Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hoja ya Dharura kuhusu Mikopo ya Elimu ya Juu Nchini

Hon. Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hoja ya Dharura kuhusu Mikopo ya Elimu ya Juu Nchini

MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipatia nafasi. Niunge mkono hoja ya Mheshimiwa Ezra, kwa namna alivyoiwasilisha hapa Bungeni na kwa namna hili tatizo linavyotukabili sisi wote katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Spika, katika eneo langu kwenye Jimbo la Vwawa, nimepigiwa simu na watu wa zaidi ya 36 wakilalamika kwamba wamekosa mikopo na wengine waliahirisha mwaka jana wakawa na matumaini kwamba mwaka huu watapata, lakini hawajapata na hali ilivyo tatizo ni kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninachotaka kusema ni kwamba hili tunalolijadili pengine tunaweza tusipate ufumbuzi kwa leo na tunaweza tusilijadili kadri inavyowezekana, lakini naliona kwamba lazima tuje na majawabu ya muda mfupi na tuje na ya muda mrefu. Sasa kwa muda mfupi nitapendekeza nini kwamba ambacho tunafikiria kwa sasa hivi. Kwa sababu nchi yeyote bila kuwa na maarifa, bila watu wake kuwa na maarifa ya kutosha. Watu bila kuwa na ujuzi huwezi kujenga uchumi imara na huwezi kuleta maendeleo ndani ya nchi ile.

Mheshimiwa Spika, ndio maana Serikali ya Awamu ya Sita, imeamua kuweka uwekezaji mkubwa kwenye hili eneo. Ukiangalia namna tulivyowekeza kwenye shule za msingi, shule za sekondari, ukiangalia madarasa yanayoendelea kujengwa, vyuo vinavyoendelea kupanuliwa, kwa uwekezaji huu ni kwamba tunataka tuijenge jamii iliyoelimika, yenye ujuzi ambao ni mahiri, itakayoweza kuleta maendeleo ya nchi yetu na ndio tutaweza kupambana na umaskini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa katika uwekezaji huu wa shule za msingi na sekondari ni lazima uwiane na namna tunavyowapeleka kwenye vyuo vya elimu ya juu na vyuo vya kati. Sasa hivi hapa pana changamoto, nafikiri lazima Serikali ituambie tunafanyaje ili tuweze kujinasua hapa. Bodi hii ya Mikopo imekuwepo kwa zaidi ya miaka 17. Ni wazi na mafanikio yapo, lakini zipo changamoto ambazo lazima tuziangalie kwa undani. Tuangalie suala la kibajeti, bajeti iliyo ukiangalia na idadi ya udahili inatosheleza? Lipo suala la muundo wa Bodi namna inavyotekeleza majukumu yake, kama taasisi, je, katika hali tuliyonayo, mazingira ya leo, huu muundo wa bodi unatosheleza? Katika hali tuliyonayo vigezo vinavyotumika katika kuwapatia watoto mikopo au kutowapatia, hivyo vigezo vinatosheleza? Namna tulivyojipanga kugharamia hii mikopo tumejipangaje? Kwa hiyo nafikiri yapo mengi ambayo ni ya msingi ili tuweze kujinasua.

Mheshimiwa Spika, sasa nataka kupendekeza kwamba katika hali ya udharura iliyopo Serikali ituambie ina Bajeti ya shillingi ngapi ambazo imepata sasa hivi? Pia Bunge hili kwa sababu ndilo linalopitisha Bajeti, tuangalie kama inawezekana zikatafutwa fedha mahali pengine popote kama tulivyofanya wakati tulipokuwa na crisis ya kwenye kilimo, kama tulivyofanya katika maeneo mengine ili tuwekeze kwenye hili eneo angalau tuvuke kwa kipindi hiki, hii itatusaidia sana.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa suala la muda mrefu, Wizara ifanye mapitio ya kitaasisi, ya kimuundo na kuangalia je, muundo tulionao huu unakidhi mahitaji ya leo ya sayansi na teknolojia? Naamini kwa kufanya hivyo, najua jitihada zimechukuliwa na Serikali, nimemsikia Waziri ameunda tume, amefanya nini, lakini ya msingi ya dharrla lazima kwanza tuje na Bajeti ya kutatua hili tatizo ndiyo tujipange sasa kwa siku zinazokuja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile la pili, tufanye mapitio ya sheria iliyopo, je, hii sheria inatosheleza? La tatu, tufanye mabadiliko ya mfumo wa utoaji wa mikopo na la nne tuangalie sasa mipango ya kupata fedha, siyo tu kwa upande wa Serikali bali tushirikishe na wadau wengine kuweza kuongeza fedha katika hili eneo na ikiwezekana badala ya kuitwa Bodi ya Mikopo iwe ni Mfuko wa Elimu na ikiwa Mfuko wa Elimu, isiwe elimu ya juu tu hata elimu ya kati.

Mheshimiwa Spika, najua kuna tatizo la muda, basi nasema naunga mkono hoja na naamini Serikali itakuja na tamko kwa suala hili la dharura. Ahsante sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)