Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021

Hon. Daniel Baran Sillo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021

MHE. DANIEL B. SILLO – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA BAJETI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa fursa hii niweze kuhitimisha hoja yangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote niweze kuwapongeza sana Wabunge wote waliochangia na kwa bahati nzuri wote wameunga mkono hoja. Kwa hiyo, hatuna hoja ya kujibu, tunawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge na tunawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini yameongelewa mengi wamechangia Wabunge wapatao kumi kwenye Kamati ya Bunge ya Bajeti, ambao ni Mheshimiwa Subira Mgalu, Mheshimiwa Josephat Kandege, Mheshimiwa Issa Mtemvu, Mheshimiwa Shally Raymond, Mheshimiwa Dkt. Faustine Ndugulile, Mheshimiwa Ali King, Mheshimiwa Luhaga Mpina, Mheshimiwa Esther Matiko na Mheshimiwa Reuben Kwagilwa pamoja na Mheshimiwa Tarimba Abbas. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yako mengi yamezungumzwa naomba nisiyarudie yote lakini nitoe msisitizo kwa mambo machache. La kwanza, ni mahitaji ya fedha za dharura kwa ajili ya barabara za vijijini imefanyika tathimini inatakiwa Shilingi bilioni 111.3, ili kurejesha hali ya mawasiliano katika barabara zetu vijijini. Kwa hiyo, tunaomba tena Serikali ijielekeze kuhakikisha kwamba hili linafanyika ili watanzania, waweze kuendelea na huduma mbalimbali za wawasiliano kwa maana ya usafiri na usafirishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili ni kufanya marejeo kwenye viwango vya Mfuko wa Jimbo. Mfuko huu wa Jimbo fedha hizi za miaka 20 iliyopita leo hii mfuko wa cement ni shilingi 18,000 mpaka shilingi 25,000 lakini wakati ule ulikuwa shilingi 10,000 mpaka shilingi 15,000. Kwa hiyo, naomba sana Serikali ifanye marejeo ili kuongeza fedha za Mfuko wa Jimbo liendane na hali halisi ya uchumi wa leo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine kubwa ni kununua cargo scanners kwenye mipaka yetu. Tuna mipaka kama tisa mikubwa tumeenda Namanga pale hakuna cargo scanner, msururu wa mabasi, wa malori ni mkubwa sana na gharama ya usafirishaji inakuwa ni kubwa sana. Kwa hiyo, tuiombe sana Serikali iweze kununua cargo scanners, kwa ajili ya kusaidia mizigo kutoka lakini pia itaongeza mapato ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni ajira kwa TRA upungufu wa staff wa TRA umefanya walipakodi wengi kutokufikiwa hasa kwenye maeneo ya Tax Audit pamoja na Block Management. Tax Audit ni truly for voluntary tax compliance kwa hiyo, kuna umuhimu mkubwa sana wa TRA kuajiri wafanyakazi wa kutosha ili sasa waweze kufanya Tax Audit pamoja na Block Management ili ku-enhance voluntary tax compliance.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni bima ya afya kwa wote. Watanzania wanaotumia bima leo ni chini ya asilimia 20 kwa hiyo, kuna haja kubwa sana Serikali ikajielekeza ikaleta Sera na Sheria, ili sasa Watanzania waweze kuingia kwenye bima ya afya kwa wote ili kuwasaidia Watanzania kupata huduma za afya katika maeneo yote.

Mheshimiwa Naibu Spika, imeongelewa habari ya daraja la Tanzanite nadhani Wabunge wamechangia sana kwa nguvu kubwa kabisa. Nadhani ni vyema basi Serikali ikajielekeza ikaangalia umuhimu na uwezekano wa daraja hili kuwa toll bridge ili tuweze kupata fedha kwa ajili ya kuendesha mkopo huu wa Shilingi bilioni 243.8 waliotoa kwenye Serikali ya Korea Kusini.

Mheshimiwa Naibu Spika, mengi yamesemwa lakini hasa hili la TARURA ameongea Mheshimiwa Reuben kwa msisitizo mkubwa sana. Kwa kweli tulitenga bajeti hii ya tozo shilingi bilioni 322, lakini tunapotoa leo dharura shilingi bilioni 111 tumeharibu utaratibu wa bajeti. Naomba Serikali iliangalie hili kwa umakini mkubwa sana ili bajeti yetu iende vizuri, watanzania wapate huduma ambazo wanatarajia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niwapongeze sana Waheshimiwa Manaibu Waziri wote wawili waliochangia, Mheshimiwa Naibu Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara ameongelea habari ya Blue Print. Tunaomba sana Mheshimiwa Naibu Waziri hili mlizingatie sana ili kurahisisha ufanyaji biashara hapa nchini, kupunguza mlolongo mkubwa sana wa taasisi zetu za Serikali. Katika ufanyaji wa biashara na ili biashara ziwe rahisi watanzania wafanye shughuli za kiuchumi waweze kulipa kodi na kuwanufaisha watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Naibu Waziri wetu wa Fedha ameongea habari ya riba kwa wakopaji. Hili kwa kweli waliangalie kwa mfano mikopo kama ya watu binafsi risk ni ndogo sana kwa hiyo, waangalie kwa ukaribu ili watanzania waweze kukopa kutoka benki yao ya biashara. Waweze kuwekeza na shughuli za kiuchumi ziendele walipe kodi kwa manufaa makubwa na mapana ya Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni Ofisi ya mpokeaji wa malalamiko ya kodi Tax Imbursement ni miaka mitatu sasa tumetunga sheria lakini bado haijaanza ofisi hii, malalamiko ya walipa kodi ni mengi sana mtaani. Naomba sana Serikali ijielekeze kuhakikisha kwamba Ofisi hii inaanza ili kupunguza malalamiko ya walipa kodi wetu ili walipe kodi kwa hiari na nchi yetu iweze kwenda mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya nawapongeza sana wote lakini niombe sana wenzetu upande wa Serikali wachukue haya yote maoni ya Wajumbe wa Kamati ya Bajeti; na sisi kama kamati tutaendelea kusimamia na kuishauri Serikali kila hatua ili tuweze kuwa na bajeti bora kwa manufaa mapana ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana na baada ya maelezo haya naomba kutoa hoja ahsante sana. (Makofi)

MHE. ISSA J. MTEMBU: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki.