Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021

Hon. Dr. John Danielson Pallangyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Arumeru-Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia kwenye hoja iliyoko mezani.

Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi nimesimama kuunga mkono hoja zote mbili, ukizingatia pia kwamba mimi ni mjumbe wa Kamati ya PIC, lakini pia nimekuwa wa ili kutoka mwisho kuchangia, kwa hiyo, mengi yameshazunguzwa na Wabunge wenzangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwapongeze sana wenyeviti wote wawili kwa hotuba zao nzuri ambazo zimejaa na zimesheheni kila tulichokuwa tunakihitaji. Lakini pia nikupongeze wewe na Mheshimiwa Spika kwa kuaminiwa na chama chetu na majina yenu yakarudi hapa nasi tukafanya kweli, na sasa hivi ninyi ndio viongozi wa kuu wa huu mhimili muhimu wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nafasi ya pekee sana nitumie nafasi hii pia kumshukuru sana mama yetu na kumpongeza kwa kazi nzuri ambazo Mheshimiwa Rais anawafanyia Watanzania, kwa uongozi mahiri. Kwa kweli amefanya makubwa. Mwaka jana ametengeneza historia kwa Watanzania, madara 15,000 kwenye sekta ya elimu si jambo dogo; lakini pia kule Arumeru Mashariki nasi tulipata madara 70 ambayo kwakweli ametua mzigo mkubwa sana kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, si sekta ya elimu tu, hata sekta nyingine alifanya kazi nzuri mno, zile fedha za UVICO 19 alizotuletea na kuzisambaza kwa uwazi mkubwa zimeweka historia kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hizo salamu za pongezi naomba sasa nirudi kwenye hoja, na nitazungumzia mambo mawili kwa ufupi sana. Nazungumzia changamoto za bodi za wakurugenzi za mashirika na taasisi zetu za umma. Lakini pia nitazungumzia upungufu wa mitaji kwa taasisi hizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumekutana na mashirika kadhaa ambayo yalikuwa na matatizo ya bodi, kwamba bodi haipo na kama ipo composition yake ina matatizo. Kwa mfano EPZA na TIC, na TIC haikuwa na bodi, lakini pia watendaji wakuu na waliokuwa wameshika nafasi zile nyeti walikuwa wanakaimu. Sasa hii kukaimu na kutokuwa na bodi kunafifisha utendaji kazi wa hizi taasisi zetu. Tunaomba Serikali iangalie kwa jicho tofauti kidogo maeneo haya na kuhakikisha kwamba taasisi hizi zinakuwa na utawala ambao ni timilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu upungufu wa mitaji, tulishuhudia kwamba kuna taasisi na mashirika kadhaa ambayo hayana mitaji ya kutosha. Kwa mfano TTCL, TPDC, TADB pamoja na EPZA. Mashirika haya yameanzishwa na Serikali na yalitegemea kuwa funded fully kwa sababu umiliki ni wa Serikali kamili. Mashirika haya, kwa mfano EPZA kwa miaka mitatu Serikali haijatoa fedha. Matunda yake ni kwamba EPZA imekuwa inafanya kazi zake kwa kusuasua. Zone pekee ambayo inaonekana inafanya kazi vizuri ni ya Benjamin William Mkapa iliyoko kule Mabibo, huku kwingine kote wanasuasua na sehemu nyingine kwa sababu wana nguvu ya kisheria ya kuchukua ardhi ya wananchi na kuwafidia, wameshindwa kuchukua lakini wakasababisha taharuki, kwamba wanachukua lakini hatimaye hawapi fedha lakini wameshatia doa kwenye maisha ya wananchi kwamba wananyang’anywa maeneo yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba Serikali itazame vizuri na kuhakikisha kwamba taasisi hizi wakati zinaanzishwa ziwe funded fully, pamoja na TADB lakini tunashukuru na tunaipongeza Serikali kwamba iliweza kutoa shilingi bilioni 208 mwezi Disemba.

NAIBU SPIKA: Malizia Mheshimiwa.

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nimesikia kengele imelia, basi niseme tu kwamba naunga mkono hoja. Ahsante sana.