Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Prosper Joseph Mbena

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. PROSPER J. MBENA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi naomba niungane na Waheshimiwa Wabunge wenzangu waliompongeza Mheshimiwa Dkt. Philip Mpango, Waziri wa Fedha na Mipango pamoja na timu yake yote ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa uwasilishaji mzuri wa Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa mwaka 2016/2017.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kabla sijachangia, naomba nichukue nafasi hii kuwashukuru sana wananchi wote wa Jimbo langu la Morogoro Kusini kwa imani kubwa waliyonionesha kwangu na kunichagua kuwa Mbunge wao kwa kura nyingi sana, nawashukuru sana. Ninachoomba tushikirikiane kwa pamoja tuondoe umaskini ambao kwa kweli uko mwingi sana katika Jimbo langu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mapendekezo haya yaliyoletwa mbele yetu na Waziri wa Fedha ni mazuri na kwa kweli tunahitaji tumsaidie kuboresha ili aje na Mpango utakaokuwa mzuri zaidi kwa nia ya kuondoa umaskini katika nchi yetu. Kwa sababu hiyo, yangu zaidi ni ushauri katika maeneo machache ambayo nimeona yakiboreshwa pengine tutakuja na Mpango mzuri zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ni eneo zima na falsafa nzima ya uchumi wa viwanda. Napata picha kwamba mapendekezo haya yameogopa kuja na mpango mkubwa zaidi ya mapendekezo haya yaliyopo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, unapozungumza kuwa na uchumi wa viwanda nilitegemea nione mapendekezo mazito zaidi ya viwanda vitakavyotukwamua ili uchumi huu sasa kweli uitwe uchumi wa viwanda, lakini humu ndani sikuona sana. Nimeona viwanda vinavyozungumzwa ni vile vilivyobinafsishwa, vichache ambavyo havionekani moja kwa moja kama kweli tumedhamiri sasa kwenda kwenye uchumi wa viwanda. Pia nimeona hata teknolojia inayozungumzwa humu inazungumzwa teknolojia nafuu na ya kati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi tukitaka tujifananishe na wanyonge wenzetu wale, tutabakia hapa hapa. Yupo Mheshimiwa Mbunge mmoja ameeleza kwamba kuna wakati tulifanana na nchi kama za Malaysia, leo hii wenzetu wametuacha sana, wao sasa wanakuwa wafadhili. Ni lazima tutoke hapa tulipo na sisi tuzungumze kwa nguvu zote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo nashauri, kwa nini kwa mfano Serikali isichukue model kama ya China. China ya sasa hivi walifanya uwekezaji mkubwa sana miaka ya 1990. Wali-phase out viwanda vyao vile vilivyokuwepo wakati ule. Viwanda vyao vingi havikuwa na efficiency kubwa katika uzalishaji, wakavi-phase out. Wakachukua technology kutoka nchi za Magharibi na wakaingia kila sekta wakafanya uwekezaji mkubwa sana. Hivyo ndivyo viwanda vinavyozalisha sasa hivi ambavyo vinaifanya China iwe hii tunayoijua leo. Nashauri na sisi tufanye hivyo, tusiogope.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tufanye maamuzi ya uhakika kabisa ya makusudi, yatakayotuwezesha tutoke hapa. Tutafute teknolojia, tutafute mashine ili tuwe na viwanda ambavyo ni vya kisasa, tuwekeze humo. Returns zitakuja baada ya miaka 10, 20, lakini tukienda kiunyongeunyonge kama tunavyoonekana kwenye mapendekezo haya, tutaendelea ndugu zangu kuwa bado tuna tatizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, labda nizungumzie upande wa miundombinu iliyoelezwa. Miundombinu ni muhimu sana katika nia nzima ya kutaka kutoka kwenye umaskini lakini pia kujenga uchumi wa viwanda. Kama walivyosema wenzangu, miundombinu ya barabara, mathalani bado haijagusa sehemu nyingi ya kuwatoa hawa maskini ambao ndio tunawazungumzia sasa hivi. Kwenye Jimbo langu ni tatizo kubwa sana pamoja na kwamba ni potential areas za kuleta uzalishaji sana hasa kwenye mambo ya kilimo. Yapo maeneo ya Kongwa yanalima sana, Waheshimiwa Wabunge wengi mna mashamba yenu kule, lakini njia mbaya sana, barabara hakuna, hizi ni sehemu za uzalishaji, unaziachaje bila miundombinu ya namna hiyo, haiwezekani!
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazungumzia viwanda vitakavyokwenda kwenye eneo kama hilo la kilimo kutumia malighafi ya mazao kuweza kusindika na kuondoa tatizo la ajira kwa vijana wetu wengi. Hivyo, nashauri, barabara hizi ziende kwenye sehemu za vijiji, walipo watu, kwenye sehemu za uzalishaji, huko ndiko tuweke misisitizo. Nazungumzia maeneo ya kwangu kule, kama Kisaki, Mvuha na Uponda, hizo ni sehemu ambazo ni potential lakini hazina barabara pia na Bwira Juu, Bwira Chini, kote huko.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tuzungumzie suala la umeme. Umeme wamejitahidi sana, lazima tuwapongeze. Nampongeza sana Mheshimiwa Profesa Muhongo, lakini tunayo maporomoko madogo madogo. Kwangu kule yapo maporomoko ya maji ya Mlulu katika Mto wa Kibana, Kijiji cha Lugeni. Ni potential kutoa megawatt nadhani moja, ambayo ni lilowatts 1000. Tukiweza kujenga uwezo wetu kwa vijiji vya namna hiyo vyenye maporomoko, tukawekeza kule, tutawasaidia sana hata wakazi wa kule, hata watu wa vijijini kule. Kwa hiyo, nashauri sana Serikali iangalie miradi kama hiyo pia iipe umuhimu mkubwa kuliko kuendelea kutegemea umeme ghali ambao tunatumia kwa ajili ya hawa wanaotumia mafuta.
Mheshimiwa Mwenyekiti, labda nizungumzie pia tatizo kubwa la ng‟ombe. Ng‟ombe tunawahitaji na viwanda tunavihitaji, lakini niishauri Serikali, moja ya njia ya kuondoa tatizo hili la migogoro ya wafugaji na wakulima kwa sasa hivi ni kuwekeza katika viwanda, hata kama vidogovidogo, kwenye maeneo hayo yenye matatizo ili wafugaji wasikae sana na ng‟ombe zao na kukosa malisho. Nitafurahi sana kama Mheshimiwa Waziri wa Kilimo utakapofika wakati wake akaja kutueleza mkakati ambao unatekelezeka wa kuondoa tatizo hilo once and for all.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nizungumzie suala la viwanda vidogo vidogo, kwa sababu uchumi wa viwanda, nazungumzia uchumi wa viwanda kwa nia ya kuondoa umaskini kote. Tunahitaji kuwa na viwanda vidogo vidogo kwa kila Jimbo. Hii itasaidia ku-address tatizo la ajira kwenye Majimbo yetu na kwangu kule tayari nimeshatenga maeneo manne kwa ajili ya kuanzisha viwanda hivyo. Nitashukuru sana kumsikia Waziri wa Viwanda, muda utakapofika, atatusaidiaje kushawishi na kuweka viwanda vidogo vidogo katika maeneo ya kwenye Jimbo langu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)