Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hoja ya Dharura kuhusu Mikopo ya Elimu ya Juu Nchini

Hon. Timotheo Paul Mnzava

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Hoja ya Dharura kuhusu Mikopo ya Elimu ya Juu Nchini

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kutoa mchango wangu kwenye hoja muhimu sana kwa Taifa letu, lakini pia kwa maisha na mustakabali wa watoto wetu na vijana wetu.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nianze kwa kukiri na kutambua mchango na kazi kubwa iliyofanywa na Serikali, kuendelea kuongeza Bajeti ya Mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu kila mwaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwaka fedha 2017/2018, mikopo ilikuwa ni billioni 427.5. Mwaka wa fedha uliopita na mwaka wa fedha tuliyonao mikopo ni billioni 570, ni hatua kubwa sana. Pamoja na hayo bado tuna changamoto na changamoto ni hii ambayo imeletwa na hoja na Mheshimiwa Ezra.

Mheshimiwa Spika, mwaka jana bajeti iliyopita ya 2021 tulikuwa na billioni 570 na kwa takwimu za Bodi wenyewe wanufaika walikuwa ni laki moja elfu sabini na saba na mia nane tisini na mbili. Mwaka huu wa fedha tulionao bajeti ni ileile bilion 570 na matarajio ni wanufaika haohao laki moja sabini na saba mia nane tisini na tatu, anaongezeka mnufaika mmoja.

Mheshimiwa Spika, changamoto tuliyonayo wenzetu Serikalini hasa Bodi na Wizara ya Elimu walipaswa wawe wameiyona. Kilichotokea hapa ni nini? Mwaka jana wanufaika tuliyokuwa nao wanufaika wapya walikuwa ni elfu sabini mia sita na tisa. Wanufaika waliokuwa wakiendelea ni laki moja na elfu saba na miambili na themanini na tatu. Mwaka huu kwa Bajeti hii hii kwa taarifa za Bodi itawalazimu kuwapa wanufaika wanaoendelea laki moja na thelathini na tano mia nane tisini na tatu. Maana yake ni kwamba kwa idadi hile wanufaika wapya wanaoanza mwaka wa kwanza wanashuka kutoka elfu sabini mpaka wanufaika elfu arobaini na mbili. Kuna tofauti ya wanafunzi wanufaika zaidi ya elfu thelathini ambao tunatarajia hawataweza kupata mikopo kwa Bajeti tuliyokuwa nayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vijana elfu thelathini ni wengi na ni nguvu kazi kubwa sana kwa nchi yetu. Kama Taifa hatupaswi kukubali hata kidogo vijana hao wakashindwa kunufaika na mikopo hii na kushindwa kupata elimu yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, changamoto ni kwamba tuna vyanzo viwili tu vya fedha kwa ajili ya vijana wa vyuo vikuu. Kwanza ni pesa inayotoka kwenye Bajeti, pia pili ni marejesho yanayofanyika kutoka na wanufaika huko nyuma. Nishauri, ushauri wa muda mfupi kabisa, Serikali na Mheshimiwa Ezra, nimshauri kwenye maazimio, ni lazima Serikali ituletee mpango wa dharura ya namna ya kuwasaidia hawa vijana zaidi ya elfu thelathini ambao tunaamini kama tukifanya takwimu vizuri sio thelathini wataongezeka kwa sababu udahili unaongezeka na watu wanaongezeka. Serikali ilete mpango wa dharura, ni namna gani vijana hawa ambao tayari vyuo vimefunguliwa, wanakwenda kupata fedha za mikopo ya kuwasaidia kuweza kufanya masomo yao vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la pili tulikuwa tunataka tushauri, kama ambavyo amesema Mheshimiwa Hasunga, la kwanza ni lazima Serikali na sisi kama nchi, Wizara na Bodi tufanye tathmini upya ya utaratibu wa utoaji wa mikopo, utendaji kazi wa Bodi ya Mikopo, vigezo na masharti yote katika kuzingatia suala la utoaji wa mikopo. Lazima tufanye tathmini ya kitaifa ya muda mrefu kwamba mfumo huu tulionao unaweza kutufikisha au unakwenda kutukwamisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, ufanyike uchunguzi, itengenezwe tume au kupitia Kamati ya Bunge, ufanyike uchunguzi wa vigezo vinavyotumika kutoa mikopo kwa watoto wetu, kwa sababu malalamiko ni mengi, vigezo vipo lakini kwa uhalisia kwenye macho ya faida ya kibinadamu hatuoni kama vinafanya kazi vizuri. Ufanyike uchunguzi wa kina wa vigezo vilivyotumika kwa miaka mitano mpaka miaka kumi, vigezo vilivyotumika, idadi na aina ya wanufaika walionufaika na mikopo ya elimu ya juu ili tujiridhishe kama Taifa kama tuko kwenye sehemu salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia sehemu nyingine tukafanye uchunguzi wa utaratibu wa urejeshaji wa mikopo hii na kiasi cha kinachorejeshwa, kinachoripotiwa na matumizi yanayotumika kwa ajili ya kutengeneza msingi mzuri kwa huko mbele tunakokwenda.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja ya Mheshimiwa Ezra, jambo hili ni la dharura, lazima twende na mpango wa dharura kama Bunge na kama nchi tuwasaidie vijana wetu. Nakushukuru sana.