Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

Hon. Dr. Oscar Ishengoma Kikoyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Muleba kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipatia fursa hii nami nichangie hoja ambayo iko mbele yetu. Kwanza kabisa nikupongeze wewe kwa kazi unayofanya ya kuliongoza Bunge letu. Vile vile nimpongeze Rais wetu kwa kuliongoza Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jana wachangiaji wengi waliongelea mambo makubwa ambayo Taifa letu linayapitia. Sisi kama Kamati ya PIC, kazi tunayoifanya ni kupitia uwekezaji wa mitaji unaofanywa na Serikali yetu kwenye mashirika yetu ya Umma. Katika mashirika ambayo yako chini ya TR yanafika zaidi ya 237 na haya yote Serikali inawekeza pesa ya walipakodi kwa lengo la kuboresha hayo mashirika na kutengeneza fedha.

Mheshimiwa Spika, katika uchambuzi wetu tumepitia mashirika na baadhi ya ripoti za TR na ripoti ya CAG, takwimu zinaonesha kwamba mashirika yetu yanafanya vizuri. Mpaka mwaka 2021 mitaji ambayo imewekezwa na Taifa letu kwenye hayo mashirika inanafikia Shilingi trilioni 67.95. Huo ndiyo utajiri ambao uko chini ya mashirika ya Umma.

Mheshimiwa Spika, ukisoma takwimu, thamani ya uwekezaji wetu katika mashirika haya umekuwa ukipanda lakini ongezeko hilo limekuwa likipungua. Kwa mfano, mwaka 2016/2017 thamani ya mashirika yetu ilikuwa ni Shilingi trilioni 49.6, imeendelea kupanda mwaka 2017/2018 imekwenda Shiligi trilioni 57.79, mwaka 2018/2019 imekwenda Shilingi trilioni 60.3, mwaka 2019/2020 Shilingi trilioni 65.19, na mwaka 2021/2022 Shilingi trilioni 67.79.

Mheshimiwa Spika, kwenye ukuaji wa ongezeko la thamani ya mifuko imekuwa ikishuka. Tunayo sababu ya kujiuliza, kwa nini uwekezaji unaongezeka lakini ongezeko au ukuaji wa ongezeko unashuka? Mwaka 2016/2017 ongezeko lilikuwa ni 63.8%, mwaka 2017/2018 ilishuka ikaja kuwa 13.6%, mwaka 2018/2019 ilishuka mpaka 8.1%, mwaka 2019/2020 ilibaki pale pale 8.1%, na mwaka 2021 ilishuka ni 4.2%. Tunao wajibu wa kujiuliza kwa nini inashuka hivyo? Tusipojiuliza leo, baada ya miaka miwili au mitatu inawezekana tukaja zero tukaanza kwenda kwenye hasi tusipochukua hatua leo.

Mheshimiwa Spika, nimeangalia haya mashirika yote, yako chini ya usimamizi wa Treasure Registrar (TR). Ukiangalia sheria inayomwanzisha wa Treasury Registrar ya Tanzania ni ya mwaka 1957, ni ya zamani sana, ni sheria kongwe. Imefanyiwa marejeo chini ya Miscellaneous Amendments Act, 2010. Ila yaliyofanyiwa marekebisho hayampi TR wetu uwezo madhubuti wa kusimamia haya mashirika. Ukiangalia, TR anatoa vigezo vya utendaji wa haya mashirika ya Umma lakini haimpi nafasi; haya mashirika ya Umma yasipotekeleza vile vigezo anavyoviweka, TR hana mamlaka ya kuwajibisha haya mashirika ya Umma. Hicho ni kikwazo kikubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukirejea hiyo sheria ambayo nimeiongelea, ni kongwe, ni ya zamani, na ukiangalia umuhimu wa uwekezaji kwenye haya mashirika, TR anapaswa kuwa na nguvu madhubuti ya kuyasimamia haya mashirika. Taasisi yoyote ambayo inashindwa kutekeleza hivyo vigezo alivyoviweka, lazima ayawajibishe ipasavyo, vinginevyo yataendelea kushuka na tutaendelea kupoteza mitaji yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna mashirika ambayo tusipoyaangalia vizuri ni cash cow ya Taifa hili. Mashirika kama TPA; mashirika mengi ambayo tukiwekeza vya kutosha, tutaweza kutengeneza mitaji na Taifa litaweza kujitegemea kwenye uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, viko vikwazo vingi ambavyo vinafanya mashirika yetu yasifanye vizuri. Mojawapo ya hivyo vikwazo ni sheria yenyewe. Napendekeza Bunge hili liitishe hiyo Sheria ya TR, Tuifanyie marekebisho. Kwa upande wangu ningependa tuifute kabisa hiyo sheria tuanze upya, TR apewe mamlaka kwenye haya mashirika ambayo anayasimamia, awe na nguvu kiasi kwamba bodi ambazo zinashindwa kufanya vizuri, wakurugenzi ambao wanashindwa kufanya vizuri awawajibishe yeye mwenyewe, akisubiri mamlaka za uteuzi kuteua bodi mpya na kuteua wakurugenzi wapya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mamlaka nyingine, kwa mfano, Ofisi ya TR Malaysia, TR ana uwezo uwezo mkubwa sana kusimamia mashirika ya Malaysia. Ukiangalia performance ya mashirika hayo yanafanya vizuri kiasi kwamba TR ana uwezo wa ku-suspend mamlaka yoyote ambayo iko chini yake bila kuuliza mtu yeyote. Ana mamlaka ya kufanya hivyo, baadaye anaandika ripoti kwa mamlaka za uteuzi, zinachagua mamlaka nyingine.

Mheshimiwa Spika, ripoti yetu imebaini pamoja na mambo mengine, kuzorota kwa utendaji wa mashirika ya Uumma kunasababishwa na mambo kadha wa kadha. Mojawapo, limetokea kwenye ripoti ya CAG ukurasa wa 13 kwamba mashirika mengi uteuzi wa bodi unachelewa. Baadhi ya mashirika yanafanya kazi chini ya wakurugenzi ambao hawana bodi na baadhi ya mashirika yametajwa. Kwa mfano, Mfuko wa Kulinda wanyamapori Tanzania; Hospitali ya Rufaa Mbeya, Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania. Hayo ni baadhi ya mashirika ambayo yametajwa na ripoti ya CAG. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa ukijiuliza kwa nini tunakuwa na mashirika ambayo hayana Bodi za Wakurugenzi? Mnajua fika, kama taasisi haina Bodi ya Wakurugenzi, Mkurugenzi na Watendaji wote hawawezi kufanya maamuzi ya kuliendeleza hilo shirika, watabaki tu ku-suspend maamuzi kwa sababu hawana chombo cha kuwa-guide. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tatizo lingine ambalo limebainika ni mwingiliano wa majukumu kwenye baadhi ya taasisi. Jana nadhani Mheshimwia Dkt. Chaya aliyasema hapa. Baadhi ya taasisi zetu zinaingiliana kimajukumu. Jana ndugu yangu Mheshimiwa Dkt. Chaya alisema, TANROADS na TAA, kwamba tuna mamlaka mbili; tuna TANROADS ambayo kazi yake kubwa na ya msingi ni kutengeneza barabara. Ila hapo nyuma tumefanya maamuzi tukaipa TANROADS kutengeneza viwanja vya ndege, lakini tuna Mamlaka ya Kutengeneza Viwanja vya Ndege ambayo ni TAA.

Mheshimiwa Spika, utengenezaji wa viwanja vya ndege na usafiri wa anga kwa ujumla, kwa wataalam mnajua, usafiri wa anga unaendeshwa kwa misingi ya Kimataifa pamoja na miundombinu yake TAA na ujenzi wa viwanja vya ndege uko chini ya mamlaka ambayo inaitwa ICAO, ni mamlaka ya Kimataifa. Hii ndiyo inatoa viwango na vigezo. Kama unavyojua TAA inakuwa regulated na Mamlaka ya Usafiri wa Anga. Sasa unashangaa, ukijiuliza huyu TANROADS anajenga viwanga vya ndege kwa mamlaka ipi na kwa vigezo vipi?

Mheshimiwa Spika, nimesikia wakati tunaongea kwenye Kamati, TANROADS walikuja pale, wakasema wamechukua wataalam wote kutoka TAA wamewapeleka TANROADS. Najiuliza, kwa nini uchukue wataalamu kutoka TAA uwapeleke TANROADS? Kwa nini hiyo kazi ya kujenga viwanja vya ndege ambayo kisheria ipo chini ya TAA, wewe unafanya kazi ya kuhamisha watumishi na kuwapeleka kule. Hii inatupa wakati mgumu na inawapa mamlaka za udhibiti wakati mgumu hasa TCAA ambayo imekasimiwa jukumu la kuhakikisha kwamba viwanja vya ndege vinajengwa kulingana na mikataba ya Kimataifa ambayo inatolewa na ICAO kupitia Chicago Convention Annex 14 ambayo inakwambia viwanja vya ndege vijengwe kwa viwango vipi na ubora upi? Sasa hii tumeikasimisha TANROADS.

Mheshimiwa Spika, naomba ujenzi wa viwanja vya ndege urudi TAA na TANROADS wafanye kazi yao ya msingi ya kujenga barabara, siyo viwanja vya ndege. Kuna maeneo wanasema pale kwamba uwanja wa ndege ni sawasawa na kujenga barabara, siyo hivyo. Kila mwaka tunakuwa na ukaguzi ambao unafanywa na ICAO, tutakwenda mbele, tutafika wakati ICAO itatu-blacklist, ndege za Kimataifa zitashindwa kuja hapa na tutakuja kufanya marekebisho tumechelewa.

Mheshimiwa Spika, nadhani wakati wa kufanya marekebisho ni sasa, ujenzi wa viwanja vya ndege urudi TAA na TANROADS iendelee na majukumu yake ya kisheria. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana, naunga mkono hoja.