Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021

Hon. Hamida Mohamedi Abdallah

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Lindi Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, kwanza nianze kwa kukupongeza kwa kuwa Msaidizi wa Spika wa Bunge la Jamhuri wa Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja zote za Kamati mbili ambazo zimewasilishwa. Pia nawapongeza Wenyeviti wote wawili kwa namna ambavyo wameweza kuwasilisha taarifa ya kazi ya mwaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie suala la EPZ ambalo mwanangu pale Mheshimiwa Ester Bulaya amelizungumzia, nami naomba niunge mkono hoja hiyo. Nizungumzie upande wa muundo wa Bodi ya EPZ. Ukiangalia muundo wa bodi namna ambavyo upo utaona kwamba, Kamati nzima ya bodi ina watu ambao ni wazoefu, wamebobea katika taasisi mbalimbali. Utaona ya kwamba wameshindwa kuisaidia EPZ iweze kusonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niwasomee Waheshimiwa Wabunge waweze kujua. Mwenyekiti wa Bodi ni Waziri wa Viwanda na Biashara. Wajumbe wa Bodi; kuna Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango, Katibu Mkuu TAMISEMI, Katibu Mkuu Nishati, Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Kamishna wa TRA, Kamishna wa Ardhi, Kamishna wa TPSF na Rais wa TCCIA.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa utaona namna ambavyo hawa ndugu zetu wanashindwa kuisimamia EPZ. Tunaamini kwamba, watu hawa Serikali iliwateua kwa kuwaona kwamba wangekuwa msaada mkubwa katika mamlaka hii ya EPZ, lakini tunaona namna ambavyo EPZ inashindwa kufanya kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, EPZ ina miaka mitatu mfululizo haijapata fedha kutika Serikali kuu ya matumizi mengineyo. Sasa tunashindwa kuelewa chombo hiki Serikali imedhamiria kuwekeza viwanda mbalimbali ambapo vitazalisha bidhaa ambazo zingeweza kuingia katika ushindani wa masoko ndani ya nchi na nje ya nchi, lakini tunaona kwamba ajira kubwa kwa vijana ingeweza kuwepo katika maeneo haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, EPZ wanashindwa kufanya kazi kwa sababu hawana fedha za kuwekeza katika zones ambazo tayari walishajipanga nazo. Kwa hiyo, naiomba Serikali kuhakikisha kwamba, wanautazama upya muundo wa bodi, waone namna gani wataisaidia EPZ iweze kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie katika suala la viwanda vidogo vidogo (SIDO). SIDO imekuwa msaada mkubwa sana kwetu na tumeona namna ambavyo imewezesha wajasiriamali wengi kuingia katika uwekezaji wa viwanda vidogo vidogo. Mwanzoni tumeona kwamba SIDO ilikuwa inafanya vizuri sana, lakini tunakokwenda SIDO inaonesha sasa maendeleo yake kushuka kwa sababu wanakosa fedha, vyanzo vyao vya mapato ni makusanyo yale ya ndani. Kutoka Serikali Kuu, kinachokwedna ni mishahara tu ya wafanyakazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunaona kuna kila namna sasa Serikali iitazame kwa macho mawili SIDO, kuhakikisha kwamba wanapewa fedha za kutosha ili waende kutoa mafunzo mbalimbali kwa wajasiriamali ili wananchi wetu waweze kuwekeza kwenye viwanda vidogo vidogo. Pia tumeona uchakavu mkubwa katika maeneo ya majengo yao ambayo wanayakodisha. Kwa hiyo, tunaona sasa Serikali ina umuhimu wa kuwasaidia ndugu zetu wa SIDO ili waweze kwenda vizuri na waendelee kutusaidia vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii kumpongea sana Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa namna ambavyo ametutafutia fedha nyingi. Nami Jimboni kwangu nimepata fedha karibia shilingi bilioni 18 kutekeleza miradi ya maji, madarasa kwa maana ya sekta ya elimu, sekta ya afya na sekta ya barabara. Kwa hiyo, tuendelee kumuunga mkono na kumwombea kwa Mwenyezi Mungu ili aendelee kumuimarisha ili aweze kutekeleza mipango yake ya kazi zake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja na ahsante sana. (Makofi)