba mbalimbali, hata ya Serikali, mnaambiwa kwamba tukitofautiana, tutatafuta arbitration kabla ya kwenda Mahakamani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa arbitration ya hawa NHIF na zahanati zetu za Serikali na zahanati za watu binafsi, ni nani? Kwa hiyo lazima kitafutwe chombo hapa ambacho kitakuwa kati, iwapo NHIF watasema mimi siwezi kulipa, basi huyu aliyetoa huduma akimbie kwenye chombo hicho aseme NHIF wananionea, nimetoa huduma hawataki kunilipa. Hilo ndilo wazo langu ambalo ningependa kuishauri Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye Kamati ya PAC ukurasa wa 28, kuna suala la Polisi, kutoandaliwa kwa hesabu na kufanyika kwa ukaguzi wa hesabu za Mfuko wa Tuzo na Tozo wa Polisi. Kamati imelieleza vizuri, huu Mfuko upo kwa mujibu wa sheria ‘The Police Force and Auxiliary Service Act, Cap No. 322’, lakini CAG amebaini kwamba, kwenye Mfuko huu kuna pesa zimewekwa kwenye Benki Kuu, bilioni 35.3, lakini pesa hizi hazikaguliwi wala haziletwi taarifa yake katika ukaguzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vyombo hivi sisi tunaviheshimu sana, vyombo vyetu hivi vya ulinzi. Tungependa viwe clean, wanafanya kazi nzuri, wasichafuliwe na mambo haya madogo madogo. Mimi niombe sana kwamba utaratibu usimamiwe chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani, kuhakikisha mifuko kama hii ambayo nia yake ni njema inakaguliwa na utaratibu unafanyika. Mzee wangu, mzee Yusuph Makamba aliwahi kusema, ukiumwa na nyoka utatibiwa na mzizi, sasa ukiumwa na mzizi unatibiwa na nini? Maana hawa polisi ndio kazi yao kukamata wezi na wahalifu, sasa kama wao ikitokea uhalifu tunafanyaje, kwa hiyo hivi ni vyombo vya kuviangalia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapo hapo kuna Idara ya Uhamiaji, kwenye idara hii ukaguzi maalum ulifanywa kwa mujibu wa kifungu cha 93, Idara ya Uhamiaji imekuwa ikitoa stika bandia za visa. Hizi DCI alibaini katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Nyerere. Vitendo hivi na stika hizi zimekuwa zikiingia kupitia KIA. Sasa CAG baada ya kufanya ukaguzi kwa kipindi cha miezi sita tu, CAG amebaini kwamba kuna upotevu wa kiasi cha Shilingi bilioni 2.4 na kuna Maafisa 32 wa Idara ya Uhamiaji ambao wanahusika na wamefika mahali wakacheza na kanzidata na kufuta kwenye kanzidata watu ambao walilipa visa, ambao ni wa nje watu 21,208.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa haya ni mapato makubwa sana ya Serikali na vitendo hivi vimekuwa vikifanyika huko zamani. Hata huko Kigoma waliwahi kiwajibishwa Maafisa Uhamiaji kwa kugonga muhuri wa entry halafu ile nanii ya visa hawakukata au dola hamsini wanachukua dola 30 wanaacha dola 20, waliwajibishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi nashukuru Mungu Kigoma mambo ni mazuri, tunaye Afisa Uhamiaji na Mkuu wa Mkoa ambaye wanasimamia mambo vizuri, yanakwenda vizuri. Uzoefu ule wa Kigoma ungeweza ukatumika kuangalia maeneo mengine yote na huu uliojitokeza KIA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)